Jumatatu, 5 Desemba 2022

WATUMISHI MAHAKAMA ZA WILAYA MPYA ‘KUBATIZWA’ KWA SIKU 20

Na Faustine Kapama-Mahakama, Kigoma

Mahakama ya Tanzania imeandaa mafunzo ya huduma kwa wateja ya siku 20 yenye lengo linaloelezewa kama ‘kuwabatiza’ upya watumishi watakaohudumu katika Mahakama za Wilaya 18 zilizojengwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia na kuzinduliwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma tarehe 25 Novemba, 2022.

Akizungumza kwenye mahojiano maalum mjini hapa leo tarehe 5 Novemba, 2022, Mkurugenzi Msaidizi Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu amesema mafunzo hayo yanalenga kuwaandaa na kuwapatia ujuzi watumishi hao ili watoe huduma bora kwa wananchi zinazoendana na uzuri wa majengo. Amesema mafunzo hayo yatatolewa kwenye Vituo vya Morogoro, Kigoma, Bukoba na Musoma.

"Tayari tumeshaanza kutoa mafunzo hayo kwenye Kituo cha kwanza cha Morogoro ambacho kimejumuisha watumishi 51 kutoka Mahakama za Wilaya tano za Gairo, Mvomero, Songwe, Kilindi na Kilombero.

"Leo tunaendelea na mafunzo haya kwenye Kituo cha Kigoma ambayo kama ilivyokuwa Morogoro yatachukua siku tano hadi Ijumaa tarehe 9 Disemba, 2022. Kituo hiki kina watumishi 34 ambao wametoka katika Mahakama za Wilaya tano za Buhigwe, Kakonko, Uvinza, Kaliua na Tanganyika," alisema.

Kwa mujibu wa Bi. Ngungulu, baadaye wataendelea kutoa mafunzo hayo kwenye Kituo cha tatu cha Bukoba kuanzia tarehe 12 hadi 16 Disemba, 2022 ambacho kina watumishi takribani 36 kutoka kwenye Mahakama za Wilaya nne ambazo ni Misenyi, Kyerwa, Nyang'wale na Mbogwe.

Amesema mafunzo katika Kituo cha nne na cha mwisho yatafanyika /’Musoma kuanzia tarehe 19 hadi 23 Disemba, 2022. Mkurugenzi Msaidizi huyo amesema Kituo hicho kinachojumuisha Mahakama za Wilaya nne za Busega, Itilima, Rorya na Butiama zenye watumishi wanaozidi 35.

"Tuna wawezeshaji wetu mahiri kutoka ndani na nje ya Mahakama ambao wamebobea katika maeneo mbalimbali ambao watawapitisha watumishi hawa katika mada kadhaa, ikiwemo Maadili na Kanuni za Maadili katika Mahakama; Huduma kwa Mteja; Wajibu na Majukumu ya Mahakama za Wilaya; Utamaduni wa Mahakama; Utii na Uvumilivu katika Mahala pa Kazi; Mabadiliko maeneo ya Kazi na Uboreshaji wa Huduma za Mahakama," amesema.

Mada zingine zitakazowasilishwa kwenye mafunzo hayo ni Matumizi ya Vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano; Utunzaji wa siri; Uelewa wa Mpango Mkakati wa Mahakama; Upatikanaji wa Haki na Uaminifu kwa Umma; Usimamizi Bora wa Mfumo wa Uendeshaji na Usajili wa Mashauri; namna ya kukabiliana na msongo wa mawazo na zingine nyingi.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Mahakama hizo 18 kwa mpigo iliyofanyika katika Mahakama ya Wilaya Busega ili kuwakilisha Mahakama zingine 17, Jaji Mkuu aliishukuru Serikali ya Tanzania kwa kutambua changamoto ya ukosefu na uchakavu wa miundombinu ya Mahakama, hivyo kuamua kuweka mipango ya ujenzi na ukarabati katika Mpango wake wa Maendeleo wa Miaka Mitano.

“Serikali ya Tanzania inatambua kuwa bajeti inayotoa kwa Mahakama isingeweza kuondoa changamoto kubwa ya uhaba na uchakavu wa majengo. Hali hii iliilazimu Serikali kutafuta fedha za ziada nje ya nchi ili kuondoa changamoto hizo,” alisema.

Aliishukuru Benki ya Dunia kwa kukubali kutoa mkopo wenye riba nafuu kwa Serikali ya Tanzania ambao umetumiwa na Mahakama ya Tanzania kujenga Mahakama hizo ili kutekeleza Mpango Mkakati wa Miaka Mitano kupitia Programu ya Maboresho (Tanzania Citizen-Centric Judicial Modernisation and Justice Delivery Project).



Mkurugenzi Msaidizi Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu akifafanua jambo wakati wa mahojiano hayo.

Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Jumanne Muna akielezea utaratibu utakavyokuwa wakati wa mafunzo kwenye Kituo cha Kigoma.
Washiriki wa mafunzo kutoka Mahakama ya Wilaya Uvinza.
Washiriki wa mafunzo kutoka Mahakama ya Wilaya Buhigwe.
Washiriki wa mafunzo kutoka Mahakama ya Wilaya Kakonko.
Washiriki wa mafunzo kutoka Mahakama ya Wilaya Tanganyika (juu na chini).

Washiriki wa mafunzo kutoka Mahakama ya Wilaya Kaliua (juu na chini).

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni