Ijumaa, 28 Oktoba 2022

UTUMISHI BORA UNALIPA: JAJI MFAWIDHI MUSOMA

Na Francisca Swai, Mahakama-Musoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya jana tarehe 27 Octoba, 2022 aliendelea na ziara yake ya kikazi kukagua shughuli mbalimbali za kimahakama katika Wilaya ya Tarime ambapo amewaasa watumishi wilayani humo kuzingatia maadili kwani utumishi bora unalipa.

Akizungumza kwenye kikao kilichojumuisha watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Tarime Mjini na Mahakama ya Wilaya Tarime, Mhe. Mtulya waliwataka watumishi hao kujenga mazingira ya kuheshimiana, kupendana, kuthaminiana na kufanyakazi kwa bidii kwani mchango wa kila mmoja wao unakamilisha jukumu la Mahakama la utoaji haki kwa wote na kwa wakati.

Jaji Mfawidhi huyo, ambaye ameambatana na viongozi mbalimbali wa Mahakama Kanda ya Musoma, aliwasihi watumishi wote kuwa waadilifu na kuishi kulingana na vipato vyao na kutumia njia halali za kujipatia vipato nje ya mshahara kulingana na fursa zinazopatikana katika maeneo yanayowazunguka.

Mhe. Mtulya aliwapongeza watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Tarime Mjini kwa kasi nzuri ya umalizaji wa mashauri licha ya uchache wao ukilinganisha na wingi wa mashauri katika kituo hicho.

Aidha, akawapongeza watumishi wanaotumia majengo ya Mahakama za Mwanzo zilizokarabatiwa hivi karibuni ambazo ni Ngoreme iliyoko Serengeti na Mtana iliyoko Tarime kwa usafi na utunzaji mzuri wa mazingira. Aliwasisitiza kuendelea na juhudi hizo na kuhakikisha mipaka ya maeneo yao inalindwa ili kuepuka uvamizi.

Katika ukaguzi huo, msafara wa Jaji Mfawidhi ulitembelea pia Mahakama ya Mwanzo Mtana ambayo ilifungwa mwaka 2000 kutokana na wananchi wa eneo hilo kusuluhisha matatizo yao kimila, hivyo Mahakama kukosa mashauri.

Mahakama hiyo imeanza kufanya kazi tarehe 1 Agosti 2022 baada ya Mhe. Mtulya kuelekeza ikarabatiwe kutokana na kukua kwa kijiji hicho, ongezeko la watu na shughuli za kiuchumi, hivyo wananchi kuhitaji uwepo wa huduma za kimahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (aliyesimama) akiongea na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Tarime Mjini pamoja na Mahakama ya Wilaya Tarime.

Kaimu Hakimu Mkazi Mahakama ya Wilaya Tarime, Mhe. Yohana Myombo (aliyesimama) akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi wa kituo cha Mahakama ya Wilaya Tarime.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya, Mhe. Fahamu Mtulya (aliyenyoosha mikono) akiteta na viongozi wa Kijiji cha Mtana kuhusiana na mipaka ya eneo la Mahakama hiyo. Mwenye tisheti ya bluu ni Mwenyekiti wa Kitongoji cha Mtana Center, Bw. Charles Daudi, mwenye tisheti nyekundu ni Mtendaji wa Kijiji cha Mtana, Bw. Kwilasa Alex na mwenye shati ya kijani ni Katibu wa Kamati ya Ardhi ya kijiji cha Mtana, Bw. Silasi Mwita.

Muonekano wa Mahakama ya Mwanzo Mtana (juu) kabla ya ukarabati. Muonekano wa Mahakama ya Mwanzo Mtana (chini) baada ya ukarabati.


Muonekano wa Mahakama ya Mwanzo Ngoreme (juu) kabla ya ukarabati Muonekano wa Mahakama ya Mwanzo Ngoreme (chini) baada ya ukarabati.


Picha ya pamoja ya viongozi wa Mahakama Kanda ya Musoma akiwemo Jaji Mfawidhi, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati). Wengine ni Naibu Msajili. Mhe. Frank Moshi (wa tatu kulia), Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Serengeti Mhe. Jacob Ndira (wa pili kulia), Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Mwanzo Ngoreme, Mhe. Peter Malima (wa kwanza kulia), Mtendaji wa Mahakama Bw. Festo Chonya (wa tatu kushoto), Afisa Tawala Mahakama ya Wilaya Serengeti Bi. Faraja Barakazi (wa pili kushoto) na Mlinzi wa Mahakama ya Mwanzo Ngoreme, Bw. Chacha Nsaho (wa kwanza kushoto).
Picha ya pamoja ya viongozi wa Kanda ya Musoma na viongozi wa Mahakama ya Wilaya Tarime akiwemo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati). Wengine ni Naibu Msajili Mhe. Frank Moshi (wa tatu kulia), Mtendaji wa Mahakama Musoma Bw. Festo Chonya (wa tatu kushoto), Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Tarime Mhe. Yohana Myombo (wa pili kulia), Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Tarime Mhe. Vicencia Balyaruha (wa kwanza kulia), Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Mwanzo Tarime Mjini Mhe. Terecia Boah (wa pili kushoto) na Afisa Tawala Mahakama ya Wilaya Tarime Bw. Herman Lomasi (wa kwanza kushoto).

Picha ya pamoja ya viongozi wa Kanda ya Musoma, viongozi wa Mahakama ya Wilaya Tarime na watumishi wa Mahakama ya Wilaya na ya Mwanzo Tarime Mjini.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni