Ijumaa, 2 Desemba 2022

PELEKENI HUDUMA ZA UWAKILI MAENEO YOTE YA TANZANIA: JAJI MKUU

Na Tiganya Vincent-Mahakama ya Tanzania

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka Mawakili wapya aliowaapitisha kutumia fursa ya uboreshaji wa miundombinu ya Mahakama hapa nchini kufungua ofisi karibu na Mahakama za Wilaya 20 zilizofunguliwa hivi karibuni.

Mhe. Prof. Juma ametoa wito huo leo tarehe 2 Disemba, 2022 katika Viwanja vya Karimjee jijni Dar es salaam wakati wa Sherehe za 67 za kuwakubali na kuwaingiza kwenye daftari Mawakili wapya 358 na kufanya Tanzania kufikisha Mawakili 11,442 wa kujitegemea.

“Pelekeni huduma za Mawakili maeneo yote ya Tanzania, Mahakama ya Tanzania inaendelea na juhudi thabiti za kusogeza huduma ya utoaji haki karibu na wananchi,” alisema.

Jaji Mkuu alisema kuwa tangu mwaka 2015 Mahakama ya Tanzania imejenga majengo ya kisasa kutoa huduma za Mahakama katika mikoa yote ya Tanzania.

Alisema majengo 20 ya Mahakama za Wilaya ambayo ameyazindua katika Wilaya za Mwanga, Same, Busega, Itilima, Butiama Rorya, Songwe, Gairo, Mkinga, Mbogwe, Nyang’hwale, Kyera, Missenyi, Kaliua, Uvinza, Buhigwe, Kakonko, Tanganyika, Kilombero na Mvomero ni fursa kwao katika utoaji wa huduma za uwakili kwa wananchi wa maeneo hayo.

Mhe. Prof. Juma alisema baadhi ya Wilaya hizo ni mpya na zina fursa za kutosha kwa Mawakili na zipo fursa nyingi za kiuchumi ambazo wanaweza kuzitumia ili kujipatia kipato na kujiendelea kimaisha.

Aliwashauri baada ya kuapishwa na kuingia katika daftari la Mawakili ni vema wakahama kutoka mijini na majiji ambako soko la uwakili lina ushindani mkubwa hasa kwa Mawakili ambao bado hawajapata uzoefu wa kutosha na kwenda vijijini ambako kuna fursa ya kuwawezesha kujijengea uwezo wa kuendelea katika kazi yao.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Dkt. Eliezer Feleshi alisema kumekuwepo na tabia ya baadhi ya Mawakili kujisahaulisha au kutoutendea haki wajibu wao wa kuisaidia Mahakama kufikia uamuzi ya haki kwa wakati.

Alisisitiza kuwa hiyo siyo tu jambo jema lisilo na maadili, bali pia linawaondolea baadhi hadhi ya kuwa Maafisa wa Mahakama wanapotekeleza wajibu kwa wateja wao.

Mhe. Dkt. Feleshi alisema ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi Mawakili ambao watashindwa kujiendeleza ipo hatari kwao kujikuta wakinukuu Sheria ambayo imeshafanyiwa mabadiliko na haitumiki tena.

“Kwa mfano, Wakili anapoamua kufanya rejea kwenye uamuzi uliotolewa na Mahakama Kuu au Mahakama ya Rufani, anapaswa kusoma uamuzi wote na kuuelewa na siyo kutumia aya moja ya uamuzi huo hivyo kuipotosha Mahakama pamoja na kwamba Mahakama nayo inalo jukumu la kuusoma ili kujiridhisha na usahihi wa hoja kwa mujibu wa uamuzi rejewa,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Mawakili wa Tanganyika (TLS), Prof. Edward Hoseah aliwataka Mawakili wapya kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maadili yaliyopo katika viapo vyao ili waweze kuepuka kujiingiza katika matatizo ya ukiukaji wa maadili ambayo yanaweza kuwasababishia kukosa sifa ya kuendelea na utoaji wa huduma hiyo.

Alisema watakaobainiki kukiuka maadili watachukuliwa hatua kwa mujibu na taratibu na Sheria zinazolinda viapo vyao kama Maafisa wa Mahakama na kuna uwezekano wa kuondolewa katika daftari la Mawakili.

Prof. Hoseah aliongeza kuwa TLS inaendelea kupambana na vishoka ambao wamekuwa wakiendesha vitendo haramu na visivyo vya kimaadili ya kiutendaji kazi za uwakili na kuchafua taaluma hiyo muhimu kwa maendeleo ya Nchi.

Alisema vitendo hivyo vimekuwa vikisababisha kushuka kwa hadhi ya taaluma ya Uwakili na kusababisha kutoaminika na Serikali na wadau mbalimbali katika jamii.

“Kuna baadhi ya watu wanaofanya kazi za uwakili ingawa wao sio mawakili, watu hawa wamekuwa wakifanya kazi mbalimbali za kiuwakili kama vile kuandaa na kuthibisha nyaraka na kushuduhia viapo. Wahalifu wa vitendo viovu ni watu wanaojifanya ni Mawakili lakini sio Mawakili, tunaendelea kupambana nao,” alisisitiza.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza katika hafla ya kuwapokea na kuwakubali Mawakili wapya 358 leo tarehe 2 Disemba, 2022 jijini Dar es Salaam.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Dkt. Eliezer Feleshi akieleza jambo katika hafla hiyo.
Rais wa Chama cha Mawakili wa Tanganyika (TLS), Prof. Edward Hoseah  akisisitiza jambo wakati wa hafla hiyo.
Meza kuu chini ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (juu) kipokea heshima kutoka kwa Mawakili wapya (chini).

Jopo chini ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe, Dkt. Eliezer Feleshi (juu) na Baraza la Elimu ya Sheria (chini) wakipokea heshima kutoka kwa Mawakili hao.

Mwakili wapya wakila kiapo mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo katika picha).

Wananchi (juu na chini) wakishuhudia matukio mbalimbali katika hafla hiyo.
(Picha na Innocent Kansha-Mahakama).







Hakuna maoni:

Chapisha Maoni