Jumamosi, 11 Februari 2023

JAJI MKUU WA TANZANIA AMTEMBELEA RAIS WA ZANZIBAR

Na Faustine Kapama-Mahakama, Zanzibar

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 11 Februari, 2023 amemtembelea Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi katika Ikulu ya Zanzibar na kuzungumza naye masuala mbalimbali, ikiwemo uboreshaji wa huduma za utoaji haki unaoendelea kutekelezwa na Mahakama ya Tanzania.

Mhe. Prof. Juma na viongozi wengine walioambatana naye waliwasili katika Ikulu Zanzibar majira ya saa 4.00 asubuhi na kupokelewa vizuri na mwenyeji wake. Baada ya utambulisho uliofanywa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Jaji Mkuu aliwasilisha salamu kwa mwenyeji wake na kuainisha mambo manane yaliyokuwa yanahitajika kutafutiwa ufumbuzi, kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Tume ya Jaji Mark Bomani mwaka 1993.

Aliyataja mambo hayo ambayo yanayohusu ucheleweshaji wa utatuzi wa migogoro, wananchi kupata fursa ya kupata haki, rushwa na maadili, uharaka wa kutoa uamuzi, imani ya wananchi kwa vyombo vya utoaji haki, uwezo wa wanaopewa dhamana ya kuwa Majaji, Mahakimu, Mawakili na wengine, uchache wa watoa huduma kwa kulinganisha na mahitaji yaliyopo na mazingira au miundombinu ya kutendea kazi.

 "Sisi Mahakama baada ya kuona matatizo ni makubwa tukaona ni vema tubadilishe mwelekeo kwa kuanzisha maboresho ambayo tunaendelea nayo sasa. Kabla ya kufanya hivyo tulifanya self-diagnosis ambapo Taasisi ya REPOA ilifanya tathimini na kwa kupitia tathimini hiyo Mahakama iliandaa Mpango Mkakati wake wa awamu ya Kwanza," Jaji Mkuu alimweleza Rais Mwinyi.

Alibainisha kuwa Mahakama imekuwa ikiboresha huduma zake tangu uhuru ili kutekeleza lengo lake kuu la kikatiba katika kutenda haki, lakini changamoto kubwa wanayokutana nayo ni namna ya kujipanga katika kutoa haki kwa wananchi.

Baada ya kuwasilisha salamu hizo, Mtendaji Mkuu aliwakaribisha maafisa wengine wa Mahakama ya Tanzania, akiwemo Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha na Kaimu Mkurugenzi wa TEHAMA, Bw. Allan Machela kuwasilisha namna Mahakama ilivyojipanga kukabiliana na changamoto hiyo.

Rais Mwinyi alionyesha kufurahishwa na jitihada zinazofanywa na kuhimiza Mahakama ya Zanzibar kutafuta namna ya kufuata mfumo huo ambao Mahakama ya Tanzania imeshaanza nao ili na wao waweze kupiga hatua kama wenzao waliyofikia.

Kabla ya kuhitimisha mazungumzo hayo, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania alisisitiza umuhimu wa kuwekeza nguvu kubwa katika kuitangaza Mahakama kwani maboresho mengi na makubwa yamefanyika katika Mhimili wa Mahakama lakini bado haijajajulikana kwa wananchi.

Prof. Ole Gabriel alibainisha pia kuwa kutoka na mabadiliko yanayoendelea duniani bila maboresho na matumizi ya TEHAMA, Mahakama haiwezi kufanya chochote. Kadhalika, alimweleza Rais Mwinyi kuwa mahusiano yaliyopo kati ya pande mbili za Mahakama ni mazuri, akagusia ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Pemba ambacho kinatarajiwa kukamilika ifikapo Juni 2024.

Akihitimisha mazungumzo hayo, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe.  Khamis Ramadhan Abdalla ameshukuru ushirikiano unaoendelea kushamiri wa Mahakama pande zote mbili. Amesema suala la kusarifu mifumo ya TEHAMA iliyopo ya Mahakama ya Tanzania litapewa kipaumbele ili kuhakikisha Mahakama ya Zanzibar inatumia mifumo hiyo.

Jaji Mkuu huyo alibainisha pia kuwa maboresho ya Mahakama ya Zanzibar yameanza na kwa sasa wanaandaa Mpango Mkakati wa Mahakama ili kuhakikisha azma iliyopo inatekelezwa.

Katika ziara hiyo, Jaji Mkuu wa Tanzania aliongoza na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha, Kaimu Mkurugenzi wa TEHAMA, Bw. Allan Machela na Afisa kutoka Kitengo cha Maboresho Mhe. John Chacha.

Waliohudhuria hafla hiyo kwa upande wa Zanzibar ni Jaji Mkuu, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. George Kazi, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Bw. Kai Mbaruk na Mrajisi, Bi. Valentine Katema.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kushoto) akimkabidhi zawadi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi alipomtembelea  leo tarehe 11 Februari, 2023 katika Ikulu ya Zanzibar.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) akisisitiza jambo alipokuwa anatoa salamu kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi alipomtembelea ofisini kwake katika Ikulu ya Zanzibar leo tarehe 11 Februari, 2023. Kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani. Picha chini Jaji Mkuu akiendelea kutoa salamu zake kwa Rais wa Zanzibar.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akisisitiza jambo alipokuwa anaongea wakati Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alipomtembelea Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi leo tarehe 11 Februari, 2023 Ikulu ya Zanzibar
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma akiwasilisha kwa ufupi kuhusu  mfumo wa TanzLii mbele ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi.

Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania akitoa maelezo mafupi mbele ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi kuhusu maboresho mbalimbali ambayo yanaendelea kufanywa na Mahakama ya Tanzania katika kuboresha huduma za utoaji haki nchini.

Viongozi wa Mahakama Zanzibar, akiwemo Jaji Mkuu, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (kushoto) wakifuatilia mambo mbalimbali kwenye hafla hiyo. Wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. George Kazi (wa pili kulia), Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Bw. Kai Mbaruk ( wa pili kushoto) na Mrajisi, Bi. Valentine Katema (kulia).
Sehemu ya watumishi wa Ikulu Zanzibar wakifuatilia matukio mbalimbali.

Viongozi wa Mahakama ya Tanzania wakichukua kumbukumbu wakati wa hafla hiyo.







Hakuna maoni:

Chapisha Maoni