Jumatatu, 23 Januari 2023

MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA ASISITIZA MAMBO MATATU MUHIMU KWA WANANCHI

Na Faustine Kapama-Mahakama, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel leo tarehe 23 Januari, 2023 ametembelea mabanda ya maonesho ya utoaji wa elimu ya kisheria katika Viwanja vya Nyerere Square jijini hapa na kusisitiza mambo matatu, ikiwemo wananchi kuendelea kuuamini Mhimili wa Mahakama kama chombo pekee cha utoaji haki nchini.

Akizungumza na Waandishi wa Habari kwenye viwanja hivyo katika siku ya pili ya Wiki ya Sheria baada ya kutembelea madanda kadhaa, Prof. Ole Gabriel amewaambiwa wananchi kuwa uamuzi wa kisheria unaotolewa na Mahakama haufanywi kiholela wala kuangalia utashi wa mtu, bali hufuata sheria na ushahidi.

“Mwananchi anapaswa kutambua kwamba pale anapofuatilia haki yake ni muhimu kwake kutoa ushahidi wa kile anachoamaini kwamba ni haki yake. Anapokwepa kutoa ushahidi inakuwa ngumu kwa uamuzi kufanyika,” amesema.

Amewaomba Watanzania kuendelea kuilinda amani iliyopo nchini na kusisitiza kuwa haki ndiyo hasa inayoleta amani, hivyo ni muhimu kuendelea kuuamini Mhimili wa Mahakama kwa kuzingatia kuwa mtu anapokwazika kwenye mifumo ya kibiashara au yoyote ile huchagua kwenye mahakamani kutafuta haki yake.

“Kwa hiyo tunawaomba wananchi waendelee kuuamini Mhimili wa Mahakama kwamba unatenda haki na pale ambapo kunaweza kuwepo na tashwishwi yoyote kwa baadhi ya watu, kwa sababu wale wanaofanya kazi mahakamani ni binadamu, tunayo mifumo mizuri sana ya kurekebishana ndani ya Mhimili,” amesema.

Akizungumzia suala la maadili, Mtendaji Mkuu amebainisha kuwa moja ya majukumu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama ni kufuatilia mienendo ya watumishi na kulinda taswila la Mhimili huo. Akagusia pia uwepo wa Kamati za Maadili katika ngazi ya Mkoa na Wilaya ambapo Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya huwa ndiyo wenyeviti katika ngazi hizo.

Aidha, katika eneo la kiutawala, Prof. Ole Gabriel ameeleza kuwa wamewekeza kwenye mafunzo kwa kada zote za watumishi wakiwemo wadereva, makatibu mahsusi, watunza kumbukumbu na wengine ili kuwaelewesha nini hasa Watanzania wanachokitarajia kutoka kwao katika suala zima la utoaji haki.

“Tumewekeza zaidi katika kuwaelimisha na kuwaelewesha umuhimu wa maadili ndani ya Mahakama kwa sababu Mahakama ni eneo takatifu, hii itawezesha kutekeleza ile nguzo ya tatu ya mpango mkakati kuhusu kuimarisha imani kwa wadau. Tumejipanga kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati, kwa uwazi na bila tashwishwi zozote za rushwa,” amesema.

Mtendaji Mkuu ametumia fursa hiyo kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwezeshaji mkubwa ambao umechochea uboreshaji wa miundombinu mbalimbali ya Mahakama ikiwemo ujenzi wa majengo ya kisasa.

“Mahakama hatufanyi biashara, hatuuzi haki, hatuuzi magari, mahindi wala ng’ombe, sisi tunatoa haki. Kwa hiyo miundombinu yetu inategemea uwezeshwaji kutoka serikalini. Mimi kama Afisa Masuhuli lazima nitoe shukrani kwa Serikali, kwa kweli tunawezeshwa vizuri, tunatumia fedha hizo vizuri na matokeo yanaonekana. Bila uwezeshwaji huo tungekuwa na changamoto kubwa zaidi,” amesema.

Prof. Ole Gabriel akabainisha pia kuwa ujenzi wa Mahakama katika ngazi mbalimbali kama Mahakama za Mwanzo unaendelea kwa kazi kubwa, ambapo Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki sita vimeshajengwa mpaka sasa na vingine 12 vitajengwa kufika mwaka 2024, lengo ni kusogeza huduma za utoaji haki karibu na wananchi.

Mtendaji Mkuu aliwasili katika Viwanja vya Nyerere Square majira ya saa tatu asubuhi na kutembelea madanda ya maonesho kadhaa ambayo yameandaliwa na wadau mbalimbali wa Mahakama wakiwemo Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Bandari, Mkemia Mkuu wa Serikali, Chuo Kikuu cha Dodoma, Mamlaka ya Kuthibiti na Kupambana na Dawa ya Kulevya, Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.

Akiwa katika mabanda hayo, Prof. Ole Gabriel alipata maelezo namna taasisi hizo zinavyofanya kazi kutoka kwa watendaji mbalimbali. Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu alipata fursa ya kuuliza maswali ili kupata ufafanuzi wa hoja mbalimbali.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akisisitiza jambo alipokuwa anaongea na Waandishi wa Habari katika Viwanja vya Nyerere Square leo tarehe 23 Januari, 2023 jijini Dodoma.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa katika banda la Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TAWJA).
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa katika banda la Chuo cha Uongozi wa Mahakama Luchoto (IJA).
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akipata maelezo katika banda la Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA).
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa katika banda la Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali. Picha chini akipata maelezo kutoka kwa watumishi wa Chuo Kikuu cha Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiuliza swali alipokuwa katika banda la Mamlaka ya Kuthibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akipata maelezo katika banda la Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa. 
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiuliza swali alipokuwa katika banda la Tume ya Taifa ya Uchaguzi. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni