Jumatatu, 20 Februari 2023

MENEJIMENTI YA MAHAKAMA KANDA YA MUSOMA YAKUTANA

·Jaji Mfawidhi aonya matumizi ya ofisi mtandao kutokwamishwa

Na. Francisca Swai-Mahakama, Musoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya amewapongeza viongozi wa Mahakama kwa utendaji kazi mzuri unaoridhisha.

Mhe. Mtulya ametoa pongezi hizo hivi karibuni katika kikao cha menejimenti cha Mahakama katika Kanda hiyo kilichofanyika katika ukumbi wa wazi wa Mahakama mpya ya Wilaya Rorya.

Jaji Mfawidhi huyo amesisitiza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) hasa wakati huu ambapo Mahakama zote za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya zinaelekea kuanza matumizi ya ofisi mtandao.

Ameelekeza Mahakama zote kuwa na mfumo wa Key Word Classification na kuuzingatia ili kutokwamisha matumizi ya ofisi mtandao pale yatakapoanza kwani uongozi wa Kanda hautomvumilia mtumishi yeyote atakayekuwa kikwazo.

Katika kikao kazi hicho ilifanyika pia tathmini ya maadhimisho ya Wiki na Siku ya Sheria nchini kwa mwaka 2023 ambapo Mhe. Mtulya alionyesha kuridhishwa jinsi watumishi wa kada mbalimbali walivyoshiriki.

“Nimeridhishwa sana na namna watumishi wote walivyojitolea kwa hali na mali kufanikisha maadhimisho hayo, hii ni ishara nzuri ya umoja (team work),” alisema.

Kadhalika, amewapongeza watumishi hao kwa kuonyesha upendo kwa jamii, kuwajali na kuwafikia watu wenye mahitaji maalumu katika Wiki ya Sheria.

Akiongea katika kikao hicho, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma, Mhe. Frank Moshi alisisitiza kila Mahakama ndani ya Kanda hiyo kuhakikisha inamaliza mashauri yake kwa wakati na kutozalisha mashauri ya mlundikano (backlog).

Naye Mtendaji wa Mahakama katika Kanda ya Musoma, Bw. Festo Chonya aliwasilisha taarifa kuhusu ukarabati wa Mahakama ya Mwanzo Kenkombyo iliyoko katika Wilaya ya Bunda.

Katika kikao hicho wajumbe walionesha kuridhishwa na taarifa hiyo. Bw. Chonya pia alisisitiza katika taarifa yake kuhusu upandaji miti na uwekaji wa vigingi katika viwanja vya Mahakama ili kulinda mipaka ya maeneo hayo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (picha juu na chini aliyesimama) akiongea jambo wakati wa kikao cha menejimenti Kanda ya Musoma. Wengine katika picha ya chini ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Musoma, Mhe. Frank Moshi (kulia) na Mtendaji wa Mahakama katika Kanda ya Musoma, Bw. Festo Chonya (kushoto).

Wajumbe wa kikao wakisikiliza kwa makini hoja za Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma, Mhe. Erick Marley wakati wa kikao hicho.
Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Musoma, Bw. Festo Chonya akifurahia jambo alipokuwa anawasilisha taarifa ya ukarabati wa Mahakama ya Mwanzo Kenkombyo.
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Rorya, Mhe. Tumaini Marwa akisisitiza jambo wakati wa kikao hicho. Aliwashukuru wajumbe kwa kufanya kikao katika Mahakama hiyo mpya.
Picha za jengo la Mahakama ya Mwanzo Kenkombyo iliyoko katika Wilaya ya Bunda (juu na chini) kabla ya ukarabati.

Picha ya jengo la Mahakama ya Mwanzo Kenkombyo baada ya ukarabati.
Picha ya pamoja ya wajumbe wa kikao cha menejimenti Kanda ya Musoma.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam).

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni