Na Faustine Kapama – Mahakama, Lushoto
Mafunzo yanayotolewa na Chuo
cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania yamechangia
kwa kiasi kikubwa kuboresha utendaji kazi kwa watumishi katika maeneo yote ya
utoaji haki, hivyo kupunguza au kuondoa kabisa malalamiko kwa Mhimili huo wa Dola
kutoka kwa wananchi.
Hayo yamebainishwa na
Mkuu wa Chuo cha IJA na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo
alipokuwa anafungua mafunzo ya siku tano kwa watumishi wa Mahakama 56 kwa ngazi
ya Makatibu Muhtasi yaliyoanza kufanyika leo tarehe 9 Agosti, 2022 katika
Chuo hicho.
“Tunaamini na tunaridhika
kuwa mafunzo tunayoyatoa yameboresha sana utendaji wa kazi. Hata wateja wa ndani wanafarijika kwa kiasi
kikubwa, huduma zimeboreshwa kwa maana ya utendaji kazi kati ya sisi wenyewe,
wahudumu wa kawaida, makarani au makatibu muhtasi umeboreka kutokana na mafunzo
ambayo wanapata,” amesema.
Mkuu wa Chuo huyo amebainisha
kuwa inafahamika kwa sasa uondoshaji wa mashauri unafanyika kwa kasi kubwa na
hatua hiyo inatokana na matunda ya mafunzo ambayo wanayatoa kwa kada mbalimbali
ndani ya Mahakama, ikiwemo Majaji na Mahakimu.
“Malalamiko ya watu
kupotezewa haki zao mahakamani yamepungua sana. Rushwa na vitendo vyote ambavyo
vilikuwa vinaichafua Mahakama, kama matumizi ya lugha mbaya, vimepungua kwa
kiasi kikubwa na mahali pengine vimeisha kabisa kutokana na mafunzo ambayo
tumekuwa tunayatoa tangu tulipokuwa tunatekeleza mpango mkakati wa kwanza na
mradi wa uboreshaji awamu ya kwanza,” amesema.
Mhe. Dkt. Kihwelo amewaambia
watumishi hao kuwa kwa muda mrefu Mahakama imekuwa kwenye uboreshaji ambao
unagusa katika maeneo mengi na kubwa
ambalo linaonekana wazi ni lile linalohusu miundombinu ya majengo ambayo
yameboreshwa ili kuwawezesha watumishi kufanya kazi katika mazingira bora.
Mkuu wa Chuo huyo akabainisha
pia kuwa wamekuwa wakitoa mafunzo kwa watumishi wa kada mbalimbali kwa muda
mrefu kwa lengo la kuboresha utendaji kazi ili kuwajengea uwezo katika kutenda
haki kila mmoja kwa nafasi yake na kuna matokeo chanya ambayo yanaonekana
kutokana na hatua hiyo.
“Hivyo lengo la mafunzo
yanayotolewa ni kujaribu kuwajengea uwezo na kubadilisha fikra za watumishi wa
Mahakama ili huduma wanazozitoa mahakamani ziendane na ubora wa majengo ambayo
yanaendelea kuboreshwa,” amesema.
Amewakumbusha washiriki
hao wa mafunzo kuwa wao ni watumishi wa Mahakama ambao jamii inawachukulia kama
Mahakimu ambao kila mmoja hutoa haki kwa namna yake, ikiwemo kutoa taarifa
sahihi kwa mteja anayetaka kujua kesi yake inakuja lini, ambayo pia ni haki ya
mtu kuifahamu.
“Tunawaomba na nyinyi
mkatende haki kwa nafasi yenu ya Katibu Muhtasi. Ukiharibu wewe hakuna mtu
anayejua kuwa ni wewe, yeye anajua ni Mahakama. (Mtu huyo atatoka) mahakamani akiwa
amekasirika na (kulalamika) majengo mazuri lakini huduma ni mbaya. Hivyo, nyinyi
ni kioo cha Mahakama,” amesisitiza.
Mhe. Dkt. Kihwelo anamini
kuna changamoto ambazo watumishi hukumbana nazo wanapotekeleza majukumu yao na
ndiyo maana mafunzo kama hayo hutolewa ili kuwasaidia namna ya kuzikabili.
Akawakumbusha pia kuwa wao ni watumishi wa umma na utumishi wa umma mwisho wa
siku ni kuwasaidia wananachi.
Mkuu wa Chuo huyo
hakuficha furaha yake kwa jinsi Kurugenzi ya Mafunzo inayoongozwa na Mkurugenzi
Msaidizi Bi Patricia Ngungulu ilivyopata washiriki kwenye mafunzo hayo ambao
wametoka katika Mahakama mbalimbali nchini, hatua ambayo inaondoa dhana
kwamba IJA ni ya watu wa upande wa Majaji na Mahakimu tu.
“Chuo chetu ni cha kipekee
kabisa, kuna vyuo vingine vya Mahakama vinatoa mafunzo kwa Majaji na Mahakimu
tu. Lakini sisi tuna bahati kwa kweli, tunatoa mafunzo kwa Majaji, Mahakimu,
wadau na watumishi wengine wote wa Mahakama na ndiyo hilo lingine ambalo
tunalifanya,” alisema.
Akitoa neno la
kumkaribisha Mkuu wa Chuo ili kufungua mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali
Watu wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick amewaambia washiriki hao
kuwa Mahakama imejipanga kuwajengea uwezo watumishi wake katika kada
mbalimbali.
“Hatua hii ni katika utekelezaji
wa azma ya Mahakama kuhakikisha watumishi wake wanajengewa uwezo kwa kuwaendeleza
kwenye kada zao na kuwa na (ujuzi mpana kwenye maeneo yao ya kazi. Jitihada)
hii imeanza na itaendelea taratibu kadri bejeti itakavyokuwa ikiruhusu,”
amesema.
Bi. Patrick amesema kundi
hilo la washiriki wa mafunzo linajumuisha Makatibu Muhtasi 56, ambapo 50
wametoka katika Mahakama mbalimbali za pembezoni katika Mahakama za Mwanzo, Mahakama
za Wilaya na Mahakama za Hakimu Mkazi, huku wengine sita wakiwa ni waajiriwa
wapya.
Amesema watumishi hao
wameitwa ili wakumbushwe upya majukumu yao juu ya shughuli za Ukatibu Muhtasi,
utunzaji wa kumbukumbu, usimamizi wa ofisi na mawasiliano ya kiofisi kwa
ujumla, uzalendo na protokali, mipango ya Mahakama na uboreshaji, mwelekeo wa
Mahakama kwa sasa katika mapinduzi ya viwanda kuelekea Mahakama Mtandao na
matumizi ya TEHAMA.
Washiriki pia watapitishwa kwenye maeneo mbalimbali kuhusu utoaji wa huduma kwa ujumla kwa kuzingatia mkataba wa huduma kwa mteja, masuala ya saikolojia na ushauri, usalama serikalini na upekuzi, kudhibiti msongo wa mawazo pamoja na mambo mengine.
Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo akiwasili kwenye ukumbi.
Meza Kuu ikiongozwa na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi kutoka katika Mahakama ya Wilaya Lushoto.
Meza Kuu ikiongozwa na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa secretarieti ya mafunzo hayo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni