Ijumaa, 27 Januari 2023

WAZIRI WA KATIBA AWATAKA WANANCHI KUTUMIA NJIA MBADALA KUTATUA MIGOGORO

Na Tiganya Vincent-Mahakama -Dodoma

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amewataka wananchi kutumia njia mbadala katika utatuzi wa migogoro ili kuwawezesha kuwa na muda mwingi katika utekelezaji wa shughuli za kujiingizia kipato.

Ametoa kauli hiyo jana tarehe 27 Januari 2023 mjini hapa wakati wa ziara yake ya kutembelea maonesho ya Wiki ya Sheria yanayoendelea katika Viwanja vya Nyerere Square.

Mhe. Dkt. Ndumbaro alisema kama kauli mbiu ya mwaka huu inavyosema umuhimu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi katika kukuza uchumi endelevu; wajibu wa Mahakama na Wadau, Wizara ya Katiba na Sheria imejipanga kuhakikisha kuwa inasisitiza matumizi ya njia mbadala katika kumaliza migogoro kwenye jamii.

Alisema njia mbadala zinaimarisha urafiki, mashauri humalizika haraka na kutumia gharama nafuu, hivyo kuwezesha pande zote kukuza uchumi wao na Taifa kwa ujumla.

Mhe. Dkt.Ndumbaro aliongeza kuwa Serikali imejipanga katika kuhakikisha inasajili wasuluhishi wa migogoro kwa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuhakikisha huduma hiyo inawafikia wananchi wengi.

“Hii mtu akitaka kufanya anaingia katika Tovuti ya Wizara na kujisajili na wakiridhika kama wana sifa wanasajiliwa kama wasuluhushi na tunawatumia vyeti vyao kwa njia ya mtandao ili waanze kuwahudumia Watanzania katika suala la usuluhishi,” alisema.

Katika hatua nyingine Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Ndumbaro amemhakikisha mwananchi aliyetaka vyeti vya kuzaliwa kutoka Wakala wa usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) vitolewe karibu na maeneo wanayoishi ili kuwapunguzia mzigo wa nauli ya kusafiri kutoka vijijini kutafuta huduma hiyo mijini.

Awali Leonard Motto alisema kuwa amekuwa akitumia kiasi cha shilingi elfu 70 kwa safari na kuja na kurudi kwake kwa ajili ya nauli kufuatilia cheti cha RITA Dodoma mjini na anapofika wakati mwingine anaelezwa akifuate cheti ni baada ya siku saba, jambo ambalo linamsababishia gharama.

Alisema ni vema RITA wakaweka utaratibu ambao utakuwa rafiki na sio mzigo kwa mwananchi anapotaka cheti cha kuzaliwa kutoka RITA ili akipate na  kurudi kwake kwa ajili ya kuendelea na majukumu merngine.

Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro (kushoto aliyekaa) akimsikiliza mzee Leonard Motto (kulia aliyekaa) wakati alipopendekeza RITa iweke utaratibu wa kutoa vyeti vya kuzaliwa siku moja.
Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro(kulia aliyekaa) akitoa maagizo kwa watumishi wa Shule Kuu ya Sheria kwa Vitendo wakati wa ziara ya kukakugua mabanda yanayotoa elimu wakati wa Wiki ya Sheria.


Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro (kushoto) akipokea maoni ya mzee Leonard Motto (kulia) wakati alipopendekeza RITA iweke utaratibu wa kutoa vyeti vya kuzaliwa siku moja

(Picha na Tiganya Vincent)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni