Jumanne, 16 Agosti 2022

JAJI WA MAHAKAMA KUU DIVISHENI YA KAZI ATETA NA WADAU

Na Emmanuel Oguda - Shinyanga

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe Katarina Mteule hivi karibuni alikutana na wadau wa Mahakama hiyo Kanda ya Shinyanga na kusisitiza ushirikiano ili kuharakisha utoaji wa haki kwa wananchi.

Mhe. Revokati alieleza lengo kuu la kukutana na wadau wa Mahakama ya Kazi ili kupata maoni yao pamoja na kushirikiana katika usimamizi wa Sheria za Kazi na Haki Kazi kwa ujumla.

“Zamani Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi ilisikiliza mashauri ya kazi ambapo Jaji alikuwa akitoka Makao Makuu Dar es Salaam, lakini kwa sasa Mahakama Kuu zote katika ngazi ya Kanda zinaendesha mashauri hayo kwa kutumia Majaji wa Mahakama hizo,” alisema.

Jaji Mteule alieleza katika kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga kuwa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi imeamua kukutana na wadau kama hatua ya Mahakama ya Tanzania kutekeleza Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania wa miaka mitano (2022/2021 – 2024-2025) unaosisitiza kurudisha imani kwa wananchi na ushirikishwaji wa Wadau.

“Zipo changamoto nyingi kwenye mashauri ya kazi, kupitia kwenu wadau wetu yapo mambo ambayo tutashirikishana kwa pamoja ili tuendelee kuongeza ufanisi katika usikilizwaji wa mashauri hayo,” alisema.

Awali akifungua kikao hicho, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athumani Matuma alipongeza jitihada za Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi kwa kuona umuhimu wa kushirikisha wadau katika usikilizaji wa mashauri ya kazi. “Tukitatua migogoro ya kazi kwa haraka na kwa haki tutakuza uchumi wa Nchi,” alisema.

Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi. Mhe. Elizabeth Nyembele alisisitiza utunzaji mzuri wa majalada, hasa kwenye ofisi za Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), kwa kuainisha mwaka shauri lilipomalizika ili kuondoa usumbufu pale linapohitajika Mahakama Kuu, hatua itakayosaidia kumaliza shauri husika kwa wakati.

Kwa upande wao, wadau walipongeza hatua ya Mahakama hiyo kuwashirikisha katika kujadili kwa pamoja masuala mbalimbali yanayohusu changamoto katika usikilizaji wa mashauri ya kazi. Wadao hao wameshauri iangaliwe namna ya kurasimisha na kutoa mwongozo au kanuni zitakazodhibiti wawakilishi binafsi katika mashauri ya kazi ili yamalizike kwa wakati.

Wadau walioshiriki katika kikao hicho walitoka katika Ofisi ya Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Makatibu wa Vyama vya Wafanyakazi Mkoa na Chama cha Mawakili Shinyanga.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Katarina Mteule (kushoto) akiongea na wadau alipokutana nao katika ukumbi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Shinyanga kujadili masuala mbalimbali yahusuyo mashauri ya kazi. Kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga Mhe. Elizabeth Mkwizu. 
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athumani Matuma akifungua kikao hicho. Aliyekaa ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Katarina Mteule.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Elizabeth Nyembele akisikiliza kwa makini hoja mbalimbali kutoka kwa wadau wa Mahakama ya Kazi wakati wa kikao hicho.
Katibu wa Chama cha Wafanyakazi (TAMICO) Kanda, Bw. Lucas Bujashi (kulia) akichangia jambo wakati wa kikao hicho.
Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga Mhe. Elizabeth Mkwizu akifafanua jambo wakati wa kikao hicho.
Viongozi wa Mahakama wakisikiliza kwa makini maoni ya wadau wakati wa kikao hicho.
Msuluhishi au Muamuzi kutoka Tume ya Usuluhishi na Uamuzi Shinyanga Bi. Magreth Kiwara akichangia jambo wakati wa kikao hicho.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni