Jumatatu, 11 Aprili 2022

WATUMISHI MAHAKAMA KATAVI WAASWA KUJIUNGA NA MAHAKAMA SACCOS

 Na James Kapele - Mahakama, Katavi

Watumishi wa Mahakama mkoani Katavi wamehimizwa kujiunga na Chama cha Ushirika cha Akiba na Mikopo cha Mahakama ya Tanzania (Mahakama Saccos) ili kujiwekea akiba na kupata sifa za kukopeshwa mikopo ya aina mbalimbali inayotolewa na Saccos hiyo.

Wito huo umetolewa leo tarehe 11 Aprili, 2022 na Mjumbe wa Usimamizi wa Bodi ya Saccos hiyo, Bw. Ewald Kilawe katika kikao kilichohusisha watumishi kutoka Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi na Mahakama ya Wilaya ya Mpanda.

Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Kilawe amewasihi watumishi wote kuona fahari ya kujiunga na Chama hicho cha ushirika ambacho kinafuata taratibu zote na sheria za nchi na hutoa mikopo yenye riba nafuu kwa wanachama wake ili kuinua vipato vyao, kuwawezesha kiuchumi na baadaye kuwa wajasiriamali wakubwa.

“Hii Saccos ni yetu sote kama watumishi wa Mahakama kwa kuwa inatusaidia katika kumaliza changamoto zinazotukabili, hasa za kifedha. Hii inatokana na ukweli kwamba kwa sasa tunatoa mikopo ya aina tano kwa wanachama ambao tayari wamekidhi vigezo,” alisema.  

Ametaja aina hiyo ya mikopo kama mikopo ya maendeleo, mikopo ya ajira mpya, mkopo wa kiwanja, dharura na hata mkopo wa sikukuu.

Awali  akifungua kikao hicho, Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi, Mhe Fredirick Shayo alitoa rai kwa watumishi kujiunga na Saccos hiyo ili kuepuka kuchukua mikopo katika taasisi nyingine za fedha ambazo riba zake bado zipo juu.

Aidha ameishauri Saccos hiyo kuangalia uwezekano wa kutumia mfumo mzuri ili kuweza kuwavutia wanachama wengi ili kuleta mafanikio zaidi ya kuanzishwa kwa chama hicho cha ushirika.

“Zipo Saccos katika taasisi nyingine ambazo zimefanikiwa sana, angalieni namna mnayoweza kufanya ili kuwavutia wanachama wengi kujiunga ili Saccos yetu ifanye vizuri zaidi. Mnaweza hata kufanya vikao vya  mara kwa mara na wanatumishi hata kupitia Video conferencing ili kuwahamasisha zaidi,” alisema Mhe. Shayo.

Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi, Mhe Fredirick Shayo (aliyesimama katikati) akiongea na watumishi wakati wa kikao hicho. Aliyeketi kushoto ni Afisa utumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi Bw, Ayoub Nyalobi.


Mjumbe wa usimamizi wa bodi ya chama cha ushirika cha akiba na mikopo, Mahakama Saccos Bw, Ewald Kilawe (aliyesimaman kulia) akifafanua jambo katika kikao hicho Katavi.


Sehemu ya watumishi waliohudhuria kikao hicho.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni