Jumanne, 21 Juni 2022

ZIARA YA TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA YALETA NEEMA LINDI

 Na Faustine Kapama– Mahakama, Lindi

Ziara ya Tume ya Utumishi wa Mahakama katika Ukanda ya Kusini mwa Tanzania imeingia siku ya pili ambapo leo tarehe 21 Juni, 2022 imetembelea Mkoa wa Lindi kuzungumza na watumishi na wadau na Kamati za Maadili, hatua ambayo imeleta neema kwa wananchi katika Mkoa huo, hususani ujenzi wa majengo ya kisasa ya Mahakama kwa ngazi zote.

Tume hiyo chini ya Mwenyekiti wake, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma imeanza kwa kukutana na Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe.  Zainab Telack ambaye aliwakaribisha Makamishna na wajumbe wote na kuwaeleza fursa lukuki zinazopatikana katika eneo lake la utawala.

“Nitumie fursa hii kuwakaribisha mkoani Lindi, karibuni sana. Niliambiwa angalau utalala Lindi leo, sasa nimesikia kidogo kidogo kwamba hamlali. Mtaifahamu lini Lindi? Mgelala ili mjue Lindi siyo porini. Lindi inafunguka, ina madini yote mnayoyajua isipokuwa almasi na dhahabu. Kwa hiyo ni fursa pekee mkikaa Lindi ili kuona fursa mbalimbali zilizopo,” alisema.

Mwenyekiti wa Tume huyo alimshukuru Mkuu wa Mkoa kwa kuitangaza vyema Lindi, hususani fursa zilizopo katika eneo lake, hatua ambayo viongozi wa Mahakama wanapaswa kuiga katika kutangaza uboreshaji mzuri wa huduma  unaofanyika. Jaji Mkuu amemuhakikishia Mkuu wa Mkoa huyo kuwa Mahakama ya Tanzania itajenga Mahakama Kuu ya kisasa ili kushughulikia migogoro itakayojitokeza kutokana na kukua kwa uchumi Lindi.

Baada ya ukaribisho huo, wajumbe wa Tume walielekea katika ukumbi maalumu uliokuwa umeandaliwa kwa ajili ya kukutana na watumishi wa Mahakama Lindi, wajumbe wa Kamati za Maadili za Mkoa na Wilaya na baadaye wadau mbalimbali katika mnyororo wa utoaji haki. Katika mikutano hiyo, viongozi mbalimbali wa Mkoa na Wilaya walipata nafasi ya kutoa maoni yao na ushauri wenye lengo la kuboresha huduma za utoaji haki kwa wananchi.

Wakuu wote wa Wilaya ndani ya Mkoa wa Lindi wameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa uboreshaji wa huduma za utoaji haki ikiwemo kujenga miundombinu ya majengo ya kisasa na pia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) katika shughuli mbalimbali za kimahakama. Viongozi hao wakashauri pia uwezekano wa kujenga nyumba za makazi kwa Mahakimu ambao wamewaelezea kuwa wanafanya kazi nzuri katika maeneo yao.

Katika mikutano hiyo,  Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara, Mhe. Zainab Mruke alipata nafasi ya kujibu baadhi ya hoja zilizoibuliwa na wajumbe na kubainisha kuwa kwa sasa kuna majengo kadhaa ya Mahakama ndani ya Mkoa huo yanayojengwa na mengine yataanza kujengwa kuanzia mwaka wa fedha ujao, yaani kuanzia Julai, 2022.

“Mahakama inafanya uboreshaji mkubwa sana, nchi ni kubwa na mahitaji ni mengi. Hivyo tunachofanya tunagawa kidogo kidogo,”alisema. Naye Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, ambaye pia ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel alikata kiu ya wajumbe alipotangaza kuwa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kitajengwa Lindi kuanzia mwaka wa fedha ujao, taarifa ambayo ilipokelewa kwa makofi na furaha.

Baada ya kufanya mikutano hiyo, ujumbe wa Tume ulielekea katika eneo ambalo kuna jengo la kisasa la Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi, ambalo limekamilika na muda wowote litakabidhiwa kwa viongozi wa Mahakama kwa ajili ya kuanza kutumika.

Tume ya Utumishi ya Mahakama imeundwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Ibara ya 112 kwa lengo la kusimamia mambo muhimu yanayohusu Mhimili wa Mahakama. Wajumbe wa Tume hiyo ni pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania (Mwenyekiti), Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji moja wa Mahakama ya Rufani anayeteuliwa na Rais, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, na wajumbe wengine wawili wanaoteuliwa na Rais.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ndiye Katibu wa Tume hiyo. Baadhi ya kazi za Tume hiyo ni pamoja na kumshauri Mhe. Rais katika uteuzi wa Majaji wa Mahakama Kuu, kumshauri Rais kuhusu masuala ya nidhamu, mishahara na maslahi ya Majaji na kushauri kuhusu ajira za Mahakimu na kusimamia nidhamu yao.

Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kushoto) akipokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe.  Zainab Telack alipowasili ofisini kwake leo tarehe 21 Juni, 2022.
Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akisaini kitabu cha wageni katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi.
Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe.  Zainab Telack akifafanua jambo.
Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akieleza jambo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara, Mhe. Zainab Mruke akiwasilisha taarifa ya utendaji ya Mahakama Lindi.

Sehemu ya viongozi wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika mkutano huo. Kutoka kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki-Temeke, Mhe. Ilvin Mugeta, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Eliamini Laitaika, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mh. Sharmillah Sarwatt, Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Bi. Enziel Mtei na Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Stephen Magoha.

Makamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Zainab Mruke. Kutoka kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald Ndika, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe . Dkt. Jaji Eliezer Mbuki Feleshi na Mawakili wa Kujitegemea Waandamizi, Mhe. Jenoveva Kato na Kalolo Bundala.

Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki-Temeke, Mhe. Ilvin Mugeta akifafanua jambo alipokuwa akieleza mfumo na majukumu ya Tume.
Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, ambaye pia ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akielezea jambo.
Picha mbili za juu na chini ni sehemu ya watumishi wa Mahakama Lindi wakifuatilia masuala mbalimbali katika mkutano wa Tume.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni