Jumanne, 21 Juni 2022

TUME YA UTUMISHI MAHAKAMA YASISITIZA USIMAMIZI IMARA WA MAADILI

 Na Lydia Churi- Tume ya Utumishi wa Mahakama

Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama kusimamia kikamilifu maadili kwa kuwa kamati hizo zina umuhimu mkubwa katika utawala wa sheria na uhuru wa Mahakama.

Akizungumza na wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama wa Mkoa wa Mtwara pamoja na Wilaya zake katika ziara ya Tume ya Utumishi wa Mahakama iliyoanza mkoani humo, Prof. Juma amesema Mahakama haiwezi kuwa na uhuru na nguvu endapo itakuwa ikikumbana na changamoto za kimaadili.

“Tukiondoa changamoto za kimaadili tutaweza kuimarisha uhuru wa Mahakama na kutoa uamuzi unaoheshimika na wananchi katika mashauri mbalimbali yanayofikishwa mahakamani”, alisema Mwenyekiti wa Tume.

Mwenyekiti huyo amewataka wajumbe wa Kamati hizo kuwaelimisha wananchi katika maeneo yao umuhimu wa Kamati za Maadili ili wazifahamu na kuzitumia katika kuwasilisha malalamiko yao ili waweze kupata haki zao za msingi. Aidha amewaomba wajumbe hao pia kusimamia maadili ya wadau wengine katika sekta ya sheria na Mahakama ambao wako katika mnyororo wa utoaji haki.

Mwenyekiti huyo wa Tume ya Utumishi wa Mahakama alisema kunapokuwa na changamoto za ukiukwaji wa maadili wananchi kuihukumu Mahakama kwa kuwa ndicho chombo chenye jukumu la msingi la kusimamia mnyororo wa utoaji haki hivyo ni vema wadau wengine wa utoaji haki wakazingatia suala la maadili wanapotekeleza majukumu yao.

“Haki haianzii mahakamani, inaanzia tangu mwananchi anapotoa taarifa ya uhalifu katika kituo cha polisi na endapo taarifa hiyo haitatolewa kwa usahihi, ndiyo mwanzo wa haki kutotendeka”, alisema Mwenyekiti huyo. 

Awali akizungumza na Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, Prof. Juma aliwapongeza watumishi hao kwa kuendelea kutoa huduma bora na kuwezesha kupungua kwa malalamiko dhidi ya rushwa.

Alisema kwa mujibu wa taarifa kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini, idadi ya malalamiko hayo imepungua. Aliongeza kuwa kupungua kwa malalamiko yanayohusiana na rushwa kunaonesha kuwa hali ya kimaadili kwa watumishi wa Mahakama imeimarika.

Naye Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustapher Siyani amewashauri Wakuu wa Mikoa na Wilaya nchini kutumia majukwaa waliyonayo kuwaelimisha wananchi kuhusu uwepo wa Kamati za Maadili na namna ya kuzitumia kuwasilisha malalamiko yao dhidi ya vitendo vilivyo kinyume na maadili ya Maafisa wa Mahakama.

“Viongozi hawa katika ngazi za mikoa na wilaya wanapopata fursa ya kuzungumzia ajenda za kitaifa kama vile Sensa, anuani za makazi na kadhalika, tunawaomba pia watumie fursa hiyo kutoa elimu kuhusu Kamati za Maadili,” alisisitiza Kamishna huyo. 

Wakati huo huo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Dkt. Elieza Feleshi ameishauri Mahakama ya Tanzania kuendelea na mpango wake maalumu wa kujenga maadili kwa wanafunzi wa shule za sekondari na vyuo vya elimu ya juu wanaosoma fani ya sheria kwa lengo la kupata wanasheria wenye maadili mema na viongozi waadilifu hapo baadaye.

Wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama wako ziara katika mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma yenye lengo la kuimarisha Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama katika ngazi za mikoa na wilaya. Wajumbe wa Tume ni pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Wajumbe wengine wawili wanaoteuliwa na Rais.
Wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama ngazi ya Mkoa na Wilaya wakiwa kwenye Mkutano kati yao na Tume ya Utumishi wa Mahakama uliofanyika jana mkoani Mtwara.
Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza.
 
Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Dkt. Eliezer Feleshi akizungumza wakati wa Mkutano wa Tume na Wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama ngazi ya Mkoa na Wilaya jana mkoani Mtwara.
Wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama ngazi ya Mkoa na Wilaya wakiwa kwenye Mkutano wa Tume jana mkoani Mtwara. Kulia ni Mkuu wa wilaya ya Mtwara Bw. Dunstan Kyobya.

Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Bi. Enziel Mtei (kulia) akiwa kwenye Mkutano wa Tume na Wadau wa Utoaji haki jana mkoani Mtwara. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe. Eliamani Isaya Laltaika na katikati ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Sharmila Sarwatt.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni