Jumatatu, 27 Februari 2023

JAJI MFAWIDHI MOROGORO AHIMIZA WAENDESHA MASHTAKA, WAPELELEZI KUTEKELEZA WAJIBU WAO

·Awataka kuzingatia weledi usiotia shaka

·Asema Mahakama haiwezi kufanya maajabu kwa ushahidi dhaifu

Na Faustine Kapama –Mahakama, Morogoro

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe amewahimiza waendesha mashitaka na wapelelezi kote nchini kutekeleza majukumu yao kikamilifu kwa vile Mahakama haiwezi kufanya maajabu, ikiwemo kumtia hatiani mhalifu kwa kuletewa shahidi dhaifu.

Mhe. Ngwembe ametoa wito huo leo tarehe 27 Februari, 2023 alipokuwa anafungua mafunzo katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro yaliyoandaliwa na Mahakama ya Tanzania, kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), kwa washiriki 250 ambao ni waendesha mashtaka na wapelelezi kutoka taasisi mbalimbali. Mafunzo hayo yamefadhiliwa na Benki ya Dunia kupitia mradi wa maboresho awamu ya pili.

Amesema jamii huwa haiielewi Mahakama hata kidogo na tena hudhihakiwa pale ambapo jamii inaamini mtu aliyeshitakiwa ni mhalifu na imeshuhudia akitenda uhalifu, lakini anaachiwa. Amewaeleza washiriki hao wa mafunzo kuwa katika mazingira hayo, chombo kinacholaumiwa ni Mahakama, jambo ambalo halipendezi hata kidogo mbele ya macho ya jamii.

“Lakini Mahakama ifanye nini kama hakuna ushahudi wa kuweza kumhusisha mtuhumiwa na uhalifu anaotuhumiwa nao. Kama upande wa mashtaka umeshindwa kuleta mashahidi wa msingi, Mahakama ifanye miujiza gani. Lakini pia, upande wa mashtaka utaendesha vipi shauri kama upelelezi haukufanywa kama inavyotakiwa. Mwisho wa yote, mchakato mzima wa haki jinai utakuwa kituko mbele ya jamii,” alionya.

Mhe. Ngwembe ameeleza kuwa uwepo wa mafunzo hayo ni majibu ya kilio cha Mahakama cha muda mrefu dhidi ya udhaifu wa uendeshaji wa mashauri ya jinai unatokana na udhaifu wa upelelezi. Ametumia nafasi hiyo kutoa shukrani za pekee kwa Benki ya Dunia ambao chini ya mradi wa kuimarisha upatikanaji haki unaomlenga mwananchi (Citizen Centric Project -CCP) umewezesha, pamoja na mambo mengine, kufanyika kwa mafunzo hayo.

Jaji Mfawidhi huyo ameeleza pia kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025, pamoja na mambo mengine, inalenga kuwepo kwa mazingira ya amani, usalama na umoja; utawala bora na utawala wa sheria; uwepo wa jamii iliyoelimika na inayojifunza na kujenga uchumi imara na shindani.

Sambamba na hilo, amesema Mahakama imejiwekea dhima ya kufanikisha umalizaji wa mashauri kikamilifu na kwa tija, hivyo upatikanaji haki kwa wakati sio tu utaimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama, lakini pia vyombo vya haki jinai na kuwepo kwa misingi bora ya amani na utulivu.

“Ni Imani yangu kwamba haki jinai haiwezi kupatikana bila kuhakikisha tuna wapelelezi wenye ujuzi na weledi usio tia shaka na wako tayari kutumia ujuzi huo kuhakikisha wale tu wanaotuhumiwa kufanya makosa wanafikishwa mahakamani na haki yao wanaipata,” Mhe. Ngwembe alisema.  

Amebainisha pia kuwa upelelezi na uendeshaji wa makosa ya jinai ni wa kisayansi zaidi kuliko hisia na nadharia za kizamani na makosa mengi yanathibitishwa kisayansi kwa kutumia ama DNA, vipimo vya kidaktari au kwa kutumia wataalam wa utambuzi wa maandishi.

“Lazima nisema hapa kwamba siridhishwi na makosa mengi yanayofikishwa mahakamani bila kuwa na upelelezi ulio kamilika, au kumkamata mtuhumiwa na kumshikilia kwenye vituo vya polisi bila kuwepo kwa upelelezi wa dhati unao mhusisha mtuhumiwa,” Jaji Mfawidhi huyo aliwaeleza washiriki hao wa mafunzo.

Amesema makosa yenye adhabu ya vifungo vya muda mrefu kama ubakaji, ulawiti na mahusiano yaliyo haramishwa kwa sharia, yaani incest by male, wakati mwingine yametumika kudhalilisha watu wasio na hatia, hata ugomvi wa kifamilia hupelekea kuhusisha makosa ya namna hiyo.

“Pia tumeshuhudia matumizi mabaya ya vipimo vya kitaalam kwa kuwatumia watu wasio na utaalam wa kutosha.  Nashawishika kutoa ushauri kwa Serikali au Bunge kutunga kanuni na vigezo vya wataalamu wanao weza kutoa ushauri wa kitaalamu ambao utakubaliwa na Mahakama, kama walivyofanya India.  Hivyo kuwepo kwa mafunzo kama haya ni ukombozi katika tasnia ya haki jinai nchini,” alisema.

Mhe. Ngwembe alieleza pia kuwa anatambua Kifungu cha 9 (1) (e) cha Sheria ya Mashtaka ya Taifa kinatoa mamlaka kwa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka kusimamia zoezi la upelelezi kwa kuelekeza na kuongoza polisi na vyombo vingine vya upelelezi, pamoja na mambo mengine, katika kupeleleza taarifa yoyote ihusuyo jinai na kutoa taarifa haraka iwezekanavyo.

“Kwa uzoefu mashauri yanayochelewa kwenye upelelezi ni pamoja na mashauri ya mauaji. Ipo mifano kwamba, ushahidi uliopatikana wakati upelelezi wa makosa makubwa yakiwemo ya mauaji ulipatikana ndani ya wastani wa siku 90, lakini zaidi ya siku 240 zilitumika kwenye mawasiliano kati ya Ofisi ya Taifa ya Mashtaka na vyombo vya uchunguzi kwenye masuala mengine ambayo hayakugusa ushahidi. Ni vema kujifunza namna ya kupunguza hali hiyo,” Jaji Mfawidhi huyo alishauri.  

Awali akimkaribisha Jaji Mfawidhi huyo kufungua mafunzo hayo, Naibu Msajili Mwandamizi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Arnold Kirekiano alizitaja taasisi zinazoshiriki mafunzo hayo ni Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Jeshi la Polisi, Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori na Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu.

Alieleza kuwa washiriki katika mafunzo hayo kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka ni 50, wapo 100 kuutoka Jeshi la Polisi, 40 kutoka TAKUKURU, 35 kutoka TAWA, 16 kutoka Mamlaka ya Kupambana na Dawa za kulevya, tisa kutoka kitngo cha kupambana na fedha haramu.

“Tunaamini kwamba kwa ushirikiano wa wadau ambao Mahakama inashirikiana nao kupitia ofisi ya Msajili wa Mahakama Kuu tutapata nafasi tena wakati mwingine ya kuangalia mafunzo siyo tu kwa wadau wengine lakini pia hata katika maeneo ya kijiografia ambayo pengine hayakuguswa katika mafunzo haya,” alisema.

Naye Mratibu wa Mafunzo kutoka IJA, Mhe. Raymond Kaswaga ameeleza kuwa mafunzo hayo ya wiki nne yamewaleta pamoja washiriki hao ili waweze kubadilishana uzoefu kuhusu utendaji kazi wao wa kila siku, ikiwemo changamoto zinazotokana na kukua kwa teknoloji na kubadilika kwa mbinu za uhalkifu na wahalifu.

Amesema kuandaliwa kwa mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa maboresho ya Mahakama ambayo yanatekelezwa kupitia Mpango Mkakati wake wa miaka mitano (2021-203/2024) na ni utekelezaji pia wa Sera ya Mafunzo ya Taifa 2003 pamoja na Sera ya Mafunzo ya kimahakama 2019. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe akizungumza wakati anafungua mafunzo ya wiki nne ambayo yamewaleta pamoja waendesha mashitaka na wapelelezi kutoka taasisi mbalimbali. Mafunzo hayo yanafanyika katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro.
Naibu Msajili Mwandamizi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Arnold Kirekiano akisisitiza jambo kabla ya kumkaribisha Jaji Mfawidhi kufungua mafunzo hayo.
Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Mhe. Raymond Kaswaga akitoa neno la utangulizi.
Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo (juu na chini) wakifuatilia uwasilishaji wa mada mbalimbali .

Sehemu nyingine ya washiriki wa mafunzo hayo (juu na chini) ikifuatilia uwasilishaji wa mada mbalimbali.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati). Wengine kutoka kulia ni Mkurugenzi wa Operesheni na Mafunzo, Pams Foundation, Bw. Samson Kassala, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Gabriel Malata, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Awamu Mbagwa na Naibu Msajili Mwandamizi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Arnold Kirekiano.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya waendesha mashtaka wanaoshiriki mafunzo hayo.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wapelelezi kutoka Jeshi la Polisi wanaoshiriki wa mafunzo.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wapelelezi na waendesha mashtaka kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana Rushwa  wanaoshiriki wa mafunzo.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wapelelezi kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori wanaoshiriki mafunzo hayo.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wapelelezi kutoka  Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, wanaoshiriki wa mafunzo hayo.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa sekretarieti.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni