Jumatano, 21 Septemba 2022

JAJI MKUU AMKABIDHI NYENZO MFAWIDHI MPYA WA MAHAKAMA YA HAKIMU MKAZI KISUTU

Na Paul Mushi – Mahakama, Moshi

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma jana tarehe 20 Septemba, 2022 amemkabidhi Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Ferdnadri Kiwonde nyenzo za kufanyia kazi mara baada ya kumteua kuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu iliyopo jijini Dar es Salaam.

Tukio hilo ambalo lilishuhudiwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani lilifanyika katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi kwa kuwa Jaji Mkuu yuko mkoani Kilimanjaro katika kikao cha kwanza cha Mahakama ya Rufani kinachofanyika katika Masjala ndogo ya Mahakama hiyo Moshi.

Akitoa nasaha na maelekezo baada ya tukio hilo, Mhe. Prof. Juma alisema kukabidhiwa kwa nyenzo hizo ambazo zinaonyesha mamlaka na majukumu ya kazi za Mfawidhi huyo ni matakwa ya kisheria ili kumuwezesha kutekeleza majukumu yake kikamilifu katika Mahakama yake na Mkoa kwa ujumla.

“Nataka usimamizi wa hali ya juu katika mifumo yetu ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), yaani JSDS II, E-filling, E-office kwenye kipindi hiki ambacho Mahakama ya Tanzania inatoka katika matumizi ya karatasi kuelekea Mahakama mtandao. Hakikisha unakagua na kusimamia suala hili ipasavyo,” Jaji Mkuu aliagiza.

Aidha, Mhe. Prof. Juma alimtaka Hakimu Mkazi Mfawidhi huyo kusimamia kikamilifu maadili kwa watumishi wenzake kwa kuwa zoezi la utoaji haki linapaswa kufanywa kwa uadilifu wa hali ya juu.  “Nakutakia kila kheri maana nina imani unajua mifumo yetu yote ya kazi zetu,” alisema.

Naye Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania alimtakia Hakimu Mkazi Mfawidhi huyo utendaji mwema katika majukumu yake mapya na kumtaka kuheshimu imani aliyopewa kuongoza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ambayo ni moja ya Mahakama kubwa na yenye mashauri mengi hapa nchini.

Naibu Msajili huyo aliyekuwa anahudumu katika Mahakama Kuu jijini Dar es Salaam ameteuliwa kuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mara baada ya mtangulizi wake, Mhe. Godfrey Isaya kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Baada ya hafla hiyo fupi, Mhe. Siyani alitembelea maeneo ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi na kufanya mazungumzo na viongozi mbalimbali katika Mahakama hiyo.

 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akimkabidhi nyezo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Ferdnandri Kiwonde kama ishara ya kuanza kutekeleza majukumu yake mapya ya kuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu iliyopo jijini Dar es Salaam.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (kulia) akimshuhudia Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Ibrahim Hamis Juma akisani kwenye nyenzo hizo. Kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Juliana Masabo.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (kushoto) akizungumza na viongozi Mahakama Kuu Moshi (hawapo kwenye picha) katika ofisi ya Jaji Mfawidhi.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akizungumza na watumishi katika Masjala ya wazi ya Mahakama Kuu Moshi.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akiteta jambo na viongozi wa Mahakama, akiwemo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (wa pili kushoto), Jaji Safina Simfukwe (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Kanda, Bw. Donald Makawia (kulia).
(Picha na Paul Mushi-Mahakama, Moshi.)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni