Ijumaa, 27 Januari 2023

MGOGORO BONDE LA MTO RUVU UTATULIWE KWA USULUHISHI

Na Eunice Lugiana-Mahakama, Kibaha

Wakati maadhimisho ya Wiki ya Sheria yakielekea ukingoni, Timu ya utoaji elimu kutoka Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha imeshauri mgogoro kati ya wakulima na wafugaji katika Bonde la Mto Ruvu utatuliwe kwa njia ya suluhishi.

Mgogoro huo umebainishwa baada ya Timu hiyo kufika katika Kijiji cha Ruvu Stesheni kwa lengo la kutoa elimu na msaada wa kisheria kwenye maeneo mbalimbali.

Akizungumza kwenye mkutano huo, Hakimu Mkazi kutoka Mahakama ya Mwanzo Magindu, Mhe. Jafari Msisi, ambaye ni miongoni mwa Timu hiyo, alisisitiza kuwa migogoro kama hiyo ya wakulima na wafugaji ni bora ikatatuliwa kwa njia ya usuluhishi badala ya kupelekwa mahakamani.

“Ikifanyika vinginevyo Mahakama itatoa uamuzi na kumpa mmoja ushindi na mwingine akikosa inaweza kukaribisha uhasama na pengine wadaawa kuzidi kutokuelewana,” alionya.

Awali, Mwenyekiti wa Kijiji hicho aliyejitabulisha kwa jina moja la Abas aliieleza Timu hiyo kuwa mgogoro huo ni wa muda mrefu na uamuzi ulishatolewa lakini wafugaji wamekuwa hawako tayari kuutekeleza.

Mwenyekiti huyo alibainisha kuwa kuna tamko lilitoka serikalini kuwataka wafugaji wote wahame katika Bonde la Mto Ruvu, lakini mpaka sasa wapo na wanaingiza mifungo yao mashambani.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo, kutokana na sitofahaiu hiyo wakulima aliamua kufanya maridhiano kwa kuunda kamati maalumu kushughulikia mgogoro huo lakini wafugaji bado hawako tayari, suala linaloleta ugumu na uadui.

Katika hatua nyingine, Mahakama ya Wilaya Mkuranga imetembelea maeneo mbalimbali wilayani humo na kutoa elimu za kisheria katika maadhimisho ya Wiki ya Sheria nchini.

Hayo yamedhihirika katika Shule ya Sekondari Mwinyi iliyoko katika Wilaya Mkuranga ambapo jopo la watoa elimu likiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya hiyo, Mhe. Herieth Mwailolo lilitembelea shule hiyo.

Akizungumza katika eneo hilo, Mhe. Mwailolo amesema Mahakama hiyo imedhamiria kufika maeneo muhimu yenye uhitaji wa elimu ya kisheria, ikiwemo mashuleni na stendi za mabasi, ambayo yanahitaji kupewa kipaumbele.

Amesema katika shule hiyo, wanafunzi wa kike wamekuwa na shauku ya kujua sheria za mirathi na kama sheria inamruhusu mtoto wa kike kurithi mali.

Naye Mwakilishi wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU), Bi. Euphrazia Kakiko, amesema rushwa ya ngono huchangia kudidimiza uchumi wa taifa na kusababisha wanafunzi kutofanya vizuri kwa kutarajia kufaulu kwa kutoa rushwa, hivyo hupelekea kupata viongozi wabovu baadaye.

Akawataka wanafunzi hao kusoma kwa bidii na kupinga vikali vitendo vya rushwa na pale wanapoona kuna viashiria wasisite kutoa taarifa kwenye mamlaka husika ili kukomesha vitendo hivyo.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Magindu, Mhe. Jafari Msisi akisikiliza swali lililoulizwa na wananchi wa Kata ya Ruvu katika mkutano huo.
Mwenyekiti wa Kijiji Cha Ruvu Ndugu Abas akifuatilia utoaji wa elimu wakati wa Wiki ya Sheria.
Baadhi ya Wananchi wa Kijiji cha Ruvu Stesheni wakisikiliza elimu iliyokuwa inatolewa.
Mwakilishi kutoka TAKUKURU, Bi. Euphrazia Kakiko akieleza jambo wakati wa kutoa elimu katika Shule ya Sekondari Mwinyi.
Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Mwinyi Wilaya ya Mkuranga wakisikiliza kwa makini elimu inayotolewa na timu ya wawezeshaji katika Wiki ya Sheria.

Utoaji wa elimu ukiendelea maeneo ya stendi ya Mkuranga. 

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni