Alhamisi, 1 Desemba 2022

BONANZA LA MAHAKAMA MTAANI LATIKISA IRINGA

Na Lusako Mwang’onda-Mahakama Kuu, Iringa.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa hivi karibuni ilifanya tamasha kubwa ambalo lilihusisha bonanza katika michezo mbalimbali, lengo likiwa kuisogeza Mahakama karibu na wananchi ili kufahamu shughuli inazofanya na kuitumia ipasavyo kama chombo chao cha usimamizi wa haki hapa nchini.

 Bonanza hilo ambalo lilipewa jina la Mahakama Mtaani, ambapo kauli mbiu yake ilikuwa ni “Njoo Tuongee Kimtaani” lilifanyika baada ya kufanya utafiti na kugundua kuwa wananchi wengi na hasa wa ngazi ya chini wanaigopa Mahakama.

Kutokana na hali hiyo, uongozi wa Mahakama katika Kanda hiyo kwa kushirikisha wadau uliona ni vyema kuandaa bonanza hilo, ambalo lilishirikisha michezo mbalimbali ikiwemo Mpira wa Miguu, Mpira wa Pete, Riadha, Kuvuta Kamba, Kucheza rede, Kukuna nazi, Kukimbiza kuku pamoja na mashindano ya kura na kunywa.

Bonanza hilo la Mahakama Mtaani lenye dhima kubwa ya kutoa elimu kuhusu maswala mbalimbali ya kimahakama na kisheria kwa ujumla lilifanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Ipogolo, ambapo Mgeni Rasmi alikuwa ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Dkt. John Utamwa huku mgeni wa heshima akiwa ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe Halima Dendego. 

Akizungumza na wananchi waliofurika kwenye tamasha hilo, Jaji Utamwa alisema kuwa lengo kubwa la bonanza hilo ni kuisogeza Mahakama mtaani na kuwafikia wananchi wa kawaida ili waijue kama chombo chao kikuu cha usimamizi wa haki.

Mhe. Utamwa alisisitiza kuwa bonanza hilo limelenga zaidi kutoa elimu katika masuala ya kisheria, ikiwemo Mirathi, Ndoa, Talaka, Ardhi na Haki Jinai hasa kwa makundi mengi mtaani ambayo yapo kwenye hatari ya ama kufanya au kufanyiwa makosa ambayo yatawapelekea wao kuletwa mahakamani.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Iringa aliushukuru uongozi wa Mahakama wa Kanda hiyo kwa kubuni tukio hilo ambalo limekuwa na faida kwa wananchi waliofika kwenye viwanja hivyo. Aliuomba uongozi huo kuendeleza mabonanza kama hayo ili kuwaongezea wananchi uelewa wa masuala mbalimbali ya kimahakama na kisheria kwa ujumla.

Mbali na michezo hiyo katika tamasha hilo, kulikuwa na burudani kutoka kwa wanamziki na vikundi mbalimbali vya ngoma za asili waliotumbuiza siku hiyo.

Tamasha hilo lilihudhuriwa na wadau mbalimbali wa Mahakama wakiwemo TAKUKUKURU, Chama cha Wanasheria (TLS), Jeshi la Polisi, Ofisi ya Mwendesha Mashtaka, na wengine ambao wote walishiriki kutoa elimu ya masuala mbalimbali ya kisheria katika mabanda yao.

Sehemu ya umati uliofika katika bonanza la Mahakama Mtaani ikimsikiliza kwa makini Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe.  Dkt. John Utamwa.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Halima Dendego akihutubia katika bonanza la Mahakama Mtaani.
Mmoja wa wanamziki wa kizazi kipya akitumbuiza umati wa watu uliohudhuria katika bonanza hilo.
Kikundi cha ngoma za asili kikitumbuiza wakati wa bonanza la Mahakama-mtaani.
Timu ya Kuvuta Kamba ya Watumishi wa Mahakama Kanda ya Iringa wakimenyana na timu ya kuvuta kamba ya Vijana wa Ipogolo katika tamasha hilo.
Timu ya kuvuta Kamba ya Wanawake ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa ikiwa jukwaani baada ya kutangazwa kuwa washindi.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tnazania, Kanda ya Iringa, Mhe. Dkt, John Utamwa akikakagua Timu ya mpira wa miguu kutoka Wilaya ya Kilolo wakati wa bonanza la Mahakama Mtaani.

Mabingwa wa Mpira wa Miguu Timu ya City Center toka mitaa ya Ipogolo Manispaa ya Iringa wakiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Mahakama baada ya kukabidhiwa Kombe na Ng'ombe dume.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni