Ijumaa, 12 Agosti 2022

MAHAKAMA SPORTS MPIRA WA MIGUU DAR ES SALAAM YAIBAMIZA TBS

Na Faustine Kapama-Mahakama

Timu ya mpira wa miguu ya Mahakama Sports, Kanda ya Dar es Salaam jana tarehe 11 Agosti, 2022 imefanikiwa kuibuka mshindi kwa bao 1-0 dhidi ya timu ya TBS katika mechi nzuri ya kirafiki iliyochezwa kwenye Viwanja vya Shule ya Sheria kwa Vitendo (Law school) iliyoko Mikocheni jijini Dar es Salaam.

Goli pekee hilo na la ushindi lilifungwa na mshabuliaji hatari wa Mahakama Sports Ghulam Katwila baada ya kupenyezewa pasi muruha kutoka kwa Winga machachari Charles Mwakapimba, maarufu kwa jina la Mwaisa mtu MMBAD katika dakika ya 16 ya mchezo kipindi cha kwanza.

Mchezo huo ulianza majira ya saa kumi na nusu jioni kwa timu zote kushambuliana kwa zamu na kulikuwepo na kosa kosa za hapa na pale. Hata hivyo, Mahakama Sports waliweza kuitumia vizuri nafasi waliyoipata katika dakika hiyo ya 16 ya mchezo na kufanikiwa kupachika bao hilo.

Kupatikana kwa bao hilo kuliamsha ari ya wachezaji wa pande zote mbili, huku vijana wa Mahakama Sports wakitandaza kandanda safi. Isingekuwa umakini wa kolikipa wa Timu ya TBS, Mahakama Sports ingeweza kujipatia magori mengi zaidi katika kipindi hicho.

Baada ya kosa kosa nyingi, wachezaji wa Timu ya TBS wakacharuka kama nyuki na kuanza kulishambulia lango la Mahakama Sports  na kufanikiwa kupata penati katika dakika ya 44 ya mchezo, baada ya beki wa Mahakama Sports Club Joseph Nchimb, kwa jina maarufu Mjomba kuunawa mpira akiwa katika harakati za kuuokoa ndani ya 18.

Hata hivyo, TBS wakashindwa kuukwamisha mpira kwenye nyavu baada ya penati hiyo kuokolewa na golikipa mahili wa Mahakama Sports Spear Mbwembwe.  Hadi timu zote zinaenda mapunziko, Mahakama Sports ikatoka kifua mbele kwa ushindi huo wa bao moja.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi kwa timu zote mbili kushambuliana kwa zamu. Wachezaji wa timu zote walishindwa kutumia vizuri nafasi walizokuwa wanazitengeneza na hadi dakika 90 zinaisha Mahakama Sports Club 1 na TBS 0.

Kikosi cha Mahakama Sports kiliundwa na Spear Mbwembwe, Nasoro Mwampamba, Gisbert Chentro, Omari Mdakama, Robert Tende Mwantimwa, Chilemba Hassan, Ghulam Katwila, Fidelis Choka, Charles Mwakapimba na Joseph Nchimbi.

Katika hatua nyingine, Timu ya Mahakama Sports ya Mpira wa Netiboli kutoka Kanda hiyo ilitoana jasho na TBS na kupoteza kwa taaaabu kwa vikapu 17- kwa 28. Kikosi cha Mahakama Sports kiliundwa Bahati Sultan, Agness Mwanyika, Tausi Mwambujhule, Rhoida Makasi, Edith Kanju, Nyangi Kisagenta, Sophia Songolo, Flaviana Jackson, Jamila Kisusu, Jackline Paul na Janevailler.

Michezo hiyo ya kirafiki ni sehemu na mwendelezo wa maandalizi ya michezo ya SHIMIWI inayotarajiwa kufanyika mkoani Tanga kuanzia tarehe 01 hadi tarehe 15 Octoba, 2022.

Akizungumza baada ya michezo hiyo, Kocha mchezaji wa Mahakama Sports Spear Mbwembwe amewapongeza vijana wake kwa mchezo mzuri waliouonyesha katika vipindi vyote na ameridhishwa na matokeo hayo. Hata hivyo amewahimiza kuendelea kufanya mazoezi kwa nguvu ili kuweza kujiandaa vizuri na mashindano yajayo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede ameshukuru kwa timu za Mahakama kwa kupambana na kwa kupata mechi hizo za kirafiki, ambazo ni kipimo sahihi kwao kuelekea mashindano ya SHIMIWI.

 “Tunawaomba wanamichezo wote na watumishi wengine wa Mahakama Mikoa yote huko waliko kuendelea kufanya mazoezi ya pamoja. Safari hii tupo makini sana kwa vile nia yetu ni kutengeneza timu imara zitakazoleta ushindi kwa Mahakama kwenye michezo yote tunayoenda kushiriki,” amesema.

Golikipa wa Mahakama Sports Spear Mbwembwe akidaka penati kutoka kwa mchezaji wa TBS kwenye mchezo wa kirafiki uliochezwa jana tarehe 11 Agosti, 2022 kwenye viwanja wa Law School. Mahakama Sports ilichomoza kwa bao 1-0.

Mchezaji na Golikipa wa Mahakama Sports wakiokoa moja ya mipira ya hatari iliyoelekezwa langoni kwao.
Wachezaji wa Mahakama Sports (picha ya juu na chini wenye jezi nyekundu) wakilisakama lango la wapinzani wao, timu ta TBS  (wenye jezi nyeusi).


Wachezaji wa Mahakama Sports wakitandaza kandanda safi katikati ya uwanja.
Wachezaji wa Mahakama Sports Rhoida Makasi (GK) na Janevailler (wenye jezi nyekundu picha ya juu) wakimzuia mchezaji wa TBS  asifunge goli. Picha ya chini mchezo mkali ukiendelea.



Wachezaji wa Mahakama Sports (juu) na timu ya TBS (picha mbili chini) wakipokea maelekezo kipindi cha mapumziko kutoka kwa walimu wao.



 





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni