Alhamisi, 11 Agosti 2022

MWANASAIKOLOJIA USO KWA USO NA MAKATIBU MAHSUSI LUSHOTO

·Awafunda kujikubali, kuwa waaminifu

Na Faustine Kapama – Mahakama, Lushoto

Mafunzo ya siku tano ambayo yamewaleta pamoja Makatibu Mahsusi 56 kutoka Mahakama mbalimbali nchini yameingia siku ya tatu leo tarehe 11 Agosti, 2022 ambapo Mwanasaikolojia, Bi. Sadaka Gandi amewaasa kujikubali, kujitambua na kujiona kuwa wao ndiyo sura ya Mahakama, hivyo wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa kujiamini na kuzigatia uaminifu wa hali ya juu.

Akiwasilisha mada kwenye mafunzo hayo yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kuhusu ‘Uthabiti, uaminifu na uvumilivu mahali pa kazi,’ Bi Gandi  amewashauri watumishi hao kujibeba wao wenyewe, kujikubali kwa namna gani ni muhimu katika ofisi na kuacha kufanya uamuzi kwa hisia bila kupima matokeo yake kwa wale wanaowahudumia katika mnyororo mzima wa utoaji haki mahakamani.

“Nyinyi ni sura ya Mahakama. Nawashauri msijichukulie rahisi rahisi, ni watu muhimu sana mahala pa kazi. Ikiwa mawasiliano yako ni duni utakuwa una uwezo mdogo wa hisia. Wewe ndiye unayepeleka hisia ya ofisi kwa watu. Hivyo, kama huna nguvu ya kujibeba utajiona umezaliwa na bahati mbaya. Chukua hatua na uhakikishe kuwa uko juu,” Mwanasaikolojia Ushauri Nasaha na Mtindo wa Maisha amesema.

Amewaambia washiriki hao wa mafunzo kuwa changamoto wanazokabiliana nazo wanapotekeleza majukumu yao ni za kawaida, hivyo wanapazwa kisimama wao kama wao na kubeba thamani waliyonayo, kwani kwa kufanya hivyo wanaweza kufanya kazi zao bila kuteteleka. Akawashauri pia kuzingatia uaminifu na mara zote kumfikiria mwajiri wao kwanza badala ya nafsi zao.

“Kuna watu wengine wanapenda kuumiza wenzao ili wapate nafuu. Ukikutana na watu wa aina hiyo ofisini kaa nao mbali. Ni muhimu kuvumilia, lakini ni vizuri zaidi kujua kitu gani cha kuvumilia,” alisema. Akawakumbusha watumishi hao kuwa hakuna mtu aliyeumbwa na Mungu na akili ya kihisia, bali yote yanayotokea yanatokana na kujifunza kutoka kwa watu wengine.

Bi Gandi akasema, “Hakuna aliyezaliwa mmbea duniani, tunajifunza. Thibiti hisia zako, utakuwa kwenye matatizo kama hutaweza. Ukiamua kitu fulani kiwe kizuri, kitakuwa tu. Unavyoitazama dunia ndivyo unavyochangamana nayo. Kama moyoni mwako kuna giza, ndivyo dunia utakavyoiona. Jambo la msingi zingatia mipaka yako na mara zote jiulize kama unaridhika kuwa kazini kwako.”

Amesema mfumo wa Mahakama unahitaji watu wenye mtazamo wa watu wazima na waliokomaa kwa vile mtazamo wa mtu mmoja unaweza kuathiri kila mtu katika taasisi na mfumo uliopo unaweza kuathiri utamaduni wa shirika na pia mitazamo ya wafanyakazi.

“Kuimarisha mitazamo chanya ya mahali pa kazi kutaleta manufaa kwa mwajiri na mfanyakazi na jambo la msingi itaongeza tija, ustawi wa wafanyakazi kwenye kilele chake na msisimko mzuri kwa ujumla ambao watu hufurahia kuwa mahali pa kazi,” Bi Gandi amesema.

Jana jioni tarehe 10 Agosti, 2022, Makatibu Mahsusi hao walipitishwa na Afisa TEHAMA Mwandamizi wa Mahakama, Bw. Allan Machella kwenye mada kuhusu matumizi ya teknolojia ya kisasa mahakamani, hatua ambayo ina jukumu muhimu katika kuhakikisha dhamira, dira na mipango ya kimkakati inatekelezwa vyema kupitia uboreshaji wa kisasa wa shughuli za kimahakama.

Aliwaambia washiriki kuwa teknolojia ya habari hutengeneza fursa na changamoto kwa pamoja ambazo zinahitaji kueleweka kikamilifu ikiwa Mahakama ya Tanzania italazimika kufaidika na kile ambacho teknolojia ya habari inatoa.

Katika mafunzo yanayoendelea, mada zingine zilizowasilishwa leo zinahusu ‘Maadili na Kanuni za Maadili kwa Utumishi wa Umma’ iliyowasilishwa na Afisa Utumishi Mwandamizi kutoka Utumishi, Bi. Getrude Chiunga na ‘Uzalendo, Itifaki na Maadili’ iliyowasilishwa na Balozi Charles Sanga.

Mwanasaikolojia, Bi. Sadaka Gandi akiwasilisha mada kwenye mafunzo yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto leo tarehe 11 Agosti, 2022 ambayo yamewaleta pamoja Makatibu Mahsusi 56 kutoka Mahakama mbalimbali nchini. 

Afisa Utumishi Mwandamizi kutoka Utumishi, Bi. Getrude Chiunga kuhusu Maadili na Kanuni za Maadili kwa Utumishi wa Umma katika mafunzo hayo.
Balozi Charles Sanga akiwasilisha mada kuhusu Uzalendo, Itifaki na Maadili kwenye mafunzo hayo yanayowaleta pamoja Makatibu Mahsusi 56.


Sehemu ya Makatibu Mahsusi (picha mbili juu na mbili chini) wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa kwenye mafunzo hayo.


Sehemu ya Makatibu Mahsusi (picha ya juu) wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa kwenye mafunzo hayo. Picha ya chini ni mmoja wa washiriki wa mafunzo akiangalia picha za mavazi wanayotakiwa kuvaa kazini watumishi wa umma kwa mujibu wa Waraka wa Utumishi Na. 6 wa mwaka 2020.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni