Ijumaa, 27 Januari 2023

ELIMU YA SHERIA YATOLEWA KILA MAHALI MBEYA

Na Ibrahim Mgallah, Mahakama Kuu Mbeya

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, kwa kushirikiana na wadau wake inaendelea na zoezi la utoaji elimu ya sheria katika maeneo mbalimbali ya jijini hapa ikiwa sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria.

Zoezi hilo lilianza tarehe 22 Januari 2023.  Utoaji elimu umejikita kwenye kauli mbiu ya mwaka 2023 inayosema, “Umuhimu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi katika kukuza uchumi endelevu: Wajibu wa Mahakama na wadau.”

Elimu ya sheria imeendelea kutolewa katika kituo cha mabasi Kabwe na katika mashule, ikiwemo Shule za Sekondari Ivumwe, Ikuti, Tulia Ackson na Itende. Vilevile elimu ya sheria imetolewa kwa wafanyakazi wa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya na kupitia vituo vya Redio Baraka fm na Rock fm.

Akitoa elimu ya sheria katika Hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe, Dkt Lilian Mongella ameishauri jamii kutumia njia ya usuluhishi katika kutatua migogoro yao mbalimbali ili kuokoa muda na gharama.

“Tunawahamasisha zaidi wadaawa wanaotafuta kutatatua migogoro yao wakimbilie kwanza kwenye kuisululisha ili kuokoa muda na gharama, jambo litakalopelekea kuokoa uchumi wao,’’ alisema Jaji Mongella.

Watu wote waliofikiwa na elimu ya sheria wameipongeza Mahakama kwa mpango huo kwani utasaidia jamii kuwa na amani, umoja na mshikamano.  Zoezi la utoaji elimu linaendelea hadi ifikapo tarehe 29 Januari, 2023.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe, Dkt Lilian Mongella akitoa elimu ya sheria kwa wafanyakazi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya.
Mahakimu na wadau wakiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi.
Mahakimu wakitoa elimu katika Kituo cha Redio Rock Fm.

Watumishi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya wakisikiliza elimu ya sheria.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni