•Jaji Ilvin Mugeta achaguliwa kuongoza Afrika Mashariki, Kati na Kusini
•Jaji Mambi atamba kwa umahiri wa TEHAMA
Na
Faustine Kapama-Mahakama
Washiriki kutoka Tanzania
katika Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mahakimu na Majaji wa Jumuiya ya Madola (CMJA)
uliofanyika jijini Accra nchini Ghana hivi karibuni wamerudi salama nchini huku
wakiwa na nyuso za bashasha baada ya “kuupiga mwingi” katika nyanja mbalimbali,
ikiwemo Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe.
Ilvin Mugeta kuchaguliwa kuiongoza Kanda ya Afrika Mashariki, Kati na Kusini.
Katika uchaguzi
uliofanyika wakati wa Mkutano huo, Mhe. Mugeta aliibuka kidedea kama Makamu
Mwenyekiti wa Kanda hiyo baada ya ‘kumgalagaza’ vikali Jaji mwenzake kutoka
Mahakama ya Rufani na kumshinda kwa kura nyingi.
Mhe. Mugeta aliwaeleza wajumbe
wa Mkutano huo kiu yake ambayo ni kuona Bendera ya Tanzania inapeperushwa
katika medani za Kimataifa. “Nimeshakuwa kiongozi wa ngazi ya juu katika Ukanda
wa Afrika Mashariki. Hata hivyo, kiu yangu siku zote imekuwa kuiona Tanzania
iking’ara zaidi kimataifa,” alieleza.
Mhe. Mugeta anaamini kuwa
Tanzania ina mambo mengi mazuri ya kuigwa na nchi zingine za Afrika. “Mahakama
ya Tanzania inaheshimiwa sana kimataifa. Tumeweza kuwa karibu na wananchi
tunaowahudumia huku watumishi wengi wa Mahakama wakiwa na maadili na taaluma ya
kutosha,” Jaji Mfawidhi huyo alisema kwa sauti ya kujiamini.
Alipoulizwa ni mambo gani
anataka kuwafanyia wapiga kura wake ambao ni Majaji na Mahakimu kutoka nchi
zote za Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika, Mhe. Mugeta alitumia mfano wa
Mwenge wa Uhuru na kusema, “Watanzania tunaijua vizuri dhana ya kuwasha mwenge
na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro. Umulike nje ya mipaka yetu, kuleta haki na
matumanini pasipo na matumaini.”
Jaji Mugeta anaamini kuwa kuchaguliwa kwake kuziongoza nchi zaidi ya 20 ni fursa kwa Tanzania kuangaza na kuleta haki kwa vitendo. Kadhalika, anaamini kuwa wajibu wake huo mpya hautaathiri utendaji kazi wake kama Jaji. “Nafasi hii siyo kazi ya kila siku. Tutakuwa na vikao mara chache na mambo mengine tutafanya kwa njia ya mtandao. Nitaendelea na kazi zangu vizuri,” aliwahakikishia wajumbe wa Mkutano huo.
Uwekezaji mkubwa wa
Mahakama ya Tanzania uliweza pia kuchomoza katika Mkutano huo uliowaleta pamoja
Majaji Wakuu 25 na wajumbe 350 (Mahakimu na Majaji) kutoka nchi mbalimbali za
Jumuiya ya Madola. Hatua hiyo ilidhihirishwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya
Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Adam Mambi ambaye alitamba kwa umahiri
wake wa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) alipopangiwa
kuratibu mawasilisho ya mada za Utatuzi Mbadala wa Migogoro “Alternative
Dispute Resolution.”
Mhe. Mambi, ambaye ni Mwandishi
wa Kitabu cha Sheria za TEHAMA “The ICT Law Book” na mmoja wa Mwanazuoni Nguli
katika eneo hilo, alikonga nyoyo za wajumbe wa Mkutano huo na kupokea pongezi
nyingi kwa kurahisisha kazi yake ya uratibu kupitia TEHAMA.
Naye Rais wa Chama cha
Majaji na Mahakimu cha Tanzania (Judges’ and Magistrates’ Association of
Tanzania-JMAT), Mhe John Kahyoza, ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda
ya Mwanza, aliwapongeza maafisa wa Mahakama wenzake kwa mwamko wao kuhudhuria
mikutano ya kimataifa. Aliongeza kuwa
kadri siku zinavyokwenda, Watanzania wanapata hamasa ya kwenda kujifunza kwa
wenzao kutoka nchi zingine.
Katika Mkutano huo wa kimataifa,
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamisi Juma alitoa mada ya kusisimua
kuhusu Mahakama Zinazotembea na Mahakama Mtandao. Katika wasilisho lake la
kiwango cha lami, Mhe. Prof. Juma ‘alishusha nondo’ tano muhimu, ikiwemo kwa Majaji
na Mahakimu kutoka nchi za Jumuiya ya Madola kugeuza kuwa fursa changamoto wanazokabiliana
nazo wanapotekeleza majukumu ya utoaji haki kwa wananchi.
Jaji Mkuu aliieleza hadhira
yake kuwa Mahakama ya Tanzania inatumia dhana ya Mpango Mkakati kama nyenzo
muhimu ya kushirikiana na Serikali pamoja na kubainisha mahitaji halisi ya
Mahakama. Alisema Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania umeiwezesha taasisi
hiyo kuwa mstari wa mbele kutatua changamoto zake yenyewe ikiwemo kupunguza
mlundikano wa mashauri.
Mhe. Prof. Juma aliwaeleza
washiriki wa Mkutano huo kuwa Mahakama Inayotembea ni nyenzo ya kulinda haki za
jamii za pembezoni na kwa kupitia Mahamaka hiyo jamii zilizo pembezoni
zimejengewa uwezo wa kulinda haki zao.
Kadhalika, Jaji Mkuu alitanabaisha
kuwa ijapokuwa Mahakama Mtandao zilitumika zaidi wakati wa Janga la Korona,
hakuna uwezekano kwa Mahakama ya Tanzania kurudi nyuma katika matumizi ya
TEHAMA. Mhe. Prof. Juma anaamini kuwa baada ya muda mfupi Mahakama zake zote
nchini Tanzania zitakuwa zimeunganishwa na mtandao ili kurahisisha ufunguaji wa
kesi na shughuli nyingine.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni