Alhamisi, 4 Agosti 2022

UTENDAJI MAJAJI MAHAKAMA YA RUFANI WAPAA

Na Faustine Kapama-Mahakama, Morogoro

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 4 Agosti, 2022 amefungua Mkutano wa Nusu Mwaka wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na kuwapongeza Majaji wote kwa mafanikio ya utekelezaji wa Mpango Mkakati Wa Miaka Mitano (2016-2021) na Programu ya Uboreshaji, hatua ambayo imechochea kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama.

Akizungumza na Majaji, wajumbe na wageni wengine waalikwa katika siku ya kwanza ya Mkutano huo wa siku mbili unaofanyika katika Hoteli ya Nashera mjini hapa, Mhe. Prof. Juma ameeleza kuwa kuna kazi kubwa ambayo imefanyika katika kutoa huduma za haki kwa wananchi ambapo kiwango cha kuridhishwa na huduma za Mahakama kimepanda kutoka Asilimia 61 (2015) hadi 78 (2019), kwa mujibu wa Utafiti wa Kuridhika wa Watumiaji na Wateja wa Mahakama (Court Users Surveys) za 2015 na 2019.

“Nitakuwa mchoyo wa fadhila endapo sitachukua fursa hii kuwapongeza Majaji wa Mahakama ya Rufani kwa kazi yenu kubwa ambayo imechangia utelezaji wa miaka mitano wa Mpango Mkakati wa Kwanza wa Mahakama na mafanikio katika utekelezaji wa Programu ya Uboreshaji,” alisema Jaji Mkuu ambaye ni Mwenyekiti wa Mkutano huo.

Amebainisha kuwa pamoja na viongozi wa Mahakama kutopata nafasi ya kutafakari mafanikio makubwa waliyopata kutokana na huduma wanazotoa kila siku, wapo wengine nje ya Mhimili wa Mahakama ambao wameyaona mafanikio hayo ambayo yametajwa katika maeneo mbalimbali, ikiwemo kwenye Andiko la Benki ya Dunia lililozaa nyongeza ya mradi wa uboreshaji.

“Benki ya Dunia wametambua mafanikio yetu. Chini ya Vigezo vya Ufanisi (Efficiency Indicators), vigezo hivi vimeonyesha kuwa uboreshaji umeleta usimamizi bora wa mashauri ambao unatoa huduma kwa haraka kwa watumiaji wa Mahakama. Kwa kurahisisha kanuni za uendeshaji wa mashauri, Mahakama imefanikiwa kupunguza hatua nyingi ambazo mashauri hupitia kabla ya kukamilika. Hatua katika taratibu za kimahakama zimepungua kutoka 38 hadi 21,” amesema.

Amesema kuwa kuanzishwa kwa mfumo wa usimamizi wa mashauri kwa njia ya kielektroniki (JSDS2) umetajwa kuwa ni mafanikio yanayoonekana ambapo matumizi ya Video Conference (Mkutano Mtandao) ambayo yamesaidia kusikiliza mashauri ya Wafungwa na Mahabusu na pia kupokea ushahidi wa Mashahidi kutoka nje ya nchi ni mafanikio makubwa. Kadhalika, Jaji Mkuu amesema kuwa kumekuwepo na mfumo imara wa mafunzo na mfumo wa upimaji utendaji kazi ambapo Majaji na Mahakimu wamejipangia idadi ya mashauri ya kusikiliza kila mwaka.

“Vigezo vya kupunguza mlundikano vililenga kushusha mlundikano hadi asilimia 0.05. Ni mafanikio kwa Mahakama kuweza kushusha asilimia hii hadi 0.15. Lengo liliwekwa la kuhakikisha idadi ya siku ambazo shauri linakuwa mahakamani kabla ya kukamilika ishuke hadi siku 350. Lengo hili limefanikiwa kwa vile shauri linadumu mahakamani kwa siku 338, ambazo ni bora zaidi ya lengo la siku 350,” aliwaambia wajumbe wa Mkutano huo.

Jaji Mkuu amesema pia kuwa kuelekea Mahakama Mtandao, Mahakama ya Tanzania imeendelea kuboresha huduma ya utoaji haki kwa wananchi kwa kuimarisha mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), huku akibainisha lengo la msingi ni kufikia Mahakama isiyotumia karatasi (paperless court), hivyo ili kufikia lengo hilo hawana budi kuendelea na maandalizi bila kurudi nyuma licha ya changamoto zinazoweza kujitokeza.

Katika Mkutano huo, Mhe. Prof. Juma aliwakumbusha Majaji hao kuwa kwa nafasi zao mmoja mmoja, au kwa ujumla wao wapo katika kilele (APEX) cha utoaji wa haki ambapo uamuzi wanaotoa una nguvu katika nchi, hivyo akabainisha kila Jaji wa Rufani ni Kiongozi. “Jaji wa Rufani Mstaafu wa Uingereza aliwahi kutoa mada nchini Bahrain kuhusu Judicial Leadership and Reform (Uongozi wa Mahakama na Uboreshaji). Aliyoyasema, yanafafanua nafasi za Majaji katika nafasi za Kiuongozi,” alisema.

Akimnukuu Jaji huyo wa Uingereza, Jaji Mkuu amesema kuwa kazi za Majaji wa Rufani za utoaji haki amezitaja kuwa zinawapa uongozi (leadership) katika kuendeleza sheria, kufafanua sheria, kuongoza katika tafsiri na kuweka ukomo wa mabishano kuhusu tafsiri sahihi ya sheria na pia Majaji wanapojizuia kuingilia kazi za Kibunge ya utungaji wa sheria, wanakuwa wakidhihirisha uongozi.

“Jaji huonyesha uongozi anapotoa tafsiri ambayo inafungua mipaka mipya katika ufahamu wa sheria. Majaji huonyesha Leadership kila wakati wanapoheshimu mamlaka ambayo Katiba na Sheria zimetoa kwa Bunge, Serikali, kwa Taasisi nyingine na hata kwa watumishi wa umma. Kila siku Jaji unaonyesha leadership unaposimamia jalada la shauri ulilopangiwa na unaonyesha leadership ukiwa mahakamani unaposimamia rufani au maombi,” amesema.

Viongozi mbalimbali wa Mahakama ya Tanzania wamealikwa katika Mkutano huo. Miongoni mwa viongozi hao ni  Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mstaafu, Mhe. Edward Rutakangwa na Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala, Bw. Steven Magoha.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza katika Mkutano wa Nusu Mwaka wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania alioufungua leo tarehe 4 Agosti, 2022 mjini Morogoro.
Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija akimkaribisha Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma kufungua Mkutano wa Nusu Mwaka wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania.
Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Kevin Mhina akitoa maelezo mafupi ya utangulizi kuhusu Mkutano wa Nusu Mwaka wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania.
Sehemu ya viongozi wa Mahakama ya Tanzania walioalikwa kuhudhuria Mkutano wa Nusu Mwaka wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania. Juu ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (kulia) na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe na chini kutoka kulia ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma na Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania.
Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji, Msajili pamoja na Naibu Wasajili wa  Mahakama ya Rufani ya Tanzania.
Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (aliyesimama kushoto) na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe.
Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania pamoja na wakurugenzi na wakuu wa vitengo.
Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na Msajili na Naibu Wasajili wa Mahakama ya Rufani.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na wageni wengine waalikwa wa Mkutano.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni