Alhamisi, 26 Januari 2023

KUMEKUCHA MAHAKAMANI KISARAWE

·Mahakimu wazama vijijini kutoa elimu ya sheria

·Mwitikio wa wananchi washangaza

Na Faustine Kapama-Mahakama

Mahakimu katika Mahakama ya Wilaya Kisarawe wameamua kuzama vijijini kutoa elimu na msaada wa kisheria kama sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria yanayofanyika nchini kote.

Timu ya Mahakimu hao ikiongozwa na Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Devotha Kisoka tayari imeshatembelea Kambi ya Jeshi ya Kisarawe na Shule ya Sekondari ya Wasichana Joketi Mwegelo kabla ya kusambaa vijijini.

“Sisi tumeamua kwenda vijijini kuelimisha wananchi kwenye masuala mbalimbali ya kisheria na tukiwa huko tutatoa pia huduma za kisheria na bahati nzuri tumeambatana na Wakili Msomi wa Kujitegemea, Mhe. Moses Chunga,” amesema.

Ameeleza kuwa timu yake ambayo inajumuisha pia Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Frank Lukosi, Hakimu Mkazi Manifred Sanga na Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo, Mhe. Zaituni Khatibu imeshatembelea Kijiji cha Masaki kilichopo katika Kata ya Sungwi.

“Kote huko tulikopita mwitikio wa wananchi ni mkubwa sana, hatukutegemea kwa kweli. Wananchi wanahamu ya kujua masuala mbalimbali yakiwemo ya ardhi, miradhi, ndoa na taraka na mengine mengi. Sisi tupo kwa ajili ya kuwatumikia na tumejipanga vizuri,” alisema Mhe. Kisoka.

Amesema kwa sasa wapo katika Kijiji cha Boga kilichopo Tarafa ya Manelumango kwa ajili ya kuendeleza zoezi la utoaji elimu kwa wananchi. Mhe. Kisoka ameahidi kufika katika maeneo yote ili elimu ya kisheria iweze kuwafikia wananchi wengi ambao hawana uelewa wa kutosha kwenye masuala hayo.

Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kisarawe, Mhe. Devotha Kisoka akizungumza na wananchi waliojitokeza katika Mahakama hiyo kupata elimu ya kisheria wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Sheria.
Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Manfred Sanga  (kushoto waliosimama) akisisitiza jambo wakati zoezi la utoaji elimu ya kisheria likiendelea.
Wanafunzi katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Joketi Mwegelo (juu na chini) wakipate elimu ya sheria kama sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria nchini.

Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo, Mhe. Zaituni Khatibu (katikati) akizungumza na wananchi (chini) katika Kijiji cha Sungwi wakati wa zoezi la utoaji wa elimu ya kisheria.

Wananchi wa Kijiji cha Sungwi wakiwasikiliza Mahakimu waliokuwa wanatoa elimu kwenye masuala mbalimbali ya kisheria. 
Utoaji wa elimu ya sheria katika Kijiji cha Boga kilichopo Tarafa ya Manelumango ukiendelea.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni