Na Dhillon John, Mahakama
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma ameagiza Watendaji wa Kituo hicho kuandaa Mafunzo ya Huduma kwa mteja mara nyingi iwezekanavyo lengo likiwa ni kuendelea
kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi wanaowahudumia.
Akizungumza mwishoni mwa wiki iliyopita wakati
akifungua Mafunzo ya siku moja ya Huduma kwa Mteja yaliyofanyika katika Ofisi
za Kituo hicho jijini Dar es Salaam, Mhe. Maruma alisema Mafunzo hayo ni muhimu kwa kuwa yanasaidia
kuimarisha utoaji huduma kwa wananchi.
“Mafunzo haya ni muhimu sana na yalikuwa yanasubiriwa
kwa muda mrefu, hivyo ni rai yangu kuwa mafunzo haya yawe yanatolewa mara kwa
mara hata kila baa ya miezi sita ili kukuza utoaji wa huduma kwa mteja,”
alisema Mhe. Maruma.
Akiwasilisha mada
hiyo kwa Watumishi wa Kituo hicho, Mwezeshaji wa Mafunzo, Bw. Remigius Kyaruzi
alisema kuwa, utoaji wa huduma kwa mteja ni njia mojawapo ya kujitangaza hivyo
ni muhimu kwa kila mmoja kufanya jitihada za kubadili mtazamo na kuwa na mtazamo
chanya ili kuweza kuwahudumia wateja kwa namna bora zaidi.
Mkufunzi huyo ambaye pia ni Mtumishi wa Kituo Jumuishi cha
Utoaji Haki Temeke aliongeza kuwa, ni muhimu pia kwa Taasisi kuangalia mbinu mpya
za kujitangaza (Organization branding) ili huduma inayotolewa kwa wateja iweze Kwenda
sambasamba na uboreshaji wa huduma.
Alizitaja njia za kuhudumia wateja ni kwa njia ya ana kwa ana, kwa njia
ya mawasiliano kupitia mitandao
ya kijamii (social media) pamoja na njia ya barua pepe.
Kwa upande wake, Jaji wa Kituo hicho, Mhe. Dkt. Zainab
Mango alisema kuwa, ili Kituo kiwe kizuri ni muhimu kila Mtumishi
kukubali kujifunza na anapokosea inapaswa aambiwe ukweli ili kutorudia kosa na hatimaye kupata matokeo chanya.
Watumishi wa Kituo hicho kwa pamoja waliahidi kubadilika
katika utoaji wa huduma ili Kituo
hicho kiwe mfano wa Taasisi katika utoaji huduma nzuri kwa wateja
wanaowahudumia.
Mafunzo
hayo yalihudhuriwa na Mhe.
Jaji Dkt.
Mango, Jaji wa
kituo hicho, Mhe. Wanjah Hamza,
Naibu Msajili
Mfawidhi wa Kituo hicho, Mtendaji, Bi. Hellen Mkumbwa pamoja na Watumishi wote wa Kituo hicho.
Sehemu ya Watumishi wa Kituo cha Usuluhishi wakiwa katika Mafunzo ya Huduma kwa Mteja 'Customer Care'.
Mwezeshaji wa Mafunzo, Bw. Remigius Kyaruzi akiendelea kutoa mada.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni