Jumamosi, 3 Desemba 2022

JAJI CHABA AWAASA WATUMISHI WA MAHAKAMA ZA WILAYA KUTOFANYA KAZI KWA MAZOEA

Na Mary Gwera, Mahakama-Morogoro

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania-Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba amewaasa Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya nchini kutofanya kazi kwa mazoea na badala yake wafanye kazi kwa ari na weledi ili wananchi wanaokuja kupata huduma katika Mahakama hizo wapate huduma zilizo bora.

Akizungumza wakati wa kuahirisha Mafunzo ya Huduma kwa Mteja kwa Watumishi wa Mahakama hizo jana tarehe 02 Desemba, 2022, Mhe. Chaba ambaye alimuwakilisha Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro alisema kuwa, ana imani kwamba, mafunzo yaliyotolewa na wawezeshaji yamegusa maeneo muhimu na kutoa uelewa wa namna ya kupambanua changamoto za kiutendaji na mabadiliko ya kifikra katika maeneo mbalimbali.

“Nina imani kuwa kufanyika kwa mafunzo haya kutakuwa chachu ya kuboresha huduma zitakazotolewa na Mahakama pamoja na wadau katika Mahakama hizi za Wilaya ili uwekezaji uliofanyika kwenye ujenzi wa majengo hayo ulete tija katika Mahakama hizo,” alisema Jaji Chaba.

Aliongeza kwa kuwasisitiza kuwa na ushirikiano miongoni mwa watumishi kwa watumishi pamoja na wadau wanaoshirikiana nao katika mnyororo wa Huduma za Haki ili kuzidi kuimarisha imani ya wananchi na wadau kutokana na uboreshaji wa huduma za Mahakama.

Kadhalika, aliwakumbusha watumishi hao walioshiriki katika Mafunzo ya huduma kwa mteja kuyatumia mafunzo hayo kama chachu ya utendaji kazi bora katika maeneo yao ya kazi na kuziishi vyema jitihada zinazofanywa na Mahakama ya Tanzania katika uboreshaji wa huduma za haki ili kuweza kuifikia dira yake ya kutoa Haki sawa kwa wote na kwa wakati.

Akitoa neno la shukrani, naye Mwakilishi wa Washiriki wa Mafunzo ambaye ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama mpya ya Wilaya ya Songwe, Mhe. Augustine Lugome amesema wamefurahishwa na mafunzo hayo na kuahidi kuyafanyia kazi vitendo ili kusudi lilikusudiwa na Mahakama lifikiwe kwa mafanikio.

“Katika kipindi cha siku tano (5) cha mafunzo haya tumejifunza mambo mengi yenye tija kupitia mada mbalimbali zilizotolewa na wawezeshaji ambazo ni pamoja na; Maadili ya watumishi, Huduma bora kwa mteja, Matumizi ya masjala na Serikali mtandao, Mradi wa uboreshaji wa Huduma za Mahakama, Matumizi sahihi ya TEHAMA na vifaa vya kielektroniki, Kushinda msongo wa mawazo na namna ya kupambana na sonona, Saikolojia na namna ya kuwianisha Maisha ya kazi na nje ya kazi na kadhalika. Hivyo tuwahakikishi tutayaishi yote tuliyofunzwa,” alisema Mhe. Lugome.

Mafunzo hayo yaliyoanza tarehe 28 Novemba, 2022 na kuhitimishwa tarehe 02 Desemba, 2022 yametolewa kwa sehemu ya Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya 18 kutoka Gairo, Songwe, Mkinga, Kilombero na Mvomero. Mafunzo kwa Watumishi wengine wa Mahakama za hizo mpya yataendelea kutolewa mfululizo kwa Watumishi wake katika vituo vya Kigoma, Bukoba na Musoma na mafunzo haya yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 23 Desemba, 2022 lengo likiwa  ni kuwakumbusha watumishi mbinu na namna bora ya kutoa huduma kwa wananchi.

Mafunzo haya yanafanyika kufuatia uzinduzi wa Mahakama mpya 18 za Wilaya zilizozinduliwa tarehe 25 Novemba, 2022 na  Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma. Mahakama zilizozinduliwa ni ;- Butiama, Rorya, Songwe, Gairo, Mkinga, Mvomero, Kilombero, Mbogwe, Nyang'hwale, Kyerwa, Itilima, Missenyi, Kaliua, Uvinza, Buhingwe, Kakonko na Tanganyika.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania-Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba akizungumza na Washiriki wa Mafunzo ya Huduma kwa Mteja wakati akihairisha Mafunzo hayo jana tarehe 02 Desemba, 2022 katika Ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro.
Washiriki wa Mafunzo ya Huduma kwa Mteja wakimsikiliza Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Messe Chaba alipokuwa akizungumza nao jana tarehe 02 Desemba, 2022 wakati wa hafla fupi ya kuahirisha mafunzo hayo.
Mwakilishi wa Washiriki wa Mafunzo ambaye ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama mpya ya Wilaya ya Songwe, Mhe. Augustine Lugome akitoa neno wakati wa hafla ya kuahirisha mafunzo ya huduma kwa mteja. Ameushukuru Uongozi wa Mahakama  kwa kuandaa mafunzo hayo ambayo wameahidi kuyafanyia kazi kwa vitendo kwa kuboresha huduma.

Afisa Utumishi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Rajab Singana akitoa mwongozo wa ratiba ya hafla fupi ya kuahirisha mafunzo iliyofanyika jana tarehe 02 Desemba, 2022.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu-Kanda ya Morogoro, Mhe. Augustina Mmbando (aliyesimama) akizungumza jambo wakati wa hafla fupi ya kuahirisha mafunzo ya huduma kwa mteja. Katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba na kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro, Mhe. Gabriel Malata.

PICHA ZA KUTUNUKIWA VYETI KWA WAHITIMU WA MAFUNZO YA HUDUMA KWA MTEJA KWA SEHEMU YA WATUMISHI WA MAHAKAMA MPYA ZA WILAYA.








Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania-Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba akiwatunuku vyeti baadhi ya Washiriki wa  mafunzo ya Huduma kwa Mteja yaliyotolewa kwa sehemu ya Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya nchini.

(Picha na Mary Gwera, Mahakama)

 

 

 

 

 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni