Alhamisi, 22 Septemba 2022

JAJI MRUMA: NGUVU YA PAMOJA YAHITAJIKA KUKABILIANA NA UKATILI WA KIJINSIA

 

Na Castilia Mwanossa- (SAUT)

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma amesema jitihada na nguvu za Pamoja zinahitajika kutoka kwa wadau wa ndani na nje ya nchi ili kuweza kukabiliana na ongezeko la vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Ameyasema hayo leo 22 Septemba jijini Dar es salaam alipokuwa kwenye kongamano lililowakutanisha wadau mbalimbali kujadili namna bora ya kushughulikia kesi za ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto wa kike ili kuwawezesha kupata haki.

Aidha, amesema kwamba Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayopambana na Madawa ya Kulevya, Uhalifu na Makosa ya Jinai “United Nations on Drugs and Crime” (UNODC) wamesaidia Mahakama na Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) kuandaa kongamano hilo ili kuwapa weledi wadau mbalimbali wa Haki Jinai dhidi ya wanawake na watoto wenye jinsia ya kike, ambapo jitihada za pamoja zinahitajika ili kukabiliana na tatizo hilo.

Ameongeza kuwa, katika utekelezaji wa haki ya jinai  kundi hili ndilo limekuwa likipata matatizo makubwa ya kufanyiwa vitendo vya udhalilishaji kama vile kubakwa na kulawitiwa hivyo kumekuwa na shida katika uendeshaji wa mashauri ya vitendo hivyo kulingana na sababu mbalimbali kama vile uwoga wa watu walioathirika kujitokeza kutoa ushahidi, ikiwemo  tatizo la jamii kuona jambo hilo ni la aibu na kutolitolea taarifa katika vyombo husika.

“Kuna shida katika upelelezi wa mashauri hayo namna gani wapelelezi waangalie ni vigezo gani ili kuweza kuthibitisha kesi, katika kesi za jinai ili mtu atiwe hatiani lazima shauri lake lithibitishwe bila kuacha kiwango chochote cha mashaka, kukiwa na mashaka yoyote inawezekana labda hiki kinachosemwa si kweli inabidi mtuhumiwa aachiwe.

“Unapokuja kwenye kesi ya udhalilishaji kuna hoja nyingi kwenye upelelezi zinaachwa kwa mfano daktari anaposema huyu mama au mtoto wa kike amebakwa amefikiaje hatima hiyo kuwa amebakwa na kuwa pengine labda uchunguzi wa vina saba (DNA) iwe ni kigezo cha watu waliofanya makosa hayo na kujua kwamba huyu mtu ni kweli aliingiliwa kimwili na hivyo kwa hapa nchini kwetu ni changamoto,” alisema Jaji Mruma.

Aidha, ametoa takwimu kwa mujibu wa taarifa kutoka tovuti ya Benki ya Dunia ambayo imeonyesha kwamba nchini Tanzania asilimia 40 ya wanawake wenye umri wa miaka 15-49 wamefanyiwa vitendo vya ukatili wa kimwili lakini pia asilimia 17 wamefanyiwa vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia na pia alisema wanawake wenye umri kati ya miaka 15-49 ambao ni asilimia 44 wameathiriwa na vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia.

Alibainisha kuwa, asilimia 52 ya wanawake vijijini wanakabiliwa na ugomvi wa kifamilia na mjini ni asilimia 45 na asilimia 30 ya watoto wa kike wanafanyiwa vitendo hivyo kabla hawajafikisha miaka 18.

Kwa upande wake Dkt. Linda Naidoo kutoka Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayopambana na madawa ya kulevya, uhalifu na makosa ya jinai “United Nations on Drugs and Crime” (UNODC), amesema vipimo vya uchunguzi wa vina saba (DNA) vinaweza kutumika kubaini mtu aliyetenda kosa la ubakaji hivyo ni vyema kutumia njia hiyo ili kurahisisha uendeshaji wa mashauri hayo.

Naye Naibu Mkuu wa Chuo Mipango Fedha na Utawala kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) - Lushoto Prof. Fatihiya Massawe amesema wako kwenye kongamano hilo kwa ajili ya kuwajengea uwezo watumishi wa Mahakama ya Tanzania ili kupata ujuzi wa kushughulikia suala hilo na kuziba pengo lililopo kwa kufanya utafiti na kuandaa mafunzo mahususi.

Kwa upande wake Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Zainab Mango amesema kuwa, Mahakama inategemea utendaji kazi wa wadau wengine hasa wanaopeleleza makosa  na wanaokuja kuthibitisha kwa kutoa ushahidi mahakamani, hivyo kama mashauri hayatapelelezwa vizuri wasitegemee muujiza kutoka mahakamani kwa sababu Mahakama inaangalia ushahidi na haiwezi kuibua ushahidi kutoka sehemu nyingine ambazo siyo maalumu kwa ajili ya kutoa ushahidi, kama upelelezi ni mzuri Mahakama haiwezi kumwachia mtu ambaye amepatikana na hatia ya kutenda kosa hilo na itatoa hukumu kwa haki.

Naye Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Susan Kihawa amesema kongamano hilo ni maalum kwaajili ya kuangalia namna nzuri ya kushughulika na Mashauri ya ukatili wa kijinsia kwa sababu licha ya kuwepo kwa juhudi mbalimbali bado suala hilo limezidi kuongezeka na kuwa changamoto ya dunia nzima hivyo wameungana na wadau kutoka nje ya nchi ili kushirikiana kutatua tatizo hilo nchini na dunia nzima.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma kongamano la siku mbili lililowakutanisha wadau mbalimbali kujadili namna bora ya kushughulikia kesi za ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto wa kike linalofanyika jijini Dar es Salaam.

Dkt. Linda Naidoo kutoka Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayopambana na Madawa ya Kulevya, Uhalifu na Makosa ya Jinai “United Nations on Drugs and Crime” (UNODC), akizungumza jambo kwenye kongamano hilo.

Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Susan Kihawa akizungumza jambo wakati wa kongamano hilo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma (walioketi  watatu kutoka kulia) akiwa katika picha ya Pamoja na wadau wa kongamano hilo.

 


Baadhi ya wadau wa kongamano hilo wakijadiliana jambo.

 (Picha na Castilia Mwanossa)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni