Jumanne, 5 Julai 2022

NEEMA YAJA MAWAKILI KUTOKA ZANZIBAR

 Na Faustine Kapama, Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ameahidi kushughulikia changamoto inayowakwamisha Mawakili kutoka Tanzania Visiwani kufanyakazi Tanzania Bara baada ya kuhitimu Skuli ya Sheria Zanzibar.

Mhe. Prof. Juma ametoa ahadi hiyo leo tarehe 5 Julai, 2022 alipokutana na Baraza la Uongozi wa Skuli ya Sheria Zanzibar ambalo wajumbe wake walifika ofisini kwake jijini Dar es Salaam kwa lengo la kujitambulisha.

Ahadi hiyo ya Jaji Mkuu inafuatia ombi liliowasilishwa kwake na Mwenyekiti wa Baraza, Mhe. Mbarouk Salim Mbarouk, ambaye ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania kuona nanma ya kuwasaidia katika suala hilo ambalo huulizwa mara kwa mara na wanafunzi na wadau mbalimbali wa sheria.

Jaji Mbarouk alisema wanafunzi na wadau huwauliza ni vipi skuli hiyo itashauliana na uongozi wa Mahakama ya Tanzania kuona namna ya kuwawezesha wanafunzi wanaomaliza Skuli ya Zanzibar kufanya kazi Tanzania bara.

“Hivi sasa lipo sharti la sheria kwamba Wakili kutoka nje ya Tanzania Bara lazima awe amefanya kazi miaka mitano kabla ya kuruhusiwa kufanya kazi Tanzania Bara. Sharti hili limekuwa likiwavunja moyo wanafunzi waliopo Skuli na wanaotarajia kujiunga katika miaka ya baadaye" alisema Jaji Mbarouk.

Akijibu hoja hiyo, Mhe. Prof. Juma alisema kuwa suala la Mawakili wa Zanzibar kuja Tanzania Bara kufanyakazi sio jambo baya kwani hiyo ni njia mojawapo ya kuwajengea uwezo kwa kuwa watakutana na changamoto mbalimbali za kisheria ambazo zitawafanya wawe wazuri zaidi.

 "Maombi yenu yote hasa hili sharti la Mawakili kutoka Zanzibar waweze kuruhusiwa kufanya kazi Tanzania Bara, nadhani (jambo hili) siyo baya, kama tunaruhusu Mawakili kutoka nje ya Tanzania kufanyakazi kwa urahisi kwa nini tuwazuie wanaotoka Zanzibar," Jaji Mkuu alisema.

Aidha, Prof. Juma aliuomba uongozi wa Skuli hiyo kuwajenga uwezo wanafunzi kwa kuwapa mafunzo ya ziada nje ya taaluma yao ya sheria ikiwemo masomo ya biashara hususani katika uchumi wa bluu ili wakikosa kazi wawe na chakufanya, na pia katika masuala ya sayansi na teknolojia, ikiwezekana watafute ujuzi nje ya nchi kwa kuzingatia hali ya ajira kwa sasa inatisha.

"Kuwajengea uwezo kutawapa nafasi ya ushindani katika upatikanaji wa ajira na hasa ikizingatiwa kwamba Zanzibar sasa ipo katika uchumi wa bluu, hivyo ni vizuri kuangalia namna gani wanaweza kufanya kazi katika maeneo ya uwekezaji na biashara, wakijenga uimara katika eneo hilo hata Mawakili kutoka Tanzania Bara watakuja kujifunza Zanzibar, naona nyinyi mna nafasi kubwa zaidi," alisema Jaji Mkuu.

Awali akielezea historia fupi ya Skuli ya Sheria Zanzibar, Mhe. Mbarouk alisema kuwa Skuli hiyo ilianza kazi rasmi mwaka 2021 baada ya uteuzi wa Mkuu wa Skuli na Baraza kupitia Sheria Namba 13 ya 2019 kufuatia aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein kuunda Kamati ya Wataalam iliyofanya utafiti wa awali wa kuundwa kwa Skuli ya Sheria Zanzibar.

Jaji Mbarouk alizitaja baadhi ya kazi kubwa za Skuli hiyo kwa mujibu wa sheria kama kuwafundisha wanasheria kuwa Mawakili, kutoa elimu endelevu katika sekta ya sheria, kutoa mafunzo ya wasaidizi wa sheria, kutoa mafunzo ya sheria kwa mahitaji ya sekta za sheria, kufanya utafiti na ushauri elekezi na kutoa machapisho na kusambaza ili kuinua ufahamu wa sheria.

Mwenyekiti wa Baraza la Skuli ya Sheria Zanzibar alibainisha kuwa Skuli hiyo imefanikiwa kutayarisha Mtaala na Mpango Kazi wa miaka mitano kupitia msaada wa fedha kutoka Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP). Amesema tayari Skuli hiyo imeingizwa katika bajeti ya Serikali ya mwaka 2022/23 hivyo, wametayarisha kanuni za taaluma na nidhamu na muundo wa taasisi na utumishi.

Wajumbe wengine walioambatana na Mwenyekiti wa Baraza katika utambulisho huo ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza na Jaji wa Mahakama Kuu Zanzibar, Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim, Mhadhiri Mwandamizi ambaye pia ni Jaji wa Mahakama Kuu Zanzibar, Mhe. Mshibe Ali Bakari, Mkuu wa Skuli, Dkt. Ali Ahmed Uki, Naibu Mkuu wa Skuli (Utawala), Bw. Khamis Juma Mwalim, Naibu Mkuu wa Skuli (Taaluma), Bw. Msemo Semvua Mavare na wajumbe wa Baraza, Prof. Mohammed Makame Haji, Hanifa Ramadhani Said na Slim Abdallah Said, ambaye ni Rais wa Jumuiya ya Mawakili Zanzibar.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akisisitiza jambo alipokuwa akiongea na Baraza la Uongozi wa Skuli ya Sheria Zanzibar leo tarehe 5 Julai, 2022 ofisini kwake jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. Mbarouk Salim Mbarouk, ambaye ni Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania akieleza kwa ufupi historia ya Skuli ya Sheria Zanzibar mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.
Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Adrean Kilimi akiwakaribisha wajumbe wa Baraza la Uongozi wa Skuli ya Sheria Zanzibar.
Picha ya juu na chini ni sehemu ya wajumbe wa Baraza la Uongozi wa Skuli ya Sheria Zanzibar wakiwa ofisini kwa Jaji Mkuu wa Tanzania.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Skuli ya Sheria Zanzibar, Mhe. Mbarouk Salim Mbarouk.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (watatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti na wajumbe wa Baraza la la Uongozi wa Skuli ya Sheria Zanzibar.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Baraza, Mhe. Mbarouk Mbarouk (wa pili kushoto) na Mkuu wa Skuli na Naibu Wakuu wa Skuli ya Sheria Zanzibar.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (wa nne kutoka kulia) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wote wa Baraza la Uongozi wa Skuli ya Sheria Zanzibar.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kulia) akifurahia jambo na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Skuli ya Sheria Zanzibar, Mhe. Mbarouk Salim Mbarouk.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni