Ijumaa, 27 Januari 2023

ELIMU KUHUSU USULUHISHI YASAMBAA CHUO CHA UALIMU MATOGORO

Na Catherine Francis-Mahakama Kuu, Songea

Katika kuendelea kuadhimisha Wiki ya Sheria nchini watumishi na wadau wa Mahakama Kanda ya Songea wamefika katika Chuo cha Ualimu Matogoro kutoa elimu kuhusu utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea, Mhe. Michael Manjale aliwaambia wanafunzi katika Chuo hicho kuwa kauli mbiu ya mwaka 2023 imejikita katika kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi, hivyo kama walimu watarajiwa hawana budi kujifunza namna bora ya kutatua migogoro nje ya Mahakama.

Alisisitiza kuwa walimu ni kundi muhimu kwakuwa wao ndiyo walezi wakubwa wa jamii nzima, hivyo hawana budi kutumia busara na hekima katika kushughulikia na kutatua matatizo ya wanafunzi wao ili kuweza kujenga kizazi kilicho bora.

Mhe. Manjale aliendelea kusema kuwa wanafunzi wamekuwa na migogoro mingi baina ya wao kwa wao au wao na walimu wao, hivyo wakiwa shuleni walimu ndiyo wasuluhishi wa matatizo. Aidha, alitumia nafasi hiyo kufundisha sheria ya mtoto pamoja na wajibu wao kama wazazi nini wanatakiwa kufanya.

Naye Wakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Mashtaka Ruvuma, Mhe.  Hebel Kihaka alisema wapo tayari kuwashauri wateja wao juu ya umuhimu wa usuluhishi kwa yale makosa ya jinai ambayo yanaweza kumalizika kwa njia hiyo kulingana na mwongozo wa kisheria wa uendeshaji wa makosa ya jinai.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Songea Mjini, Mhe. Diana Manase alifafanua maana ya Wiki ya Sheria na kwanini Mahakama inaadhimisha Wiki hiyo ya utoaji elimu ya sheria kila mwaka nchini.

Katika maelezo yake, Mhe. Manase alisema maadhimisho hayo yapo mahususi kwa ajili ya kutoa elimu na msaada wa kisheria bure na wananchi hupata nafasi ya kujifunza majukumu na utendaji kazi wa kila ofisi.

Wakati wa zoezi hilo la utoaji elimu, Walimu na Wanafunzi walipata nafasi ya kuuliza maswali kuhusu mambo mbalimbali, ikiwemo utaratibu wa kufungua na kusikilza mashauri kwa njia ya kielektroniki, jinsi ya kufungua mashauri yanayohusu matunzo ya mtoto pamoja na utaratibu uliopo kwenye ofisi ya Wakili Serikali kuwatetea wananchi ambao hawana uwezo wa kujigharamia.

Baadhi ya Wanafunzi wa Chuo cha Ualimu Matogoro waliohudhuria hafla hiyo.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea, Mhe. Michael Manjale akitoa elimu kwa Wanafunzi na Walimu wa Chuo cha Ualimu Matogoro.
Baadhi ya Walimu wa Chuo cha Ualimu Matogoro waliohudhuria utoaji wa elimu.
Mwanafunzi Aloyce Cassian akiuliza swali kwa watoa elimu.
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Songea Mjini, Mhe. Diana Manase akifafanua jambo.
Wakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Mashtaka Ruvuma, Mhe. Hebel Kihaka akitoa elimu katika chuo hicho.

Wakili wa Kujitegemea, Mhe. Dickson Ndunguru akitoa elimu kwa Wanafunzi na Walimu wa Chuo cha Ualimu Matogoro.

Watumishi na Wadau wa Mahakama waliotoa elimu katika Chuo cha Ualimu Matogoro wakiwa katika picha ya pamoja.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni