Jumatatu, 5 Desemba 2022

JAJI MLACHA AHIMIZA ARI MPYA KWA WATUMISHI MAHAKAMA ZA WILAYA MPYA

Na Faustine Kapama-Mahakama, Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha amewataka watumishi wanaohudhuria mafunzo ya huduma kwa mteja katika Kituo cha Kigoma kutekeleza majukumu yao kwa ari mpya ili kuiwezesha Mahakama ya Tanzania kufikia malengo ambayo imejiwekea.

Akizungumza wakati anatoa neno la ufunguzi wa mafunzo ambayo yamewaleta pamoja watumishi 34 kutoka Mahakama za Wilaya tano za Buhigwe, Kakonko, Uvinza, Kaliua na Tanganyika leo tarehe 5 Disemba, 2022 katika Kituo hicho, Mhe. Mlacha aliwahimiza washiriki hao kuwa wasikivu kwa vile yote watakayoelezwa na wawezeshaji ni sehemu ya Mpango Mkakati wa Mahakama.

“Ni imani yangu na Mahakama kwa ujumla mtatoka mkiwa watu wapya, ari mpya na uwezo mkubwa wa kufanya mambo ambayo yatakuwa tofauti yatakayoiwezesha Mahakama ya Tanzania kuvuka na kufikia malengo ambayo imejiwekea,” alisema.

Jaji Mfawidhi huyo alibainisha kuwa miongoni mwa malengo na mbinu za kufanikisha utekelezaji wa Dira na Dhima ya Mpango Mkakati wa Mahakama awamu ya pili 2020/2025 ni kuwajengea watumishi uwezo wa kufanya kazi zao vizuri. Akaeleza kuwa ndio maana ikaamuliwa kabla ya kuanza majukumu yao rasmi watumishi wa hizo Mahakama mpya wapewe mafunzo maalumu.

“Ni matarajio yangu baada ya mafunzo haya kila mshiriki atakuwa ameiva kwa kubadilika kifikra, kimtazamo na weledi na hivyo kuachana na utendaji wa kimazoea ambao ulichangia wananchi kukosa imani dhidi ya huduma zetu,” alisema.

Mhe. Mlacha aliishushukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kutoa fedha kupitia mkopo wa Benki ya Dunia ili kugharamia uboreshaji wa huduma za Mahakama, yakiwemo mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi watakaofanya kazi kwenye majengo ya Mahakama mpya za Wilaya.

Naye Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert chuma, akizungumza katika hafla hiyo fupi ya ufunguzi wa mafunzo hayo katika Kituo cha Kigoma, amewahimiza watumsishi hao kuwa mabalozi na nuru katika utendaji kazi.

Amesema mafunzo watakayopewa yakawe chachu kwao katika kuleta mabadiliko chanya na yenye tija kifikra na kimtazamo, hivyo kuacha kufanya kazi na kuwahudumia wananchi kwa mazoea.

“Uzuri wa majengo kama mlivyoyaona unapaswa kusaili ubora wa huduma zetu, kwa maana huduma mnazotoa ziendane na uzuri wa jengo. Haitoishi tu kuhudhuria mafunzo, elimu mtakayoipata muitumie kubadilisha mitazamo,” Mhe. Chuma alisema.

Alibainisha kuwa uboreshaji wa miundombinu unaoendelea hivi sasa ndani ya Mahakama ni utekelezaji wa nguzo ya kwanza ya Mpango Mkakati wa Mahakama ambao unalenga kusogeza huduma karibu na wananchi.

Msajili Mkuu alifafanua kuwa utekelezaji huo unakutana na nguzo ya pili ya upatikananji wa haki, yaani utoaji wa huduma za haki inayofikika na wananchi kupata huduma kwenye maeneo bora na wezeshi.

“Tunatambua uwepo wa matumizi ya Tekonolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ambayo yanarahisisha utoaji na upatikanaji wa huduma. Usogezaji huo unaendana na huduma bora na zenye tija kwa wananchi, hivyo kusaili nguzo ya tatu ya kurudisha au kujenga imani kwa umma,” alisema.

Mahakama ya Tanzania imeandaa mafunzo ya huduma kwa wateja ya siku 20 kwa watumishi watakaohudumu katika Mahakama za Wilaya 18 zilizojengwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia na kuzinduliwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma tarehe 25 Novemba, 2022.

Mafunzo hayo ambayo yatatolewa kwenye vituo vya Morogoro, Kigoma, Bukoba na Musoma yanalenga kuwaandaa na kuwapatia ujuzi watumishi hao ili watoe huduma bora kwa wananchi zinazoendana na uzuri wa majengo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha akizungumza wakati akitoa neno la ufunguzi wa Mafunzo kwa watumishi Kituo cha Kigoma leo tarehe 5 Disemba, 2022.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert chuma akisisitiza jambo wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo.
Mkurugenzi Msaidizi Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu akiwakaribisha watumishi kwenye mafunzo katika Kituo cha Kigoma.
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Bw. Moses Mashaka akitoa utambulisho wa watumishi wanaoshiriki mafunzo katika Kituo hicho.
Meza kuu chini ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (katikati) ikifuatilia mambo mbalimbali wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo. Wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania kutoka Kanda hiyo, Mhe. Stephen Magoinga (kushoto) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert chuma (kulia).
Meza kuu chini ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na Sekretarieti ya Mafunzo.
Meza kuu chini ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu Wakazi wa Mahakama za Wilaya Kaliua,  Buhigwe, Uvinza, Kakonko na Tanganyika, mtawaliwa, wanaohudhuria mafunzo hayo.
Meza kuu chini ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi kutoka Mahakama ya Wilaya Kakonko.

Meza kuu chini ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi kutoka Mahakama ya Wilaya Uvinza.
Meza kuu chini ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi kutoka Mahakama ya Wilaya Buhigwe.
Meza kuu chini ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi kutoka Mahakama ya Wilaya Tanganyika.
Meza kuu chini ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi kutoka Mahakama ya Wilaya Kaliua.

Meza kuu chini ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi wote kutoka Mahakama ya Wilaya tano za Buhigwe, Kakonko, Uvinza, Kaliua na Tanganyika wanaoshiriki mafunzo katika Kituo cha Kigoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni