Alhamisi, 26 Januari 2023

MAJAJI MOROGORO WATOA SOMO MUHIMU UTATUZI WA MIGOGORO YA ARDHI

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

Katika kuadhimisha Wiki ya Sheria, Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro tarehe 24 Januari, 2023 walikutana na viongozi waandamizi wa Mkoa huo kutoa elimu ya sheria na namna bora ya kutatua migogoro ya ardhi ambayo imekithiri mkoani hapa.

Akizungumza katika Semina iliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda hiyo, Mhe. Paul Ngwembe alisema kuwa viongozi katika Mkoa huo wanamwakilisha Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo wapo kusimamia amani na utulivu wa nchi.

Alisema kuwa viongozi hao wana haki ya kuingilia mgogoro wowote unaoweza kuchangia uvunjifu wa amani ili kufanya usuluhishi na kurejesha amani iliyotoweka na kama itashindikana watapaswa kuupeleka mgogoro huo katika mamlaka inayohusika ili utatuliwe.

Jambo hilo liliungwa mkono na Jaji Gabriel Malata ambaye alifafanua kuwa Serikali inauwezo wa kutatua mgogoro wa ardhi kwa kuichukua ardhi husika na kuimiliki ikiwa mmiliki wake amashindwa kuiendeleza kwa mujibu wa masharti yaliyopo kwenye hati ya umiliki.

“Jukumu mama la kiongozi yeyote ni kuhakikisha amani na utulivu vinaendelea kuwepo katika himaya yake, hivyo nitoe rai yangu kuwa inapotokea migogoro yeyote tuwe mstari wa mbele kuitatua kwa njia ya usuluhishi na itakaposhindikana tuifikishe katika vyombo husika,” alisema Mhe. Malata.

Kwa upande wake, Jaji Messe Chaba aliwaasa viongozi hao kuwashirikisha wanasheria waliopo katika ofisi zao kwani watawasaidia kutatua changamoto nyingi zinazohitaji utatuzi wa kisheria kwa kuwa wana uelewa wa kutosha.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Fatma Mwassa alitoa shukrani kwa Jaji Mfawidhi na timu yake kwa kuupokea mwaliko na kutoa elimu kwenye mambo hayo ya msingi, hatua ambayo inaboresha mahusiano mazuri kati ya Serikali na Mahakama na kuomba utaratibu huo kuendelea.

“Tunatambua kuwa Mahakama ipo katika maadhimisho ya Wiki ya Sheria na sera kuu ni utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi, nasi tumeandaa mkutano huu ili tuweze kupata elimu. Elimu hii tutaitoa vijijini ili nao wapate kujua haya tuliyojifunza,” alisema.

Semina hiyo iliwakutanisha viongozi wa Mkoa huo, wakiwemo Wakuu wa Wilaya zote, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa na Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashari zote, Wenyeviti wa Halmashauri, Makatibu Tawala wa Wilaya, Maafisa Tarafa, Wakuu wa idara, taasisi na vitengo serikalini.

Viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mororogo (juu) wakimsikiliza Jaji Mfawidhi, Mhe. Paul Ngwembe (chini).
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (juu) akizungumza katika Semina iliyoandaliwa na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Fatma Mwassa (chini).
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Fatma Mwassa akimsikiliza kwa makini Jaji Ngwembe.

Wajumbe katika semina hiyo (juu na chini) wakimsikiliza Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Gabriel Malata (picha chini aliyesimama).


Meza Kuu ikifuatilia hoja mbalimbali katika semina hiyo. Kutoka kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Messe Chaba, Jaji Mfawidhi, Mhe. Paul Ngwembe, Mkuu wa Mkoa, Mhe. Fatma Mwassa na Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe, Gabriel Malata.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni