Ijumaa, 27 Januari 2023

WANANCHI WAISHUKURU MAHAKAMA KWA KUANDAA WIKI YA SHERIA

Na Francisca Swai-Mahakama, Musoma

Wananchi wameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kuandaa Wiki ya Sheria kwa ajili ya utoaji elimu na msaada wa kisheria bure na kwa urahisi.

Akitoa shukrani hizo, Mkazi wa Musoma Mjini, Bi. Veronica John amesema kuwa elimu inatolewa kwa uhuru, kwani watumishi pamoja na wadau wanakuwa na muda wa kutosha kusikiliza, kutoa maelezo, ufafanuzi na ushauri wa masuala mbalimbali.

“Hali niliyokuta ni tofauti kabisa na pale watumishi hawa wakiwa maofisini ambapo wanakuwa na mizunguko na shughuli nyingi,” alisema baada ya kutembelea mabanda mbalimbali katika Viwanja vya Mukendo ambayo yameandaliwa na Mahakama na wadau wake.

 Naye Mtendaji wa Chemba ya Wafanyabiashara kwenye Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) Mkoa wa Mara, Bw. Francis Ngowi amesema maonesho hayo kila mwaka yamekuwa na manufaa kwa kuwakutanisha wadau mbalimbali pamoja, kufahamiana tofauti na kila mmoja akiwa ofisini kwake.

Amesema hatua hiyo inawawezesha kuwahudumia wananchi kwa pamoja, hivyo mwananchi akitembelea maonesho hayo ya Wiki ya Sheria anaweza kupata huduma nyingi kwa wakati mmoja.

Kwa upande wake, Wakili Christopher Waikama ametoa wito kwa wananchi kuendelea kutembelea maonesho hayo ili kupata ushauri wa masuala mbalimbali hasa namna ya kufanya usuluhishi ili kupunguza migogoro mikubwa hasa iyohusiana na ardhi.

Amesema mwananchi akitembelea maonesho hayo ataweza pia kujifunza vitu mbalimbali kutoka kwa wadau wanaoshiriki kama vile Jeshi la Polisi, Mawakili wa Kujitegemea, Afya, TAKUKURU, Msaada wa Kisheria, RITA, NIDA na wengine wengi.

Naye Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Musoma Mjini, Mhe. Bahati Bwire na Hakimu Mkazi, Mhe. Gibson Ngojo, wanaoshiriki kutoa elimu katika Viwanja hivyo wamesema mwitikio wa wananchi ni mkubwa na wengi wana matatizo ya ndoa, talaka, mirathi na ardhi.

Maonesho hayo ya Wiki ya Sheria yanatolewa katika maeneo mbalimbali ikiwemo viwanja vya Mukendo Musoma Mjini, taasisi za elimu katika shule za Msingi, Sekondari na Vyuo na stendi mbalimbali ndani ya Mkoa wa Mara.

Mtumishi kutoka TAKUKURU, Bw. Amos Ndege (aliyesimama katikati) akitoa elimu katika Shule ya Msingi Nyasho B iliyoko Musoma Mjini.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (wa kwanza kulia) akipata ufafanuzi wa matumizi ya vifaa vya zimamoto katika banda ya wadau wa Jeshi la Polisi, Zimamoto na Dawati la Jinsia.
Mkuu wa Mkoa wa Mara, Meja Jenerali Suleiman Mzee akipata huduma za afya katika banda la wadau wa Afya lililoko katika Viwanja vya Mukendo Musoma Mjini.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara, Bw. Msalika Makungu (mwenye miwani) akipata maelezo kutoka kwa Hakimu Mkazai, Mhe. Gibson Ngojo (mwenye fulana nyeupe) kuhusiana na huduma zinazotolewa katika banda hilo la Ndoa, Talaka na Mirathi.
Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama Kuu Musoma Bw. Simon Lubili (anayeandika) akimsikiliza na kumhudumia mteja, Bi. Veronica John (aliyejifunga lemba) alipotembelea banda ya maboresho na malalamiko katika Viwanja vya Mukendo Musoma Mjini.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (wa tatu kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na wadau kutoka banda la Chemba ya Wafanyabiashara TCCIA. Mwenye fulana ya rangi ya bluu ni Mtendaji wa Chemba ya Wafanyabiashara Mara, Bw. Francis Ngowi.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni