Jumatano, 8 Februari 2023

JAJI MKUU, VIONGOZI WA TAWJA WAKUTANA

Na Magreth Kinabo –Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 8 Februari, 2023 amekutana na uongozi mpya wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) na kuahidi kuendeleza ushirikiano uliopo ili chama hicho kiweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu.

Sehemu ya uongozi huo chini ya Mwenyekiti wake, ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Barke Sehel, ulifika ofisini kwa Jaji Mkuu jijini Dar es Salaam majira ya asubuhi, lengo kuu likiwa kujitambulisha na kupokea maelekezo mengine katika kuendeleza chama hicho.

Akizungumza na uongozi huo, Jaji Mkuu ameahidi kuendeleza ushirikiano na chama hicho kwa kuzingatia umuhimu wake katika Mahakama ya Tanzania. Amekishauri chama hicho kufanya utafiti kwenye masuala mbalimbali, ikiwemo usawa wa kijinsia.

 “Niko tayari kuendelea kushirikiana nanyi, mnafanya kazi nzuri kwa maendeleo ya Mahakama ya Tanzania. Nawashauri mfanye tafiti katika hili eneo la usawa wa kijinsia na tupo tayari kuwasaidia,” alisema.

Amekihakikishia Chama hicho kuwa kitaendelea kutekeleza majukumu yake bila kuingiliwa na mtu yoyote. “Fanyeni kazi zenu kwa uhuru, hamtaingiliwa na mtu yoyote,” alisema.

Kadhalika, Jaji Mkuu amekishauri Chama hicho kuangalia uwezekano wa kuijumuisha Zanzibar katika uongozi kwa kuzingatia mfumo wa uchaguzi uliopo kwa sasa hautoi nafasi kubwa kwa wajumbe kutoka visiwani kuchaguliwa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TAWJA alimshukuru Jaji Mkuu kwa ushirikiano aliouonyesha. Ameahidi kuwa wapo tayari kufanya utafiti kama alivyoshauri kwa kuwa nguvu kazi wanayo. Aidha, uongozi huo umeahidi kushughulikia suala la uwakilishi wa uongozi kutoka Zanzibar.

Katika utambulisho huo, Mhe. Sehel aliongozana na viongozi wengine, wakiwemo Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Dkt. Zainabu Mango, ambaye ni Katibu, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Martha Mpaze, ambaye ni Katibu Mwenezi na Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama kutoka Kibaha, Mhe. Nabrike Mbaba, ambaye ni Mweka Hazina.

Hivi karibuni, TAWJA ilifanya uchaguzi wa viongozi katika ngazi ya taifa. Viongozi wengine waliochaguliwa katika chama hicho walikuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Victoria Nongwa, ambaye ni Makamu Mwenyekiti, Mhe. Patricia Lusinda kama Katibu Msaidizi na Mhe. Pamela Meena ambaye ni Katibu Mwenezi Msaidizi. Viongozi hao watadumu katika nafasi hizo kwa kipindi cha miaka miwili. 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (juu na chini) akizungumza na viongozi wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) ambao wamemtembelea leo tarehe 8 Februari, 2023 ofisini kwake jijini Dar es Salaam.

Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Barke Sehel, ambaye ni Mwenyekiti wa TAWJA (juu na chini) akifafanua jambo alipokuwa anazungumza na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ofisini kwake.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) akiwasikiliza viongozi wa TAWJA waliofika ofisini kwake kujitambulisha.
Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Barke Sehel, ambaye ni Mwenyekiti wa TAWJA akisaini kitabu cha wageni ofisini kwa Jaji Mkuu.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Dkt. Zainabu Mango, ambaye ni Katibu, akisaini kitabu cha wageni.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Martha Mpaze, ambaye ni Katibu Mwenezi akisaini kitabu hicho.

Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama kutoka Kibaha, Mhe. Nabrike Mbaba, ambaye ni Mweka Hazina akisaini kitabu cha wageni akiwa ofisini kwa Jaji Mkuu wa Tanzania.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wakuu wa TAWJA. Kushoto ni Mwenyekiti, ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Barke Sehel na kulia ni Katibu, ambaye ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Zainab Mango.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa TAWJA waliofika ofisini kwake kujitambulisha. Kutoka kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Martha Mpaze (Katibu Mwenezi), Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Barke Sehel (Mwenyekiti), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Zainab Mango (Katibu) na Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama kutoka Kibaha, Mhe. Nabrike Mbaba (Mweka Hazina).

(Picha na Faustine Kapama-Mahakama)

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama Dar es Salaam.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni