Na Mayanga Someke, Mahakama-Sumbawanga
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga,
Mhe. Dunstan Ndunguru amewataka watumishi wa Mahakama ya Mkoa Rukwa kutojihusisha na
vitendo vya rushwa na badala yake wazingatie maadili ili waweze kufanya kazi bila
bughudha.
Akizungumza na Watumishi wa Mahakama hiyo hivi karibuni katika
kikao cha pamoja, Mhe. Ndunguru alisema kuwa, tuhuma za rushwa ni muhimu
kuzifuta kwa kufuata maadili ya kazi, kupendana pamoja na kushirikiana huku
akiwasihi watumishi hao kuepuka na kuacha vitendo vya utovu wa maadili ikiwemo
rushwa.
“Rushwa mahakamani inamgusa kila mtumishi wa Mahakama kwa
namna moja au nyingine, hivyo naomba suala hili liachwe maana linachafua
taswira ya Mahakama, mtumishi yeyote atakaejihusisha na vitendo vya rushwa, Mahakama
haitamvumilia,” alisisitiza.
Mbali na hilo, Jaji Ndunguru aliwakumbusha Viongozi wa Mahakama hiyo kuwa na desturi ya kufikisha taarifa muhimu kwa watumishi wa chini yao
mara tu wanapozipata ili taarifa mbalimbali ziweze kufahamika katika
ngazi zote za Mahakama.
“Nataka taarifa ziweze kumfikia kila mmoja wetu katika ngazi
ya Mahakama ili ajue kinachoendelea kwenye Mhimili wa Mahakama, ikiwemo Mpango Mkakati
wa Mahakama” alisema.
Kadhalika; Jaji Mfawidhi aligusia suala la watumishi kutambua
na kuheshimu mipaka kwa kila ngazi ya Mahakama ili kuepuka migongano isiyo ya
lazima.
Mhe. Ndunguru aliongeza kwa kuwasihi watumishi kujitokeza
kwa wingi kwenye programu ya mazoezi ambayo hufanyika siku za Jumatatu, Jumatano
na Ijumaa ya kila wiki katika viwanja vya mahakama kuu Kanda ya Sumbawanga ili kuimarisha
afya zao.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Dunstan Ndunguru akizungumza na Watumishi wa Mahakama ya Mkoa wa Rukwa (hawapo katika picha) katika kikao cha pamoja kilichofanyika hivi karibuni. Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Maira Kasonde na kushoto ni Mtendaji wa Kanda hiyo, Bw. Emmanuel Munda.
Watumishi wa Mahakama ya Mkoa Rukwa wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Dunstan Ndunguru (hayupo katika picha) alipokuwa akizungumza nao katika kikao kati yake na Watumishi hao.
Watumishi
wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Dunstan
Ndunguru.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni