Alhamisi, 26 Januari 2023

DAR ES SALAAM YAZIZIMA UZINDUZI WIKI YA SHERIA

·Wananchi wafurika mitaani wakiandamana

·Jaji Mfawidhi atoa ujumbe mzito kwa wananchi

Na Dillon Uisso-Mahakama, Dar es Salaam

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi ametoa wito kwa wananchi wa Kanda hiyo kutembelea mabanda ya Wiki ya Sheria ili kupata elimu na ushauri wa kisheria na kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuongeza umakini na ubora katika Mhimili wa utoaji haki.

Mhe. Maghimbi ametoa wito huo katika uzinduzi wa Wiki ya Sheria katika Kanda ya Dar es Salaam, tukio lililohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Mahakama na Serikali, akiwemo Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Mhe. Ng’wilabuza Ludigija ambaye alikuwa mgeni rasmi akimwakilisha Mkuu wa Mkoa, Mhe. Amos Makala.

Viongozi wengine waliohudhuria hafla hiyo ni Majaji wa Kanda ya Dar-es-salaam pamoja na Divisheni za Mahakama Kuu, Naibu Wasajili, Mahakimu, watumishi wa kada mbalimbali pamoja na taasisi za kiserikali zinazohusika kwenye mnyororo wa utoaji haki pamoja na wananchi waliojitokeza kwa wingi.

Akizungumza wakati wa kumkaribisha mgeni rasmi, Mhe. Maghimbi alisema kuwa Mahakama ikiwa ndio chombo cha utoaji haki imekuwa mstari wa mbele kutekeleza takwa la kikatiba la utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi chini ya Ibara ya 107A (2) (d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisisitiza kuwa utatuzi mbadala wa migogoro kwa njia ya usuluhishi umekuwa ni chombo kikuu duniani, hivyo matumizi yake yaimarishwe ili kuleta ustawi wa jamii na kukuza uchumi endelevu kwani wadaawa hutumia muda mfupi kutatua migogoro na kuwawezesha kujikita katika shughuli za uzalishaji.

Kuhusiana na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Jaji Mfawidhi huyo aliwasihi wananchi kufika katika mabanda yaliyoandaliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kupata elimu kwa kuwa mashauri yote sasa yanasajiliwa kwa njia ya matandao na pengine kusikilizwa kwa njia ya Mkutano Mtandao.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mhe Ludigija alitoa rai kwa wananchi wa Mkoa wa Dar es salaam kutembelea viwanja hivyo ili kupata elimu na kujua dhima ya Mahakama kwa kauli mbiu ya mwaka 2023 ambayo ni “Umuhimu wa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya Usuluhishi katika Kukuza Uchumu Endelevu: Wajibu wa Mahakama na Wadau.” Aliendelea kusisitiza kwamba usuluhishi ni njia bora ya kuokoa muda, kukuza uchumi wa nchi na kudumisha mahusiano ya wananchi.

Mkuu wa Wilaya huyo alifurahishwa na kauli mbiu hiyo kwani Mahakama imetambua juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, katika kukuza uwekezaji na juhudi za kukuza uchumi endelevu.

Aliahidi kuwa wataendelea kuitangaza Mahakama kwa ujumla na hasa Kituo cha Usuluhishi ili wananchi wakimbilie zaidi kusuluhishwa migogoro yao, hivyo kudumisha amani nchini.

Maandamano hayo yaliyoanzia katika viwanja vya Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, maarufu Mwembeni yalihudhuriwa na mafuriko ya watu. Waandamanaji walipita katika mitaa mbalimbali kabla ya maandamano hayo kuhitimishwa katika Mahakama ya Hakimu Kisutu kwenye viwanja ambavyo vinatumika kutoa elimu na msaada wa kisheria katika kipindi chote cha Wiki ya Sheria kupitia mabanda ambayo yameandaliwa na Mahakama na wadau mbalimbali.

Waandamanaji wakipita katika mitaa mbalimbali jijini Dar es Salaam katika uzinduzi wa Wiki ya Sheria.
Bendi ya Jeshi la Polisi ikiongoza maandamano hayo. 
Yalikuwa mafuriko ya wananchi. 
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (wa pili kulia), Jaji Cyprian Mkeha (katikati) na Jaji Katharina Mteule (kushoto) wakikatiza mitaa wakiwa kwenye maandamano hayo.
Pasha pasha misuri ikiendelea baada ya kufika katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu (picha juu na chini).


Meza Kuu ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Mhe. Ng’wilabuza Ludigija (katikati) ikiimba wimbo wa taifa kabla ya uzindizi wa Wiki ya Sheria. Wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (wa tatu kushoto), Jaji Amir Mruma (wa tatu kulia), Jaji Agnes Mgeyekwa (wa pili kushoto), Jaji Cyprian Mkeha ( wa pili kulia), Jaji Biswalo Mganga (wa kwanza kushoto) na Jaji  Mustapha Ismail (wa kwanza kulia).

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Mhe. Ng’wilabuza Ludigija akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Wiki ya Sheria. Wangine wanaoshuhudia kuanzia kushoto ni Jaji Amir Mruma, Jaji Fatma Maghimbi, Jaji Mustapha Ismail, Jaji Boswalo Mganga na Jaji Cyprian Mkeha. 

Moja ya mabanda yaliyoandaliwa na Mahakama kutoa elimu na ushauri wa kisheria kwenye Wiki ya Sheria katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni