Jumatatu, 11 Aprili 2022

MLUNDIKANO WA MASHAURI KUWA HISTORIA KANDA YA SHINYANGA

 Na Emmanuel Oguda-Mahakama, Shinyanga

Jitihada zinazofanywa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athuman Matuma katika kumaliza mlundikano wa mashauri ndani ya Kanda hiyo zimeanza kuonekana.

Hali hii imejitokeza hivi karibuni mara baada ya Kikosi kazi ilichoundwa kinachojumusha jumla ya Mahakimu Wakazi mbalimbali kutoka Kanda hiyo kufanikiwa kumaliza mashauri ya mlundikano 54 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu na Wilaya Bariadi.

Hatua hiyo inafuatia Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga kuanza kutekeleza mkakati madhubuti iliyojiwekea wa kumaliza mashauri ya mlundikano (backlog) katika Mahakama zote ndani ya Kanda hiyo.

Mkakati huo ulifikiwa mapema mwezi Machi, 2022 katika kikao kazi kati ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga, Majaji wa Mahakama Kuu na Mahakimu wote wa Kanda hiyo.

Baada ya kumaliza kazi kubwa mkoani Simiyu, leo tarehe 11 Aprili, 2022, kikosi kazi hicho kimehamia katika Mahakama ya Wilaya ya Maswa, ambapo jumla ya mashauri 10 yameanza kusikilizwa.  Miongoni mwa Mahakimu wanaounda kikosi kazi hicho, Mhe. Christian Lugumira na Mhe Enos Misana, wameanza kusikiliza mashauri hayo na wanatarajia kumaliza ndani ya siku 14.

Baada ya kumaliza kusikiliza mashauri hayo ndani ya muda uliopangwa, kikosi kazi cha Mahakimu hao kitahamia Mahakama ya Wilaya nyingine yenye mashauri ya mlundikano na kukamilisha ndani ya muda uliokubaliwa katika jitihada za kuondoa mlundikano ndani ya Kanda ya Shinyanga.

Moja kati ya maazimio yaliyofikiwa katika kikao kazi ni pamoja na kuanzishwa kwa kikosi kazi maalum kwa lengo la kumaliza mlundikano wa mashauri yote ya muda mrefu katika Mahakama zote ndani ya Kanda ya Shinyanga.

Tarehe 14 machi, 2022, timu ya Mahakimu Wakazi wanne kutoka Mahakama za Wilaya Maswa, Kahama, Shinyanga na Meatu ilifika katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu na Wilaya Bariadi kwa ajili ya kuanza kazi ya kuondoa mashauri yote ya mlundikano yaliyopo katika Mahakama hizo.

Katika hatua nyingine, ili kukabiliana na ongezeko au uzalishaji mpya wa mashauri ya mlundikano, Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga imejiwekea mkakati wa ndani wa kumaliza mashauri mahakamani ili kukabiliana na suala la mlundikano.

Mahakama za Mwanzo wamekubaliana kumaliza mashauri ndani ya miezi mitatu toka kufunguliwa hadi kumalizika. Kadhalika Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya zitamaliza mashauri mapya ndani ya miezi sita huku Mahakama Kuu ikijiwekea kumaliza mashauri ndani ya miezi 12.

Kikosi kazi hicho chini ya uongozi wa Majaji watatu wa Mahakama Kuu kinaendelea na jitihada za kumaliza mashauri ya mlundikano katika Mahakama zote kwa muda uliopangwa ili kukamilisha malengo yaliyowekwa ambapo inatarajiwa baada ya muda mfupi Kanda ya Shinyanga itaandika historia ya kuwa na mashauri ya mlundikano sifuri (0).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athuman Matuma.

Mwonekano wa jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni