Ijumaa, 12 Agosti 2022

BALOZI SANGA ‘AWAPIKA’ MAKATIBU MAHSUSI KUHUSU UZALENDO, MAADILI

Na Faustine Kapama – Mahakama, Lushoto

Mwanadiplomasia nguli nchini, Balozi Charles Sanga amewasihi Makatibu Mahsusi na watumishi wengine wa Mahakama ya Tanzania kuzingatia uzalendo na maadili mema wanapotekeleza majukumu yao ya utoaji haki kwa wananchi ili kuonyesha dhamira ya kweli katika kuitumikia Tanzania.

Akiwasilisha mada kwenye mafunzo yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kuhusu ‘Uzalendo, Itifaki na Maadili’ ambayo yanajumuisha Makatibu Mahsusi 56 kutoka Mahakama mbalimbali nchini, Mhe. Sanga amesema kuwa uzalendo ni njia pekee inayomwongoza mtumishi katika njia zake sahihi.

“Nawasihi mjitoe nafsi zenu kwa ajili ya nchi na watu wengine. Tumieni nafasi ambazo umepewa na Mungu kwa faida ya watu wengine. Kuna mambo mengine huwa yanashangaza sana, utakuta mtu anamwaga chakula! huu sio uzalendo hata kidogo. Kumwaga chakula siyo uzalendo. Jifunze tabia ya kumaliza chakula,” Mhe. Sanga aliwaambia watumishi hao wa Mahakama.

Amewaambia maana halisi ya uzalendo ni kuwa na moyo uliotukuka upendo kwa nchi na wananchi wake, kuheshimu nembo za nchi kama Wimbo wa Taifa; Bendera ya Taifa; Ngao ya Taifa; Twiga, kuwa na dhamira hai na kuipenda nchi yako kwa moyo wako wote, akili zako zote, kwa nguvu zako zote na upendo kwa nchi kama unavyojipenda mwenyewe.

“Uzalendo unadai daima kuwa mkweli hata kama utajenga maadui, woga ni adui wa maisha. Usifanye kazi kwa woga wala usiwe mwoga kutetea ukweli. Ujasiri utakufanya uweze kufikia malengo yako katika maisha. Fanyeni kazi kwa bidii, kila siku ni siku mpya; usizoee kazi wala usimzoee mtu. Fedha ni matokeo ya kazi na siyo msingi wa kufanya kazi,” amesema.

Balozi Sanga amewakumbusha washiriki wa mafunzo hayo kuwa jamii isiyo na maadili mema na uadilifu ni jamii iliyooza, hivyo akawashauri kujiepusha na ubinafsi, ulafi, uchoyo, chuki, ufisadi, kiburi na majivuno pamoja na hasira na vitendo vyovyote vya rushwa kama rushwa ya fedha, rushwa ya ngono na rushwa ya upendeleo kwa kutumia familia, ukabila, ukanda na undugu.

“Mna wajibu wa kuwa waaminifu kwa nchi; kufanya kazi kwa uadilifu na kwa kuheshimu sheria, kanuni na taratibu bila unafiki. Uaminifu wa kweli unakudai kusema ndiyo au hapana kulingana na uhalisia wa mazingira bila woga au unafiki. Fanyakazi bila kuchoka au kukataa tamaa ili kutekeleza malengo kwa wakati uliopangwa. Uwe na unyenyekevu na upole kuyapokea mapungufu yanayotokea sehemu yako ya kazi bila kutoa visingizio na kujitetea ili uweze kujisahihisha,” amesema.

Awali, Makatibu Mahsusi hao walikutana na Afisa Utumishi Mwandamizi kutoka Utumishi, Bi. Getrude Chiunga, ambaye aliwapitisha kwenye mada kuhusu ‘Maadili na Kanuni za Maadili kwa Utumishi wa Umma’ na kusisitiza kuwa maadili ni msingi wa kila kitu katika utumishi wa umma.

“Mnatakiwa kufanya kazi kwa uadilifu na kuepuka matumizi mabaya ya madaraka. Wewe una wajibika pale ulipo, siyo kiongozi wako. Makatibu Mahsusi tunasemwa sana huko nje kwa vitu vidogo vidogo kama mavazi na tabia mbaya. Mavazi na utanashati katika kutoa huduma unatusaidia kutuaminisha. Hivyo, nawasihi tubadilishe mienendo yetu nje na ndani ya mahala pa kazi,” amesema.

Bi Chiunga akawasihi kuzingatia kanuni za maadili ya utendaji wanapotekeleza majukumu yao kazini, ikiwemo kutoa huduma bora, utii kwa Serikali, bidii ya kazi, kutoa huduma bila upendeleo, kufanya kazi kwa uadilifu, kuwajibika kwa umma, kuheshimu sheria na matumizi sahihi ya taarifa.

“Katika matumizi sahihi ya taarifa, watumishi wa Umma wanapaswa kuzingatia Sheria ya Nyaraka Na.3 ya Mwaka 2002, kuzingatia Mwongozo wa  Matumizi  Sahihi na Salama ya TEHAMA Serikalini wa mwaka 2017, ikiwemo kuepuka matumizi ya anuani za barua pepe katika mawasiliano ya Serikali na kuepuka matumizi ya mtandao kutuma nyaraka zote za siri,” amesema.

Akawahimiza pia kujali muda wa kazi na kufika kazini mapema na kwa wakati, kuondoka baada ya kukamilisha kazi na siyo tu baada ya muda wa kazi kuisha, kutulia ofisini na kufanya kazi, kuwa tayari kufanya kazi kwenye kituo chochote cha kazi unachopangiwa, kufanya kazi kwa ufanisi na kukamilisha majukumu na kutumia utaalamu, ujuzi na maarifa kuongeza tija kazini.

Hata hivyo, Bi Chiunga amekemea uvujaji wa siri za Serikali kupitia vyombo vya habari na njia nyingine, ukiritimba katika upatikanaji wa taarifa kwa vyombo vya habari, wananchi na watumishi ambazo wanapaswa kuzijua na kuficha kwa makusudi taarifa ambazo umma au watumishi wenzao wana haki ya kuzijua.

Mwanadiplomasia nguli nchini, Balozi Charles Sanga akisisitiza jambo alipokuwa anawasilisha mada kuhusu Uzalendo, Itifaki na Maadili mbele ya Makatibu Mahsusi 56 kutoka Mahakama mbalimbali nchini wanaohudhuria mafunzo katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).

Afisa Utumishi Mwandamizi kutoka Utumishi, Bi. Getrude Chiunga akiwasilisha mada kuhusu Maadili na Kanuni za Maadili kwa Utumishi wa Umma kwenye mafunzo hayo.

Sehemu ya Makatibu Mahsusi 56 (picha mbili juu na mbili chini) wanaohudhuria mafunzo IJA wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa na wawezeshaji.

Sehemu nyingine ya Makatibu Mahsusi 56 (picha mbili chini) wanaohudhuria mafunzo IJA wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa na wawezeshaji.


Bi Emiliana Mayiku (anaye angalia kamera) ni miongoni mwa Makatibu Mahsusi 56 wanaohudhuria mafunzo hayo.

Sehemu nyingine ya Makatibu Mahsusi 56 (picha mbili juu na mbili chini) wanaohudhuria mafunzo IJA wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa na wawezeshaji.

Sehemu nyingine ya Makatibu Mahsusi 56 (picha mbili chini) wanaohudhuria mafunzo IJA wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa na wawezeshaji.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni