Jumatatu, 4 Julai 2022

‘MPANGO MKAKATI AWAMU YA KWANZA UMESOGEZA HUDUMA ZA MAHAKAMA KARIBU NA WANANCHI’

Na Tiganya Vincent-Mahakama, Dodoma

 Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amesema Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania na Programu ya Uboreshaji wa Huduma katika awamu ya kwanza ya utekelezaji umefanikiwa kuimarisha miundombinu na kusogeza huduma za utoaji haki karibu na wananchi. 

Amesema hivi sasa miundombinu ikiwemo ya majengo na ile ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano imeboreshwa ndani ya Mahakama, jambo lililowasaidia wananchi wengi kupata huduma za haki katika mazingira rahisi na kwa gharama nafuu. 

Mhe. Prof. Juma alisema hayo Jana Jijini Dodoma alipokutana na Timu ya Benki ya Duniani iliyofika Ofisi kwake Kujitambulisha na kuelezea juu ya kuwasili nchini kwa ajili ya kutembelea miradi iliyotekelezwa katika awamu ya kwanza kwa ufadhili wa mkopo wa Benki hiyo wenye masharti nafuu na maandalizi ya utekelezaji wa awamu ya pili. 

Alisema miradi iliyotekelezwa awamu ya kwanza inawiana na malengo ya Benki ya Dunia ya kuhakikisha kuwa miradi inayotekelezwa inaboresha utoaji wa huduma za Mahakama inasaidia katika  kupambana na  umaskini pamoja na kudumisha usawa wa kijinsia. 

Jaji Mkuu alisema yaliyotokana na utekelezaji wa mpango wa uboreshaji wa utoaji wa huduma za Mahakama nchini awamu umesababisha wapokee kutoka kwa Taasisi ya Bretton Woods kwa kufikia malengo ya mradi huo. 

Kiongozi wa Timu ya ujumbe wa Benki ya Dunia Christine Owuor alisema wamewasili nchini Tanzania kwa ziara ya kikazi ya wiki mbili ya kukagua utekelezaji miradi yenye thamani ya Dola za Marekani milioni 65( bilioni 141 za Kitanzania ) ambazo zilikuwa ni kwa ajili ya uboreshaji wa utoaji wa huduma kwa Mahakama.

Alisema Timu hiyo imeshapitia miradi inayoendelea katika Mkoa wa Kigoma, Tabora na Morogoro na inatarajia kuendelea katika Mkoa wa Kagera, Dar es salaam na Arusha ili kuona utekelezaji wake. 

Kiongozi huyo alisema katika miradi ambayo wameshapitia Tanzania imefanya vizuri kiasi ambacho nchi nyingine zinatakiwa kutembelea miradi hiyo kwa ajili ya kujifunza jinsi ya kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama kwa wananchi. 

Aidha, Bi Christine aliongeza kuwa Ujumbe huo pia unafuatilia kuangalia maandalizi ya jinsi Tanzania ilivyojiandaa katika utekelezaji wa awamu ya pili ya uboreshaji wa utoaji wa huduma kwa Mahakama ya Tanzania. 

Serikali ya Tanzania hivi karibuni ilisaini mkataba wa mkopo wa masharti nafuu wa jumla ya Dola za Marekani milioni 90 ( Tshs bilioni  200) na Benki ya Dunia ili kutekeleza awamu ya pili ya Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Utoaji Haki unaolenga kuboresha ufanisi na uwazi wa upatikanaji haki kwa wananchi kwa urahisi zaidi.

 Mkataba huo ulisainiwa baada ya Benki ya Dunia baada ya kuridhishwa na utekelezaji mzuri wa awamu ya kwanza ambao ulileta uboreshaji kadhaa katika mfumo wa Mahakama ya Tanzania katika suala la miundombinu na utoaji wa huduma. 

"Matarajio yetu ni kuona kwamba Mradi ujao utawawezesha watu waliombali wanapata huduma za Mahakama katika mazingira ya karibu na kwa wakati (…) tunafurahishwa na Mahakama kwa kutumia teknolojia habari na mawasiliano wakati wa kusikiliza na kutoa uamuzi wa mashauri mbalimbali," alisema. 

Mkuu wa Kitengo cha Uboreshaji cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dk Angelo Rumisha alisema katika awamu ya pili ya mradi, Mahakama ina mpango wa kujenga Mahakama Kuu katika kila Mkoa pamoja na kuongeza idadi ya Mahakama za Mwanzo nchini kote. 

Alisema katika utekelezaji wa awamu ya kwanza ya  uboreshaji wa miundombinu na utoaji wa huduma kwa Mahakama ulipelekea Benki ya Dunia kuitunuku tuzo kufuatia mageuzi makubwa ndani ya Mahakama.

Mhe. Dk. Rumisha aliishukuru Benki ya Dunia kwa kuendelea kuonesha imani kwa Tanzania na kuongeza awamu ya mkopo wenye masharti nafuu ambao utaendeleza juhudi za kusogeza huduma za utoaji haki karibu na wananchi.

1.   

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma( katikati) akiongea na Ujumbe Benki ya Dunia ambao uko nchini kwa ajili ya kutembelea miradi ya awamu ya kwanza ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania wa kuboresha huduma. Picha ya chini akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Ujumbe huo wa Benki ya Dunia.

Picha ya juu na chini ni sehemu ya Ujumbe kutoka Benki ya Dunia.


  Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma(wa tano kutoka kulia) akiwa katika picha ya pamoja jana jijini Dodoma na Ujumbe Benki ya Dunia ambao uko nchini kwa ajili ya kutembelea miradi ya awamu ya kwanza ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania wa kuboresha huduma.

(Picha na Tiganya Vincent-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni