Na Faustine Kapama-Mahakama
Jaji Mkuu wa Tanzania,
Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma jana tarehe 19 Septemba, 2022 alizindua vikao vya Mahakama ya Rufani katika Masjala ndogo Moshi Mkoa wa Kilimanjaro, hatua ambayo imelenga kusogeza
huduma za utoaji haki karibu na wananchi kwa ngazi hiyo ya Mahakama ya juu hapa
nchini.
Akizungumza katika uzinduzi huo ulioashiria kuanza kwa vikao vya Mahakama hiyo, Mhe. Prof. Juma alibainisha faida lukuki kufuatia kuanzishwa kwa Masjala ya Moshi, ikiwemo kutatua changamoto za Masjala ndogo ya Mahakama ya Rufani ya
Arusha, kutatua changamoto za wakazi wa Mkoa wa Kilimanjaro na kutekeleza Mpango
Mkakati wa Mahakama wa kusogeza huduma karibu na wananchi.
“Wakazi wa Mkoa wa Kilimanjaro
sasa watakuwa na huduma (za kimahakama) kuanzia Mahakama za Mwanzo mpaka
Mahakama ya Rufani ndani ya Mkoa na Kanda yao. (Kuanzishwa kwa Masjala hii) kutawapunguzia
gharama na umbali wakazi wa mkoa wa Kilimanjaro,” alisema.
Mhe. Prof. Juma alisema
kuwa Masjala hiyo itatatua changamoto ya mlundikano wa mashauri katika Masjala ya
Arusha. Alisema moja ya changamoto za Moshi ni uwepo wa mashauri mengi ya
madawa ya kulevya ya washtakiwa wanaokamatwa katika Uwanja wa Kimataifa wa Ndege
wa Kilimanjaro yanayowahusu raia wa kigeni na Watanzania.
Alibainisha kuwa baada ya
mashauri hayo kumalizika katika ngazi ya Mahakama Kuu Moshi huwa yanaingia
katika foleni ndefu ya kusubiri kusikilizwa katika Masjala ndogo ya Mahakama ya
Rufani Arusha. “Jambo hili lilizua malalamiko mengi na ya mara kwa mara kutoka
kwa wahusika (wafungwa). Kuanzishwa kwa vikao Moshi kutafanya mashauri hayo
pamoja na mengine yote yasikilizwe kwa haraka,” Mhe. Prof. Juma alisema.
Jaji Mkuu aliongeza, “Kuanza
kwa vikao vya Mahakama ya Rufani Moshi kutasaidia sana kutatua changamoto kubwa
ya mlundikano wa mashauri yanayosubiri kusikilizwa Arusha. Ni hatua kubwa, idadi
ya mashauri yanayosikilizwa Arusha itaongezeka kwa sababu sasa mashauri ya
Moshi yatakuwa yanasikiliziwa Moshi.”
Aidha, Mhe. Prof. Juma alieleza
kuwa kuanzishwa kwa Masjala hiyo kutawapa fursa wananchi wa Kilimanjaro kupata taarifa
muhimu za kimahakama na kisheria kupitia tovuti ya Mahakama, ikiwemo upatikanaji
wa uamuzi ya Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani kwenye TANZLII.
Kadhalika, Jaji Mkuu alibainisha
kuwa uanzishwaji wa Masjala hiyo utapeleka uzoefu wa Mahakama ya Rufani kwa
Mawakili na wadau wa sheria katika Mkoa wa Kilimanjaro ili kusaidia katika
uimarishaji wa ujuzi na ukuzaji wa falsafa ya sheria kwa wadau.
Akizungumza katika halfa
hiyo, Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Emmanuel Mrangu alisema kuwa Moshi
ilitangazwa kama Masjala ndogo ya Mahakama ya Rufani na Gazeti la Serikali 579
la Mwaka 2020 mnamo tarehe 24 Julai, 2020 na baadae Gazeti la Serikali Na. 520
la Mwaka 2022 la tarehe 12 Agosti, 2022.
Alisema hadi kufikia
Septemba, Masjala ndogo ya Moshi ilikuwa na jumla ya mashauri 295 yanayoendelea
na kati ya hayo, mashauri saba ndiyo mashauri yenye umri mrefu zaidi unaofikia
miaka mitano tangu yaliposajiliwa. Mhe. Mrangu alieleza kuwa kati ya hayo saba,
mashauri ya jinai ni sita na shauri moja ni la madai.
“Kwa kipindi cha mwezi
Januari mpaka Septemba 2022, Masjala ndogo ya Moshi imesajili jumla ya mashauri
51 na kati ya hayo, mashauri 30 ni ya madai na mashauri 21,” Naibu Msajili huyo
alisema.
Kuhusu mashauri ya
mlundikano, Mhe. Mrangu alisema kuwa hadi kufikia mwezi Septemba 2022, Masjala
ndogo ya Moshi ilikuwa na jumla ya mashauri ya aina hiyo 62 na kati ya hayo,
mashauri ya madai yalikuwa 16 na mashauri ya jinai yalikuwa 46.
“Kwa idadi ya mashauri 62
ya mlundikano na kwa wastani wa mashauri 33 ambayo hupangwa kwa kikao kimoja,
tutahitaji vikao viwili kumaliza mzigo huo wa mlundikano,” alisema.
Safari ya kusogeza huduma
za Mahakama Kuu Moshi ilianzia Mwaka 1921 wakati utawala wa Wakoloni
walipotunga Kanuni za Masjala ya Mahakama Kuu— High Court Registries Rules,
1921 [GN No. 27/1920]. Kanuni hizi zilianzisha Masjala ya Mahakama Kuu Dar es
Salaam na Masjala za Mahakama Kuu Tanga, Tabora na Mwanza. Masjala ya Tanga
ilihudumia Wilaya za Pangani, Usambara, Moshi na Arusha.
Mpaka kufika mwaka 1993,
wakazi wa mkoa wa Kilimanjaro walikuwa wakipata huduma za Mahakama Kuu jijini
Arusha. Ilipofika mwaka 1993 ndipo Mahakama Kuu Moshi ilianzishwa ili
kuwasogezea huduma wakazi wa Mkoa wa Kilimanjaro.
Kwa upande wa Mahakama ya
Rufani tokea ilipoanzishwa mwaka 1979, wakazi wa Mkoa wa Kilimanjaro wamekuwa
wakipata huduma za Mahakama hiyo katika Masjala ndogo ya Mahakama ya Rufani ya
Arusha. Katika kalenda ya Mahakama ya Rufani ya 2022 iliyotolewa Septemba 2021,
kikao cha kwanza cha Mahakama ya Rufani Moshi kilipangwa kuanza tarehe 19
Septemba hadi tarehe 7 Oktoba, 2022.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni