Jumamosi, 6 Agosti 2022

MAHAKAMA YAISHUKURU SERIKALI KWA KUWAWEZESHA UNUNUZI MABASI MANNE

Na Tiganya Vincent-Mahakama

Mahakama ya Tanzania imeishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapa fedha za kununua magari manne kwa ajili ya usafiri kwa watumishi wake.

Pongezi hizo zimetolewa jana tarehe 5 Agosti, 2022 jijini Dar es salaam na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabliel wakati akipokea magari hayo kutoka kwa Mkurugenzi wa Ununuzi na Ugavi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Charles Chale.

Akipokea magari hayo, Mtendaji Mkuu  alisema yatapelekwa katika Kanda nne za Mahakama ambazo ni Morogoro, Shinyanga, Mwanza na Musoma.

Prof. Ole Gabriel alisema bado kuna baadhi ya Kanda zenye changamoto ya usafiri lakini watumishi ambao bado hawajapata magari wasivunjike moyo kwani ushirikiano wa Serikali na Mahakama ni mzuri na yapo magari mengine yatakayonunuliwa.

Alisema jitihada za Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Profesa Ibrahim Juma ni kuona Watanzania wanapata haki kwa wakati, hivyo kama watumishi wakiwa na usafiri wa uhakika itasaidia kutekeleza azima hiyo.

Prof Ole Gabriel aliwataka watumishi na madereva watakaokabidhiwa magari hayo kuyatunza ili yaweze kufanya kazi kwa muda mrefu na kusaidia katika uendelezaji wa mnyororo wa utoaji haki kwa wakati.

Kwa upande wake, mmoja wa madereva hao watakaoendesha magari hayo, Bw. Juma Chikoti alisema usafiri huo utaongeza morali na tija kwa watumishi kwa kuwa watafika kwa wakati kazini huku akiahidi kulitunza.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabliel (kushoto) akizungumza mara baada ya kupokea mabasi wanne  kutoka kwa Mkurugenzi wa ununuzi na ugavi wa Mahakama ya Tanzania Charles Chale jana tarehe 5 Agosti, 2022 jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Ununuzi na Ugavi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Charles Chale akitoa maelezo mafupi wakati wa kukabidhi mabasi wanne kwa  Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabliel.

(Picha na Tiganya Vincent-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni