Na Mwandishi wetu-Mahakama
Wakili wa Kujitegemea,
Msomi Capt. Ibrahim Bendera amewaomba wananchi kutatua migogoro waliyonayo kwa
njia ya usuluhishi kwani kukumbilia mahakamani kuna madhira mengi, ikiwemo kutumia
muda mwingi na huanzisha vita baina ya wadaawa.
Katika utenzi wake
ulioimbwa katika maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika Mahakama ya
Hakimu Mkazi Kisutu kwa Kanda ya Dar es Salaam hivi karibuni, Msomi Bendera amewaalika
wananchi kukutana na kupatana, kufanya vinginevyo kunaweza kuendeleza mgogoro
na chuki.
Sehemu ya Utenzi huo inasema,
“Madhila mnayapata, Kwanza ni muda kupita, Pili kuanzisha vita, Kesi
kuishindania. Nenda rudi isokwisha, Chuki nzito kupandisha, Yauongeza
mshawasha, Kesi kuishindania. Uchumi utapwelea, Uendelevu kupotea, Na muda
mtauchezea, Kesi kuishindania.”
Msomi Bendera anaendelea
kueleza, “Njooni tuwapatanishe, Mje tuwashirikishe, Mje tuwaunganishe, Kesi
kuishindania. Ni bora usuluhishi, Bila kuweka uzushi, Ni kwa amani mtaishi, Usuluhishi
kutumia. Msipo usuluhisha, Mgogoro hautokwisha, Na chuki mtajivisha, Usuluhishi
kutumia.”
Kwenye utenzi huo ulioimbwa na wanafunzi wa Shule ya Msingi Lioness Miburani
kutoka Temeke, Wakili huyo amewasihi wananchi kuanza na usuluhishi kwanza pale wanaposhindana kwa vile
taratibu zilizopo, zikiwemo za kimira zinahimiza kupatana na siyo kugombana.
Akawahimiza wanasheria wenzake, kama wadau muhimu, kuwa katika mstari
wa mbele kutumia usuluhishi wakati wa kutatua migogoro. Katika kukazia msimamo
huo, Msomi Bendera anasema, “Wadau wa Mahakama, Wapo na wamesimama, Twashirikiana
mema, Ya haki kusimamia. Wadau ni kina nani? Mawakili namba wani, Na wale serikalini,
Ya haki kusimamia.”
Watanzania hivi karibuni waliadhimisha Siku ya Sheria kote nchini kama
ishara ya kuanza mwaka mpya wa shughuli za kimahakama, huku ujumbe mkuu
ukiwahimiza wananchi kupeleka mahakamani migogoro ambayo imeshindikana
kukatuliwa kwa njia ya usuluhishi.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni