Jumamosi, 13 Agosti 2022

TAIFA LINAWAHITAJI, LINAWATEGEMEA: NAIBU MKUU WA CHUO IJA

Na Faustine Kapama – Mahakama, Lushoto 

Naibu Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Prof. Fatihiya Massawe leo tarehe 13 Agosti, 2022 amehitimisha mafunzo ya siku tano yaliyowaleta pamoja Makatibu Mahsusi 56 kutoka Mahakama mbalimbali nchini kwa kuwahimiza watumishi hao wa Mahakama kufanyakazi kwa bidii na kuzingatia mema na yanayokubalika katika jamii kwa vile Taifa linawahitaji na kuwategemea.

Ametoa rai kwa Makatibu Mahsusi hao kuwa kuzingatia mafunzo na maelekezo yote waliyoyapata na kisha kuyatafsiri kwa kufanya kazi kwa weledi na kwa kiwango cha hali ya juu kwenye vituo vyenu vya kazi. “Ninawahimiza mkafanye kazi kwa bidi kubwa na kwa kuzingatia yaliyo mema na yanayokubalika katika jamii. Napenda mfahamu kuwa Taifa linawahitaji na kuwategemea sana,” amesema.

Naibu Mkuu wa Chuo huyo amewaambia watumishi hao wa Mahakama ya Tanzania kuwa wanapaswa kutambua kuwa kwa kupitia majukumu yao wanashiriki kutoa huduma kwa wateja moja kwa moja na kupitia huduma hizo hujenga imani za wananchi katika Mahakama kwa ujumla.

“Ninaamini mafunzo haya yamewajenga vizuri sana, ni imani yangu kuwa mtazingatia mafunzo haya katika kuboresha utoaji wa huduma kwa mteja kwa kufanya kazi kwa bidi, ufanisi, maarifa na kumjali mteja kila mnapotoa huduma kwake, kwa kuwa mteja ndiye mlipa kodi na ndiye mwajiri,” amesema.

Amewakumbusha pia kutambua kuwa mafunzo waliyoyapata endapo watayazingatia kwa ufasaha yatawatambulisha vema kwa wananchi kwa kuwa wamepewa dozi nzuri ya utendaji wa kazi mzuri, hivyo wataweza kushiriki na kuchangia katika kutekeleza malengo yaliyopo kwenye mpango mkakati na vipaumbele vya Mahakama.

Prof. Massawe anaamini mambo ambayo wananchi wanayoyalalamikia kama vile ucheleweshaji wa huduma, uwepo wa rushwa, huduma kuwa duni, kauli zisizoridhisha, majivuno, matumizi mabaya ya vyeo au jina la Mahakama wataenda kuyaondoa na kusaidia kurejesha imani na mtazamo chanya kwa jamii.

“Nimatumaini yangu kuwa mtakwenda kufanya kazi kwa nguvu moja na ari kubwa kwa lengo la kuleta mabadiliko chanya vituoni. Mwende mkatimize wajibu wenu kwa weledi, ustadi, uaminifu, maadili na nidhamu ya hali ya juu.  Ni matarajio yetu kuwa mtaijenga na kuilinda taswira nzuri ya Mahakama pamoja na viongozi wake. Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto unawatakia utekelezaji mzuri wa majukumu yenu,” amewaasa Makatibu Mahsusi hao.

Akitoa neno la shukurani kwa niaba ya washiriki, Mwenyekiti wa Makatibu Mahsusi hao, Bi Dianess Mwakatundu alieleza kuwa kwa moyo wa dhati wanaupongeza uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kuwapa fursa hiyo adhimu ya mafunzo na wameahidi kutekeleza yale yote waliyojifunza na kuleta mabadiliko makubwa na yenye tija katika vituo vyao vya kazi.

Kabla ya mafunzo hayo kuhitimishwa, Makatibu Mahsusi  hao walipitishwa kwenye mada kadhaa, ikiwemo 'Kuthibiti Msongo wa Mawazo na Jinsi ya kuwa na Hasira kama Mtumishi wa Umma' iliyowasilishwa na Mshauri Mwelekezi, Bw. Geofrey Wawa na kuhusu 'Ujuzi wa Kifedha na Maisha ya Ujasiliamali' iliyowasilishwa na Mkurugenzi na Mshauri Mwelekezi, Bw. James Rhombo.

Jana tarehe 12 Agosti, 2022, washiriki hao wa mafunzo walipitishwa kwenye mada mbalimbali na wawezeshaji mahiri, ikiwemo ‘Huduma kwa Mteja’ iliyowasilishwa na Mhadhiri kutoka Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Dkt. Yustin Bangi na baadaye mada kutoka kwa Naibu Mkurugenzi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi Patricia Ngungulu kuhusu ‘Stahiki na Wajibu wa Mwajiri na Mtumishi katika Utumishi wa Umma.’

Akiwasilisha mada yake, Dkt. Bangi amewaeleza Makatibu Mahsusi hao kuwa tendo la huduma kwa mteja ni endelevu, hivyo huduma wanayotoa inatakiwa iwe rafiki. “Kuna watu wengi wanaogopa kuja mahakamani. Ikitokea nimekuja halafu unanifokea unanipotezea mwelekeo. Ona huruma kwa mwenzio na uvae viatu vya huyo unayemhudumia. Usiwe na upendeleo na kumbuka siyo kila mtu anaweza kuwa Katibu Mahsusi, nyinyi ni watu muhimu sana, nawaomba mzingatie weledi mnapowahudumia wateja wenu,” amesema.

Amewasisitiza kuwa na maarifa ya kutatua matatizo ya wateja wanaofika kupata huduma na kila mteja anayefika mbele yao anatakiwa kutambuliwa, kusikilizwa, kuheshimiwa, kujaliwa na kuhudumiwa.

“Kuna mambo muhimu sana ya kujiuliza hapa. Usafi wako binafsi ukoje; sura zenu ninaonekanaje mnapokutana  na wateja. Sura zenu ziwe za kumkaribisha mteja na akija mteja mbele yako anatakiwa apate kile anachotarajia,” Dkt. Bangi aliwaambia watumishi hao wa Mahakama.

Kwa upande wake Bi Ngungulu amewaeleza washiriki hao wa mafunzo kuwa kila mwajiri au mtumishi anazo stahiki au haki kwa mujibu wa sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali inayosimamia utumishi wa mahakama au umma na kila upande unapaswa kuhakikisha kwamba unazingatia utoaji wa haki au stahiki kwa upande mwingine.

Alizitaja baadhi ya stahiki au haki za mtumishi wa umma kama kupewa nyaraka muhimu zinazohusiana na utumishi wake, kulipwa mshahara au ujira kama ujira wa kazi aliyofanya na kupata likizo na nauli ya likizo kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.

Zingine ni kupata mafao ya hitimisho ya kazi au ajira, kupewa mafunzo ya kujengewa uwezo na kuendelezwa kitaaluma, kupata usalama wa afya na maisha yake katika sehemu za kazi, kupata usalama wa afya na maisha yake katika sehemu za kazi na kulipwa fidia kwa kuumia kazini.

“Hata hivyo ili mtumishi au mwajiri aweze kupewa stahiki au haki anazopaswa kupewa ni lazima atimize wajibu wake kwa mujibu wa makubaliano ya mkataba wake wa ajira. Wajibu ni lazima utekelezwe kwanza ndio stahiki/haki zitatekelezeka,” alisema.

Ametaja sehemu ya wajibu wa mtumishi kama kutekeleza majukumu yake ya kikazi kila siku kulingana na taaluma, fani na kazi aliyoajiriwa nayo; kutimiza malengo ya mwajiri kwa mujibu wa makubaliano na kuzingatia Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo iliyopo mahali pa kazi na kama inavyotolewa na mamlaka mbalimbali za Serikali, kuwa na utii na nidhamu.

Wajibu mwingine ni kufanya kazi kwa kushirikiana na kuaminiana, kujenga na kuimarisha mahusiano mema mahali pa kazi; kuheshimu mipaka ya kazi na miiko; kutoa huduma bora, kufanya kazi kwa bidii, umakini na kwa ufanisi; kutoa huduma bila upendeleo na kuwa mwadilifu katika kazi.

Akataja pia baadhi ya majukumu ya mwajiri ikiwemo kuchukua hatua za kinidhamu kwa makosa ya mtumishi akiwa kazini, kumpa mtumishi majukumu ya kufanya na mpango kazi na kuandaa au kutengeneza na kusimamia uzingatiaji wa sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali ya utumishi.

Majukumu mengine ni kumlipa mtumishi ujira wake kwa kadri ya makubaliano baada ya kutimiza wajibu wake na kwa muda uliokubaliwa; kumjengea mtumishi mazingira wezeshi ili aweze kutekeleza majukumu yake kwa utulivu na ufanisi; kusimamia na kufuatilia utendaji kazi wa mtumishi siku hadi siku na kumuendeleza mtumishi kwenye kada (career) yake.

Naibu Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Prof. Fatihiya Massawe akiwasilisha hotuba leo tarehe 13 Agosti, 2022 kuhitimisha mafunzo ya siku tano yaliyowaleta pamoja Makatibu Mahsusi 56 kutoka Mahakama mbalimbali nchini.

Mratibu wa Mafunzo Mahakama, Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Elia Baha akitoa neno la utangulizi kabla ya kuhitimishwa kwa mafunzo hayo.
Mwenyekiti wa Makatibu Mahsusi, Bi Dianess Mwakatundu akitoa neno la shukurani kwa waandaji wa mafunzo hayo.
Meza kuu ikiongozwa na Naibu Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Prof. Fatihiya Massawe (katikati) muda mchache kabla ya kuhitimishwa kwa mafunzo hayo. Wengine ni Naibu Mkurugenzi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi Patricia Ngungulu (wa pili kushoto), Hakimu  Mkazi Mfawidhi katika Mahakama ya Wilaya ya Lushoto, Mhe. Rose Ngoka (kushoto) na wawezeshaji wa mafunzo, Bw. Geofrey Wawa (wa pili kulia) na Bw. James Rhombo (kulia).

Meza kuu ikiongozwa na Naibu Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Prof. Fatihiya Massawe (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa sekretarieti ya Mahakama na IJA baada ya kuhitimishwa kwa mafunzo hayo.
Naibu Mkurugenzi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi Patricia Ngungulu kuhusu Stahiki na Wajibu wa Mwajiri na Mtumishi katika Utumishi wa Umma katika mafunzo hayo.
Mhadhiri kutoka Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Dkt. Yustin Bangi akisisitiza jambo alipokuwa anawasilisha mada kuhusu Huduma kwa Mteja kwa Makatibu Mahsusi hao.
Mshauri Mwelekezi, Bw. Geofrey Wawa akieleza jamnbo alipokuwa anawasilisha mada kuhusu Kuthibiti Msongo wa Mawazo na Jinsi ya kuwa na Hasira kama Mtumishi wa Umma.
Mkurugenzi na Mshauri Mwelekezi, Bw. James Rhombo akiwasilisha mada kuhusu Ujuzi wa Kifedha na Maisha ya Ujasiliamali katika mafunzo hayo.


Sehemu ya Makatibu Mahsusi 56 (picha mbili juu na mbili chini) wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa na wawezeshaji.

Sehemu nyingine ya Makatibu Mahsusi 56 (picha mbili chini) wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa na wawezeshaji.



Sehemu nyingine ya Makatibu Mahsusi 56 (picha mbili juu na mbili chini)  wakifuatilia mada mbalimbali.


Sehemu nyingine ya Makatibu Mahsusi 56 (picha mbili chini) wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa na wawezeshaji.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni