Jumanne, 22 Novemba 2022

WATUMISHI WA MAHAKAMA, WADAU KIGOMA WASHIRIKI MAFUNZO YA ZIMAMOTO NA UOKOAJI

Na Festo Sanga-Mahakama, Kigoma

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji katika Mkoa wa Kigoma hivi karibuni liliendesha mafunzo kuwajengea uwezo kinadharia na kwa vitendo watumishi wa Mahakama ya Tanzania, wateja na watoa huduma za ulinzi na usafi kuhusu uokoaji na uzimaji moto.

Akifungua mafunzo hayo kwa washiriki 42 wakiwemo watumishi kutoka Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya ya Kigoma, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kigoma Bw. Moses Mashaka alisema Jeshi hilo limelenga kuwapa ujuzi wa kujikinga na kupambana na ajari za moto ili kuepusha au kupunguza athari zinazoweza kutokea ikiwa janga hilo litatokea.

Aidha aliwakumbusha washiriki wote kuzingatia mafunzo watakayoyapata na kuhakikisha wanajisajili kila mara wanapokuwa ofisini  kwenye mashine maalumu ya kurekodi mahudhurio ili kuwa na taarifa sahihi za idadi ya  wanaokuwepo ndani ya jengo ikiwa ni hatua za awali za uokoaji kama litatokea janga lolote.

“Tumeandaa mafunzo haya kwa gharama ili muweze kutumia vyema vifaa na mifumo iliyopo katika majengo kujikinga, kujiokoa na kuokoa mali za ofisi dhidi ya majanga ya moto na mengine yanapotokea, hivyo kuepusha au kupunguza madhara yanayoweza kutokea” alisema Bw. Mashaka.

Naye Mkaguzi Msaidizi wa Zimamoto na Uokoaji Bahati Salumu ambaye alikuwa mwezeshaji wa mafunzo hayo aliwaeleza washiriki kuhusu mifumo mbalimbali iliyomo katika jengo mahususi kwa ajili ya kujikinga na kujiokoa dhidi ya  majanga ya moto na majanga mengine.

Alitaja baadhi ya mifumo ikiwemo vigunduzi moshi, vizima moto, alama za njia za dharura na eneo maarufu kama “Refugees Area”au kitaalamu likiitwa “Balcon” ambalo hutumika kwa watu waliozingirwa na moto ili waokolewe.

Aidha, katika mafunzo hayo, washiriki walikumbushwa juu ya namna ya kuukabili moto kwa kutumia vifaa vya kuzimia moto vilivyopo katika mazingira mbalimbali vikiwemo mchanga mkavu, matawi ya miti mibichi, mitungi ya gesi ya kuzima moto (fire extinguishers), Blanketi maalum (fire blanket) na mfumo maji ya kuzima moto kwa mpira (horse reel).

Mafunzo hayo ni utekelezaji wa mkakati wa kuimarisha usalama wa watumiaji wa jengo na mali za ofisi na pia ni takwa la kisheria kupitia Kanuni Na.6 (1) (c) ya Kanuni za Jeshi la Zimamoto na Uokoaji za mwaka 2008 kuhusu kuwezeshwa kimafunzo juu ya tahadhari za kuchukuliwa na watumiaji wote wa jengo katika jitihada za kupambana na majanga ya moto.

Mwezeshaji kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Mkaguzi Msaidizi Bahati Salumu akitoa mafunzo ya nadharia kwa washiriki wa mafunzo hayo yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma.
Mwezeshaji wa mafunzo kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Mkaguzi Msaidizi Bahati Salumu akionesha namna ya kuzima moto kwa kutumia Blanket maalum.
Mshiriki wa mafunzo kutoka Mahakama ya Tanzania, Bi Christina Mpungu akizima moto uliowashwa kwa kutumia Blanketi maalumu ikiwa ni sehem ya mafunzo kwa vitendo.

Mshiriki wa Mafunzo kutoka Kampunzi ya Ulinzi ya Suma JKT, Bi Christa Samson akiwa tayari amefanikiwa kuzima moto kwa vitendo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni