Ijumaa, 2 Desemba 2022

WATUMISHI WA MAHAKAMA ZA WILAYA WAASWA KUWA WABUNIFU

Na Mary Gwera, Mahakama-Morogoro

Mkurugenzi Msaidizi wa Kurugenzi ya Usimamizi wa Mashauri- Mahakama ya Tanzania, Mhe. Agness Mchome ametoa rai kwa Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya kuwa wabunifu na uwezo wa kufanya kazi zaidi ya zile za taaluma zao ‘multitasking’ ili kuendana na kasi ya mabadiliko ya kiteknolojia.

Akiwasilisha Mada ya Usimamizi na Uratibu wa Mashauri kwa njia ya Kieletroniki (JSDS) kwa watumishi hao jana tarehe mosi Desemba, 2022 mkoani Morogoro, Mhe. Agness alisema ubunifu ni muhimu hususani katika kipindi hiki ambacho Mahakama inaendelea kuboresha huduma zake.

“Napenda kutoa rai kwenu Watumishi wenzangu kila mmoja kwa nafasi yake, tafuteni namna ya kuwahusisha hata Madereva, walinzi na watumishi wa kada nyingine kuingia kwenye mfumo wa JSDS ili kuendana na mabadiliko ya ki-TEHAMA,” alisema Mhe. Agness.

Aliongeza kwa kueleza umuhimu wa kujua kazi zaidi ya moja husaidia pia kuziba changamoto ya upungufu wa watumishi, kuokoa muda na vilevile kuongeza tija katika kazi.

Akiwakumbusha Watumishi hao kuhusu matumizi ya ‘JSDS’, Mhe. Mchome amewasisitiza pia kuwa makini katika usajili ya mashauri na matumizi mengine yanayohusiana na mfumo huo muhimu kwa Mahakama ya Tanzania.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi wa TEHAMA-Mahakama ya Tanzania, Bw. Allan Machella akiwasilisha Mada ya Matumizi bora na sahihi ya Vifaa, Mifumo na Miundombinu ya TEHAMA amewaasa Washiriki wa Mafunzo ya Huduma kwa Mteja kuendana na kasi ya mabadiliko ya kiteknolojia kwa kuwa kila siku kuna kitu cha kujifunza katika eneo hilo.

Kadhalika Mkurugenzi huyo amewakumbusha kutunza vifaa, mifumo na miundombinu ya TEHAMA kwa kuwa ni nyenzo muhimu katika kuwezesha utekelezaji wa shughuli za Mahakama.

“Ulimwengu wa sasa ni ulimwengu wa kidijitali ‘digital transformation’, hivyo Watumishi mnapaswa kujua kwamba teknolojia imekuwa ni sehemu ya Maisha yenu ya kila siku na mnatakiwa kujifunza mambo mapya kila siku ili msipitwe na mabadiliko ya Teknolojia yanayojitokeza kila wakati,” alisisitiza Bw. Machella.

Naye Mwezeshaji wa Mafunzo, Bw. Godfrey Wawa aliyewasilisha mada ya Jinsi ya kukabiliana na Msongo amewaeleza washiriki wa mafunzo kuwa wanatakiwa kuwa makini kwa kutoongozwa na hisia pindi wanapotaka kufanya uamuzi wowote katika maisha yao ya kiutumishi na maisha binafsi.

Aidha; katika siku ya nne (4) ya mafunzo hayo ilitolewa pia Mada kuhusu Matumizi na Utunzaji wa majengo ya Mahakama pamoja na Vifaa vyake ambapo Maafisa kutoka Kitengo cha Usimamizi wa Majengo cha Mahakama ya Tanzania wamewaasa Watumishi wa Mahakama za Wilaya mpya kuyatunza majengo na kutoa taarifa kwa wakati endapo kuna hitilafu/dosari yoyote.

Leo tarehe 02 Desemba, 2022 ni siku ya mwisho ya Mafunzo kwa sehemu ya Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya 18 kutoka Gairo, Songwe, Mkinga, Kilombero na Mvomero. Mafunzo kwa Watumishi wengine wa Mahakama za hizo mpya yataendelea kutolewa mfululizo kwa Watumishi wake ambapo yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 23 Desemba, 2022.

Tarehe 25 Novemba, 2022 Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alizindua Mahakama ya Wilaya Busega iliyowakilisha Mahakama nyingine mpya za Wilaya mpya 17, Mahakama hizo zilizojengwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia ni pamoja na; Butiama, Rorya, Songwe, Gairo, Mkinga, Mvomero, Kilombero, Mbogwe, Nyang'hwale, Kyerwa, Itilima, Missenyi, Kaliua, Uvinza, Buhingwe, Kakonko na Tanganyika.

Mkurugenzi Msaidizi wa Kurugenzi ya Usimamizi wa Mashauri- Mahakama ya Tanzania, Mhe. Agness Mchome (aliyesimama kulia) akiwasilisha Mada ya Usimamizi na Uratibu wa Mashauri kwa njia ya Kieletroniki (JSDS) kwa sehemu ya Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya. Mhe. Agness alitoa mada hiyo jana tarehe mosi Desemba, 2022 katika Ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro.
Mkurugenzi Msaidizi wa Kurugenzi ya Usimamizi wa Mashauri- Mahakama ya Tanzania, Mhe. Agness Mchome akisisitiza jambo alipokuwa akiwasilisha mada ya Usimamizi na Uratibu wa Mashauri kwa njia ya Kieletroniki (JSDS) kwa baadhi ya Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya.


Washiriki wa Mafunzo ya Huduma kwa Mteja ambao ni sehemu ya Watumishi wa Mahakama za Wilaya mpya wakifuatilia mada inayotolewa na Mwezeshaji (hayupo katika picha).
Mkurugenzi Msaidizi wa TEHAMA-Mahakama ya Tanzania, Bw. Allan Machella akiwasilisha Mada ya Matumizi bora na sahihi ya Vifaa, Mifumo na Miundombinu ya TEHAMA kwa washiriki wa mafunzo ya huduma kwa mteja.
Mhandisi Ujenzi kutoka Kitengo cha Usimamizi wa Majengo cha Mahakama ya Tanzania akiwasilisha mada ya Matumizi na Utunzaji wa majengo ya Mahakama pamoja na Vifaa vyake.
Mwezeshaji wa Mafunzo, Bw. Godfrey Wawa akiwasilisha mada ya Jinsi ya kukabiliana na Msongo kwa washiriki wa mafunzo.





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni