Jumamosi, 11 Februari 2023

MNA KILA SABABU YA KUJIVUNIA MAFANIKIO MLIYOPATA: RAIS MWINYI

·Asema maboresho yaliyofanywa ni mapinduzi katika mfumo wa utoaji haki

Na Faustine Kapama-Mahakama, Zanzibar

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa hatua iliyochukua na kufikia mafanikio makubwa katika kuboresha huduma za utoaji haki kwa wananchi.

Mhe. Dkt. Mwinyi ametoa pongezi hizo leo tarehe 11 Februari, 2023 katika Ikulu ya Zanzibar alipotembelewa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma pamoja na viongozi wengine waandamizi wa Mahakama ya Tanzania.

Mna kila sababu ya kujivunia mafanikio makubwa ambayo mmeyapata,” Rais Mwinyi alisema na kumwelekeza Jaji Mkuu wa Zanzibar, “Kwa sehemu kubwa to adopt mfumo huu ambao wenzetu wameshaanza nao ili na sisi tuweze kupiga hatua kama ambayo wao wamefika.”

Rais wa Zanzibar ameonyesha kuridhishwa na mifumo ya utoaji haki inayoendelea kutekelezwa na Mahakama ya Tanzania, ikiwemo mfumo wa kusajili mashauri kwa njia ya mtandao, kupandisha nakala za hukumu kwenye mfumo maalumu wa Tanzlii, kuanzisha Mahakama inayotembea, ili kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati.

“Hii mifumo yote, kuanzia huu wa TanzLii, e-ofice, mobile court na mingine mingi inaonekana ndiyo moja ya sababu kubwa ya mafanikio haya, kwa hiyo lazima na sisi twende huko, (...) tuchukue yote ambayo yamefanyika huko yakaonyesha mafanikio, (....) haya ni mapinduzi makubwa katika mfumo mzima,” alisema.

Amebainisha kuwa alipoingia madarakani alitambua kufanya maboresho kwenye Serikali pekee hakutasaidia, hivyo aliwaita wenzake na kukaa na Jaji Mkuu na kuagiza uboreshaji kufanyika ndani ya Mahakama, akiamini ndiyo njia pekee itakayoifanya nchi kusonga mbele kimaendeleo.

Rais Mwinyi alielezea furaha yake kwa Mahakama upande wa Zanzibar baada ya kulichukulia suala hilo kwa uzito wake na wameanza kufanya maboresho makubwa. “Wananipa taarifa kwamba mnashirikiana kwa karibu, niseme tu kwamba kama kuna sekta katika muungano wetu yenye ushirikiano wa karibu ni Mahakama kuliko sekta zingine, bila shaka inatokana na watendaji waliopo,” alisema.

Mhe. Dkt. Mwinyi aliendelea kusema, “Sasa sina uhakika, au tuombe Mungu muendelee kuwepo, maana wakati mwingine kama hakuna mfumo wa kufanya mtu anayeingia asiwe na hiari mara nyingi mambo yanaweza kurudi nyuma kwa sababu tu kaja mtu mwingine, lakini tuombe kwamba hii iliyoanza itengenezewe mfumo ili tusirudi nyuma.”

Ameahidi kuendelea kuiwezesha Mahakama ya Zanzibar hasa kwenye maeneo ya kuimarisha miundombinu ya majengo na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ambayo amesema ni muhimu katika kuboresha na kuharakisha huduma za utoaji haki kwa wananchi.

Amepongeza hatua zilizochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kujenga Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Pemba, jambo ambalo litasaidia kupunguza gharama katika Serikali yake ya kujenga miundombinu hiyo.

“Tunashukuru sana kwa ushirikiano mkubwa mnaowapa wenzenu wa Zanzibar na sisi kama Serikali tunaahidi kwa yale yote ambayo yanahitaji msukumo wa Serikali tutakuwa tayari kuyafanya,” alimwambia Jaji Mkuu wa Tanzania pamoja na viongozi wengine wa Mahakama alioambatana nao.  

Viongozi wengine ambao waliambatana na Mhe. Prof. Juma kumtembelea Rais Mwinyi ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha, Kaimu Mkurugenzi wa TEHAMA, Bw. Allan Machela na Afisa kutoka Kitengo cha Maboresho Mhe. John Chacha.

Waliohudhuria hafla hiyo kwa upande wa Zanzibar ni Jaji Mkuu, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. George Kazi, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Bw. Kai Mbaruk na Mrajisi, Bi. Valentine Katema.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (juu na chini) akisisitiza jambo alipokuwa anaongea na Ujumbe wa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ambao umemtembelea leo tarehe 11 Februari, 2023 Ikulu ya Zanzibar.



Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma baada ya mazungumzo na ujumbe wake.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Dkt. Angelo Rumisha.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Dkt. Angelo Rumisha (kushoto) na Kaimu Mkurugenzi wa TEHAMA, Bw. Allan Machela.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa Mahakama ya Tanzania.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Meza Kuu ambao ni Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (wa pili kushoto), Jaji Mkuu wa Zanzibar,  Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (wa pili kulia), Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (kushoto) na Jaji wa Mahakama Kuu Zanzibar, Mhe. George Kazi (kulia).
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Meza Kuu na viongozi wa Mahakama ya Tanzania na Zanzibar baada ya mazungumzo yao.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni