Alhamisi, 23 Juni 2022

TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA YAMALIZA ZIARA YAKE KANDA YA KUSINI

 Na Faustine Kapama– Mahakama,         Songea

Tume ya Utumishi wa Mahakama leo tarehe 23 Juni, 2022 imemaliza ziara yake katika mikoa ya Kanda ya Kusini mwa Tanzania kwa kuzungumza na kutoa elimu kuhusu kazi zake kwa watumishi wa Mahakama, wadau mbalimbali katika mnyororo wa utoji haki na Wenyeviti wa Kamati za Maadili wa ngazi katika Mkoa na Wilaya kwa kutembelea  Mkoa wa Ruvuma.

Chini ya Mwenyekiti wake, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Tume hiyo ilianza kwa kukutana na Mkuu wa Mkoa, Brigedia Jenerali Wilbert Ibughe na kufanya naye mazumgumzo mafupi kabla ya kuelekea kwenye ukumbi maalumu ambao ulikuwa umeandaliwa kwa ajili ya kufanya mikutano na wadau mbalimbali.

Katika mikutano hiyo, Mkuu wa Mkoa huyo ameahidi kushirikiana na Mahakama ikiwemo kutoa kipaumbele kwenye mahitaji yake ya kupata viwanja kwa ajili ya makazi ya Mahakimu ili kuuwezesha Mhimili huo wa dola kutekeleza majukumu yake kwa uhuru na ufanisi unaohitajika.

Kikao cha kwanza kiliwahusisha wadau mbalimbali wa Mahakama wakiwemo Jeshi la Polisi, Magereza, Waendesha Mashtaka, Mawakili wa Kujitegemea, Viongozi wa dini, Maafisa Ustawi wa Jamii pamoja na wadau wengine katika mnyororo wa utoaji haki. Baada ya hapo, ulifuata mkutano wa Wenyeviti wa Kamati za Wilaya na Mkoa kabla ya wajumbe wa Tume hiyo kukutana na watumishi wa Mahakama katika Mkoa wa Ruvuma.

Kabla ya vikao vyote hivyo vitatu ambavyo viliongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania kama Mwenyekiti wa Tume kufanyika, washiriki wote walipata burudani safi kutoka kwa Kwaya kabambe ya Mahakama, Kanda ya Songea ambayo iliatumbuza kwa nyimbo mbalimbali, hususani ule unaohamasisha wananchi kushiriki kwenye sensa, wimbo ambao ulionyesha kukonga nyoyo za maafisa na wadau wote waliohudhuria mikutano hiyo.

Katika kikao cha mwisho cha watumishi wa Mahakama, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Songea, Mhe. Yose Mlyambina aliwasilisha taarifa ya utendaji wa Mahakama katika Kanda yake ambayo imesheheni mambo mbaloimbali ya kiutendaji.

Mhe. Mlyambina amewaeleza Makamishna na wajumbe wa Tume, pamoja na mambe mengine, kuwa Mahakama Kanda ya Songea wameendelea kusimamia nidhamu ya watumishi kwa kutoa elimu ya maadili ya Mahakimu na utumishi wa Mahakama.

“Yapo makatazo tuliyoyatoa kupitia vikao vyetu vya ndani na tumeendelea kuonyana na kurekebishana kadiri tuwezavyo. Tumeunda kamati za nidhamu kuanzia ngazi ya Kanda hadi wilaya kwa lengo la kurekebisha tabia za watumishi zinazokinzana na maadili ya kiutumishi,” amesema.

Mhe. Mlyambina ameeleza kuwa Kamati za maadili za maafisa wa Mahakama kuanzia ngazi ya Mkoa hadi Wilaya zinaendelea kutekeleza majukumu yake vizuri ambapo katika kipindi cha mwaka 2021/2022 kamati hizo zimekaa vikao vyote vinavyotakiwa kisheria na taarifa za vikao hivyo zimewasilishwa.

“Aidha, Kanda ya Songea ilitekeleza agizo la kuundwa kwa kamati za nidhamu za watumishi wasio mahakimu kwa kuteua wajumbe na mwenyekiti ni mtumishi kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma. Mpaka sasa hakuna shauri lolote la nidhamu kwa mtumishi lililowasilishwa kwenye kamati hiyo,” amesema.

Akizungumzia hali ya mashauri, Jaji Mfawidhi huyo amebainisha kuwa  Mahakama Kanda ya Songea imeendelea kutekeleza jukumu la msingi na la kikatiba la utoaji haki kwa wananchi kwa Mahakama kupokea, kusikiliza na kutoa hukumu kwa mashauri mbalimbali yanayofikishwa mahakamani kuanzia ngazi ya Mahakama za Mwanzo hadi ngazi ya Mahakama Kuu Kanda ya Songea.

Amesema katika usikilizaji wa mashauri kuanzia Januari hadi Juni, 2022, Mahakama Kuu Kanda ya Songea na Mahakama za chini yake kwa mwezi Desemba 2021 kulikuwa na mashauri ya madai 324 yaliyobaki na yakafunguliwa mashauri 930, mashauri 955 yalimalizika na mashauri 299 yamebaki.

Mhe. Mlyambina amesema kuwa kwa upande wa mashauri ya jinai, kwa mwezi Desemba mashauri ya jinai 803 yalibaki, mashauri 1849 yalifunguliwa, mashauri 1992 yaliamuriwa na mashauri 632 yamebakia.

Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi ya Mahakama, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwaaga watumishi wa Mahakama Kanda ya Songea baada ya mkutano wa Tume na watumishi hao leo tarehe 23 Juni, 2022.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Songea, Mhe. Yose Mlyambina akiwasilisha taarifa ya utendaji wa Mahakama katika Kanda yake.
Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki-Temeke kinachoshughulika na mashauri ya mirathi, ndoa na talaka, Mhe. Ilvin Mugeta akiwapitisha watumishi kwenye mada inayohusu muundo na majukumu ya Tume.
Picha ya juu na chini ni sehemu ya watumishi kutoka Kanda ya Songea wakimsikiliza Jaji Mugeta.

Kwaya ya Mahakama Kanda ya Songea ikitumbuiza washiriki wa mkutano wa Tume.
Meza kuu ikiongozwa na Mwenyekiti wa Tume na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja. Kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Songea, Mhe. Yose Mlyambina na kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge.
Meza kuu ikiongozwa na Mwenyekiti wa Tume na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na Makamishina wa Tume.
Meza kuu ikiongozwa na Mwenyekiti wa Tume na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na Makamishina wa Tume, Katibu wa Tume na Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma.
Meza kuu ikiongozwa na Mwenyekiti wa Tume na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na Sekretarieti ya Tume.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni