Jumatano, 25 Januari 2023

MAHAKAMA KIBAHA YATEMBELEA GEREZA LA MAHABUSU MKUZA

·Mahabusu wafunguka kuhusu dhamana, kukamatwa tena baada ya kuachiwa

Na Eunice Lugiana-Mahakama, Kibaha

Katika kutoa elimu wakati wa Wiki ya Sheria nchini, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha imetembele Gereza la Mahabusu Mkuza na kusikiliza kero zao, ikiwemo ukosefu wa dhamana kwenye makosa yanayodhaminika na ucheleweshaji wa mashahidi kuletwa mahakamani.

Akizungumza katika Gereza hilo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Joyce Mkhoi amesema kuna kesi nyingine zinazofikishwa mahakamani ambazo zinaweza kumalizika kwa njia ya usuluhishi.

“Kwa mfano polisi wanaweza kufanya usuluhishi kama wakati mwingine wahusika wakikubaliana kulipana fidia kwa makosa madogo kuliko kusubiri shauri lifike mahakamani, hii inapoteza muda,” alisema.

Naye Mwendesha Mashtaka Kiongozi, Bi. Auralia Makundi alibainisha kuwa kama mshtakiwa anataka kukiri kosa anaweza kuandika barua kwa Mkuu wa Mashtaka wa Mkoa na kisha majadiliano hufanyika na kama wakikubaliana shitala litaondolewa kwa kulipa kiasi fulani cha fedha.

“Kama majadiliano yatashindikana basi nyaraka zote zilizokuwa zinatumika kwenye mchakato huo zitateketezwa na jambo hilo litabaki kuwa siri na kesi itaendelea,” alisema.

Kwa upande wao, Mahabusu wa gereza hilo wameomba upande wa mashtaka kufungua dhamana kwa mashauri ambayo yanadhaminika na kuleta mashahidi mahakamani kwa wakati. Wamelalamikia pia suala la wao kukamatwa tena mara wanapoachiwa na Mahakama au pale upande wa mashtaka unapoamua kuondoa shitaka.

Katika hatua nyingine, timu ya waelimishaji kutoka Mahakama hiyo imetembelea Kijiji cha Soga na kupokea malalamiko kutoka kwa wananchi. Akiongea katika ofisi ya Mtendaji wa Kijiji hicho, Mzee Kufa Kulala amesema  wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi wengi hawajui taratibu na sheria za ardhi, hivyo husababisha migogoro kuwa mikubwa zaidi.

Aidha amesema wananchi wanalalamikia ada za ufunguaji wa mashauri kuwa kubwa ukilinganisha na hali ya uchumi wa sasa, hivyo kupelekea juhudi zinazofanywa katika kutatua migogoro kutokuleta matunda katika Kijiji hicho.

Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya Kibaha zimejikita kutoa elimu hasa katika Wilaya ya Kibaha Vijijini maana ndio maeneo ambayo yamekuwa na mgogoro mkubwa wa ardhi.

Timu ya watumishi kutoka Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha ikiwa katika picha ya pamoja na maafisa Magereza baada ya kutembele Gereza la Mahabusu Mkuza.
Mzee Kufa Kulala akieleza changamoto zinazolikabili Baraza la Usuluhishi Soga


Hakimu Mkazi, Mhe. Felister Ng'hwelo akitoa elimu katika viwanja vya ofisi ya Mtendaji Soga Kibaha Vijijini.
Hakimu Mkazi Mariam Nguvu akitoa elimu kuhusu wosia katika viwanja hivyo.


(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni