Ijumaa, 17 Februari 2023

JAJI MFAWIDHI AKUTANA NA VIONGOZI WA MAHAKAMA MKOA WA MANYARA

Na Christopher Msagati-Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. John Kahyoza leo tarehe 17 Februari, 2023 amekutana kwa mara ya kwanza na viongozi wa Mahakama Mkoa wa Manyara kujadili mambo mbalimbali ya kiutendaji.

Akizungumza katika kikao kazi hicho, Mhe. Kahyoza alisisitiza watumishi kufanya kazi kwa ushirikiano na kuzingatia nidhamu ili kufanikisha malengo ya Kanda na kuboresha huduma za utoaji haki kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi huyo alisema kuwa ni jukumu la viongozi wote kusimamia masijala zao kwa ufasaha, ikiwemo vielelezo vyote vinavyofikishwa mahakamani kila siku.

Viongozi hao walitumia nafasi hiyo kupitia na kujadili maoteo ya bajeti ya Mahakama Mkoa wa Manyara na Wilaya zake kwa mwaka wa fedha 2023/2024.

Kadhalika, walitumia kikao hicho kufahamiana kwa vile ni mara ya kwanza kwa viongozi hao kukutana tangu kuanzishwa kwa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara mwezi Novemba, 2022.

Kikao hicho kilichofanyika majira ya asubuhi katika katika Ukumbi wa Mahakama Kuu Manyara kimehudhuriwa na Jaji wa Mahakama Kuu katika Kanda hiyo, Mhe. Gladys Barthy, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Bernard Mpepo, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara, Mhe. Mariam Lusewa pamoja na Mtendaji wa Mahakama Kuu Manyara, Bw. Jacob Swalle.

Viongozi wengine waliokuwepo ni pamoja na Mahakimu Wakazi Wafawidhi, Maafisa Utumishi na Tawala wa Wilaya za Babati, Hanang, Mbulu, Kiteto na Simanjiro katika Mkoa wa Manyara.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. John Kahyoza (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi waliohudhuria katika kikao kazi hicho.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. John Kahyoza akisisitiza jambo wakati wa kikao cha viongozi wa Mahakama Mkoa wa Manyara.
Baadhi ya viongozi wa Mahakama Mkoa wa Manyara wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. John Kahyoza.

Wajumbe wa kikao wakifuatilia uwasilishaji wa maoteo ya bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024 katika kikao kazi hicho.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama Dar es Salaam).

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni