Ijumaa, 16 Septemba 2022

MENEJIMENTI YA MAHAKAMA YARIDHISHWA NA MIRADI UJENZI NYUMBA ZA MAJAJI, MAKAO MAKUU

Na Tiganya Vincent-Mahakama, Dodoma

Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania imeridhishwa na miradi miwili ya ujenzi wa nyumba za Majaji na Makao Makuu ya Mahakama Tanzania ilizopo katika maeneo ya Iyumbu na NCC jijini Dodoma.

Hayo yamebainishwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel wakati wa ziara fupi iliojumuisha Menejimenti ya watumishi wa Mahakama waliotembea maeneo hayo ili kuona ujenzi unavyoendelea.

Alisema majengo hayo yanatarajiwa kukabidhiwa Desemba 31, 2022 ili yaanze kutumika kama walivyokubaliana na Wakandarasi.

"Makao Makuu na haya majengo yanatarajiwa kukamilika Desemba 31, 2022, naamini Wakandarasi watatimiza makubaliano yaliyowekwa. Ujenzi wa Makao Makuu umefikia asilimia zaidi 68 na ujenzi wa nyumba za Majaji wa Mahakama ya Rufani umefikia asilimia 27,"alisema Prof. Ole Gabriel.

Alifafanua zaidi kuwa wanafanya hivyo kwa lengo la kutimiza ahadi ya Mahakama kuhamia Dodoma kama zilivyofanya Taasisi na Wizara mbalimbali. Mtendaji Mkuu huyo alisema kuwa wanatarajia kutumia shilingi bilioni 129.7 hadi kukamilika kwa ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

"Tunaishukuru sana serikali kutokana kuendelea kutoa fedha za ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama na majengo ya makazi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu, tunaamini Majaji watafanya kazi wakiwa katika mazingira rafiki yanayoendana na kazi zao,"alisema.

Alisema nyumba za makazi ya Majaji zikikamilika zitakuwa na uwezo wa kuchukua familia 26 katika jengo mmoja. Naye Msanifu Majengo Rose Nestory aliwasihi wajumbe kutoka Mahakama ya Tanzania kutokuwa na wasiwasi wowote kwa sababu majengo hayo yatakamilika kwa wakati uliopangwa.

Alisema wao kama wasanifu wanaishukuru Serikali kutokana na kutoa ushirikiano katika ujenzi huo ili kuhakikisha kila kitu kinakwenda sawa katika suala zima la ukamilisha nyumba za majaji pamoja na Makao Makuu ya Mahakama.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Rasimali Watu wa Mahakama ya Tanzania Beatrice Patrick alimpongeza Mtendaji Mkuu wa Mahakama kutokana na usimamizi mzuri wanaofanya katika ujenzi huo.

Alisema wao kama wajumbe wa Menejimenti kutoka Mahakama ya Tanzania wameridhishwa na ujenzi huo, hivyo wanaishkuru Serikali kutokana na juhudi inayofanya ili kuhakikisha Mahakama hiyo inahamia jijini Dodoma.

Beatrice alitoa wito kwa wakandarasi hao kutobweteka badala yake waongeze bidii katika ujenzi wanaofanya ili wakamilishe kwa wakati.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa ufafanuzi kwa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania wakati wa ziara ya kutembelea majengo ya makazi ya Majaji na Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma jana.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa ufafanuzi mbele ya nyumba za Majaji wa Mahakama ya Rufani wakati wa ziara ya kutembelea majengo ya makazi ya Majaji na Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma jana.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwaonyesha eneo ambalo limeezekwa kwa kioo ambalo liko ghorofa ya sita wakati wa ziara ya Mnejimenti ya Mahakama ya Tanzania ya kutembelea majengo ya makazi ya Majaji na Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma jana.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama Profesa Elisante Ole Gabriel akitoa ufafanuzi kwa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania akiwa katika ghorofa ya sita  wakati wa ziara ya kutembelea majengo ya makazi ya Majaji na Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma jana.
Mkurugenzi wa Utawala na Rasimali Watu wa Mahakama ya Tanzania Beatrice Patrick akitoa maelezo kwa niaba ya watumishi wenzake wakati wa ziara ya Menejimenti ya kutembelea majengo ya makazi ya Majaji na Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma jana.
Maendeleo ya ujenzi wa nyumba za makazi ya Majaji wa Mahakama ya Rufaa yalipofikia hadi katikati ya mwezi huu ambayo yako mjini Dodoma.
Mfano wa muonekano wa Jengo kwa ajili ya makazi ya majaji wa Mahakama ya Rufaa yatakavyoonekana mara baada ya kukamilika mjii Dodoma mwishoni mwa mwaka huu.

Msanifu Majengo Rose Nestory akitoa maelezo kuhusu miradi ya ujenzi wa nyumba za Majaji wa Mahakama ya Rufaa na Mahakama Kuu na Makao Makuu ya Mahakama jana wakati wa ziara ya Menejimenti ya Mahakama kwenye Makao Makuu ya Ofisi zao zinazojengwa.

(Picha na Tiganya Vincent-JOT)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni