Alhamisi, 4 Agosti 2022

RAIS WA JMAT TAIFA AKUTANA NA VIONGOZI WAPYA WA JMAT MWANZA

 Na Stephen Kapiga- Mahakama, Mwanza

Rais wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (JMAT) Taifa, Mhe. John Kahyoza leo tarehe 4 Agosti amekutana ofisini kwake katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki jijini hapa na viongozi wapya wa Chama hicho, tawi la Mkoa wa Mwanza waliochaguliwa hivi kwa ajili ya kujitambulisha.

Viongozi hao ni Mhe Monica Ndyekobora ambaye ni Mwenyekiti wa JMAT Mwanza pamoja na Mhe. Godfrey Ndege ambaye ni Katibu wa JMAT Mwanza. Katika ziara hiyo, Rais wa JMAT Taifa, ambaye pia ni mlezi wa Chama hicho Kanda ya Mwanza alipokea malengo ya viongozi hao wapya katika kipindi cha uongozi wao.

Baadhi ya malengo waliyowasilisha ni kuwawezesha wanachama wa JMAT, tawi la Mwanza kuielewa JMAT kupitia vikao vyao, kutoa mada mbalimbali za kisheria wakati wa vikao, kutoa elimu ya kisheria kwa wananchi na vikundi mbalimbali, kushiriki katika utalii wa ndani na kuandaa miradi mbalimbali kwa ajili ya kutunisha mfuko wa Chama.

Akizungumza na viongozi hao, Mhe. Kahyoza aliwashukuru kwa ujio wao na kwa mikakati mizuri waliojiwekea. “Binafsi niwapongeze kwa kuchaguliwa kwenye nafasi hizo na niwapongeze kwa mikakati na malengo ambayo mmejiwekea kama tawi ambayo naamini mnaweza kuyatekeleza kwa ufanisi Zaidi,” alisema.

Amewashauri viongozi hao kuunda kamati ya elimu itakayokuwa inaratibu zoezi zima la mada na nini kitachoenda kufundishwa katika vikao vyao au kwa jamii. Alisema ni vizuri kuwepo kwa kamati nyingine kama kamati ya maafa ili kuweza kuwasaidia wanachama pindi wapatapo maafa.

Pia aliwashauri namna bora ya kuangalia michango ya wanachama katika tawi lao ili kuweza kukidhi malengo hayo waliojiwekea ikiwemo na hayo aliyowashauri.

 



Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza ambaye pia JMAT Taifa na mlezi wa JMAT Kanda ya Mwanza akieleza jambo kwa viongozi wa tawi.


Mwenyekiti wa JMAT Mwanza, Mhe Monica Ndyekobora (Juu) na Katibu wa JMAT Mwanza, Mhe. Godfrey Ndege (chini). 



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni