Na. Ibrahim Mdachi – IJA Lushoto
Majaji wapya walioteuliwa
hivi karibuni juzi wametembelea Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga kujifunza
mambo mbalimbali, ikiwemo ubunifu uliofanyika unaochochea kwa haraka utoaji wa
huduma za haki kwa wananchi, hatua iliyopelekea Mahakama hiyo kuwa ya mfano katika
matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) hapa nchini.
Katika ziara yao fupi,
Majaji hao walioongozana na wenzao kutoka Mahakama Kuu Zanzibar walipokelewa na
Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakamu Kuu katika Kanda, Mhe. Dkt. John Ubena ambaye
aliwaeleza kwa kifupi jinsi TEHAMA inayorahisisha shighuli za kimahakama katika
Mahakama hiyo.
Jaji Ubena alisema kuwa
kupitia TEHAMA, Mahakama hiyo imeweza kupunguza kwa kiasi kikubwa mrundikano wa
mashauri sambamba na kuwa na utaratibu mzuri na salama wa mgawanyo, uhifadhi na
utafutaji wa majalada kwa wakati, jambo ambalo limepunguza kama sio kumaliza kabisa
malalamiko toka kwa wadaawa.
Naye Naibu Msajili wa
Mahakama hiyo, Mhe. Beda Nyaki aliwapitisha Majaji hao katika baadhi ya mifumo na
kuonesha jinsi inavyofanya kazi ukiwemo mfumo wa kusajili mashauri “Judicial
Statistical Dashboard System - JSDS 2” katika hatua zote, kuanzia kupokelewa na
kufunguliwa jalada mpaka kutolewa uamuzi.
Aliongeza kuwa mfumo huo
unafanya kazi masaa 24 kwa wiki, hivyo kuwarahisishia wadaawa kuweza kufungua
mashauri wakati wowote na mahala popote pale walipo.
Akitoa maelezo ya mifumo
mbalimbali inayotumiwa na Mahakama ya Tanzania katika walisilisho lake mbele ya
Majaji hao, Afisa TEHAMA, Bw. Mussa Mwinjuma alisema mifumo hiyo imekuwa msaada
mkubwa kwa watumishi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku ambapo
imewawezesha kutoa huduma kwa haraka kwa kadiri inavyohitajika.
Sambamba na mifumo ya
kitaifa inayotumiwa na Mahakama ya Tanzania, Afisa TEHAMA huyo aliwapitisha
Majaji katika mifumo ya ndani inayotumiwa na Mahakama hiyo ambayo ndiyo hasa
imeifanya kuwa ya mfano nchini, ukiwemo mfumo wa ukusanyaji taarifa za
kumbukumbu tuli “Tanga Record Centre Database-TCRD”.
Alisema kuwa Kanda ya
Tanga ilianza kutumia Kanzi data hiyo tangu mwaka 2017 kwa kusajili taarifa za
majalada ya mashauri yaliyomalizika kusikilizwa na kupelekwa mahali
yalipohifadhiwa kweye kituo cha kuhifadhia kumbukumbu tuli kwa lengo la
kumsaidia mtumishi kutambua na kulichukuwa jalada stahiki kwa urahisi mahala
lilikohifadhiwa.
Aliongeza kuwa kanzi data
hiyo imewarahisishia Majaji na wadau kupata majalada yaliyosikilizwa kwa haraka
na urahisi mkubwa pindi wanapoyahitaji kwa madhumuni mbalimbali. Pia Majaji
walipitishwa kwenye mfumo unaokusanya taarifa za majalada yanayopokelewa kutoka
Mahakama za chini “Lower Court Records” ambao umesaidia kuondosha kadhia ya
upotevu wa taarifa za majalada.
Taarifa zinazokusanywa na
mfumo huo ni pamoja na namba ya kesi, majina ya wadaawa, jina la mtumishi
aliyepeleka na kupokea jalada hilo. Afisa TEHAMA huyo aliongeza kuwa mfumo huo
hutoa ripoti za majadala yaliyorudishwa na ambayo hayajarudishwa katika vituo
vyake vya awali.
Majaji hao wapo kwenye
mafunzo elekezi yanayoendelea Wilayani Lushoto
ambayo yanaendeshwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakam Lushoto kwa
kushirikiana na Mahakama ya Tanzania ili kuwaandaa, kuwapatia uelewa mzuri,
kuwajengea uzoefu wakutosha na kuwaweka tayari kuyakabili majukumu muhimu na
mzito yaliyoko mbele yao.
Mafunzo hayo ambayo ni
muendelezo wa mafunzo mbalimbali yanayoendelea kutolewa na Chuo hicho kwa watumishi
wa Mahakama na wadau wa sekta ya sheria nchini yalianza tarehe 31 Agosti, 2022
na yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 16 Septemba, 2022 chuoni hapo.
Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakamu Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga, Mhe. Dkt. John Ubena (aliyesimama) akiwakaribisha Majaji wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Majaji wa Mahakama Kuu Zanzibar waliofanya ziara fupi katika Mahakama hiyo.
Baadhi ya Majaji wa Mahakama Kuu wakiwa ndani ya chumba cha kisasa cha kutunzia kumbukumbu tuli.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni