Jumatatu, 31 Oktoba 2022

IJC MWANZA YAANZA KUWANUFAISHA WAKAZI KATA YA BUSWELU

Na Stephen Kapiga, Mahakama Mwanza

Wananchi wa Kata Buswelu Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza wameishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kuwasogezea huduma ya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) kilichojengwa katika eneo hilo huku wakikiri kunufaika na uwepo wake ikiwemo kuziwezesha familia takribani 100 kupata maji safi na salama yanayopatikana katika kisima cha Kituo hicho kilichozinduliwa hivi karibuni.

Akizungumza na Diwani wa Kata ya Buswelu, Bi. Sarah Ng’wani aliyetembelea Kituo hicho hivi karibuni, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Mhe. John Kahyoza alimueleza Diwani huyo namna ambavyo Mahakama zilipo ndani ya jengo la ‘IJC’ zinavyoshirikiana na jamii inayowazunguka.

“Kwakuwa sasa tuna uhakika wa kupata maji mengi na yanayokidhi mahitaji yetu ndani ya jengo hili na bado tunabaki na ziada, tumeona ni bora pia maji haya kugawa kwa wananchi wanaoishi nyumba za hapa jirani na IJC na maji haya yatatumika kwa matumizi ya nyumbani tu na si kwa jili ya kufanyia biashara” alisema Mhe. Kahyoza.

Nao wananchi wanaozunguka kituo hicho jumushi kwa nyakati tofauti waliwashukuru Viongozi wa Mahakama Kanda ya Mwanza kwa kuwakumbuka na kuweza kuwasaidia kuondokana na kadhia hiyo kwani maji ndio kila kitu katika maisha na kazi za kila siku majumbani.

“Kwa kweli bila maji huwezi kufanya jambo lolote lile ukiwa nyumbani. Kwa jambo hili waliloamua Mahakama kutusaidia maji bure bila ya kulipa chochote kwa kweli tunawashukuru sana Viongozi wa Mahakama kwani inaonesha kweli wanatoka katika mazingira na familia ambazo kwao kushirikiana na watu ni jambo la muhimu na sio kujitenga na jamii kwa sababu ya nafasi zao ndani ya Mahakama” alisema Mzee Sufiani Juma.

Ikumbukwe kuwa eneo la Buswelu limekuwa na changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji ya bomba hivyo kufanya kuwa ngumu kupata maji kwa familia ambazo hazina huduma ya maji ya kisima. Kufuatia kadhia hiyo, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel alifanya zoezi la uchimbaji wa kisima chenye urefu wa mita 180 na kufunga pampu ya kusukuma maji kwa kutumia nguvu ya jua ili kuwezesha upatikanaji wa maji ndani ya jengo la IJC Mwanza kwa gharama nafuu.

Akitoa shukrani zake kwa niaba ya wananchi wa kata hiyo alipotembelea Kituo hicho hivi karibuni, Diwani wa Kata ya Buswelu, Bi. Sarah Ng’wani aliipongeza Mahakama kwa kuweza kuikumbuka jamii inayozunguka jengo hilo.

“Kwanza kabisa kwa niaba ya wananchi wangu tunaishukuru Mahakama ya Tanzania, Jaji Mfawidhi wa hapa na Mtendaji kwa kuweza kudumisha uhusiano huu na wananchi. Hii inanifanya nijivunie kutoa eneo hili la kujenga jengo hili kwani hapo awali eneo hili lilikuwa limetengwa kwa ajili ya ujenzi wa shule, lakini niliposikia uhitaji wa Mahakama kuhitaji eneo niliweza kuishawishi ‘ODC’ (Ofisi ya Mkuu wa Wilaya) ya Ilemela na hatimaye eneo hili kutolewa kwa Mahakama” alisema Bi. Sarah.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Mwanza alimtembeza Diwani huyo katika ofisi zote zilizopo katika jengo hilo na kumuelezea namna kila Ofisi inavyotenda kazi katika jengo hilo jambo ambalo lilimvutia diwani huyo.

“Kwakweli nimefurahia mazingira namna yalivyo bora, kuanzia Mahabusu hasa Mahabusu ya watoto jinsi yalivyo rafiki kwa watoto na hivo kufanya kila ofisi kuwa rafiki kwa watumiaji na wateja wake. Hii kwa kweli inatupa imani sisi jamii kweli haki inaonekana inaenda kutendeka ndani ya jengo hili,” aliongeza Diwani huyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. John Kahyoza (mwenye suti nyeusi) akiwa katika picha ya pamoja na Diwani wa Buswelu, Bi. Sarah Ngw'ani (mwenye nguo ya kitenge) aliyetembelea Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kilichopo Kata ya Buswelu mkoani Mwanza. Wengine ni Viongozi Mahakama wanaofanya kazi katika Kituo hicho.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe. John Kahyoza (kushoto) akimfafanulia jambo Diwani wa Buswelu, Bi Sarah Paul Ng’wani (katikati)  alipotembelea na kukagua Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki 'IJC' Mwanza hivi karibuni.

Maoni 1 :

  1. Hongera sana Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza kwa kuweka uhususiano mzuri na jamii inayozungukama Mahakama. Kitendo tu Cha kutoa maji kwa wananchi ni utu wa kutosha kwa mwanadamu . Mungu ibariki Mahakama ya Tanzania Kanda ya Mwanza na viongozi wake kwa ujumla pamoja na watumishi wake.

    JibuFuta